crc - kiswahili version
TRANSCRIPT
MKATABA WA HAKI ZA WATOTOBARAZA KUU LA UMOJA WA MATAIFA
WARAKA NAMBARI A/RE/44/25 (DESEMBA 12, 1989)
PAMOJA NA KIAMBATISHO
Baraza Kuu,
Likirejea maazimio yake ya nyuma, hasa maazimio nambari 33/166 la tarehe 20 Disemba 1979 na 43/112 la tarehe 8 Disemba 1998, na yale ya Tume ya Haki za Binadamu na Halmashauri ya Uchumi na Jamii kuhusiana na mapatano ya haki za watoto.
Likizingatia hasa azimio kuhusu haki za mtoto nambari 1989/57 la tarehe 8 Machi, 1989 ambapo tume iliamua kupitisha rasimu ya mapatano kuhusu haki za mtoto kwa Halmashauri ya Uchumi na Jamii nambari 198/79 la tarehe 24 Mei 1989,
Likitangaza kwa mara nyingine kwamba haki za watoto zinahitaji ulinzi wa kipekee na muafaka, na wito wa kuziboresha mara kwa mara hali za watoto ulimwenguni kote na pia kwa maendeleo yao na elimu katika hali ya amani na usalama,Likijua kwa hakika kwamba hali ya watoto katika sehemu mbalimbali duniani imeendelea kuwa mbaya kutokana na hali za kijamii zisizoridhisha, majanga ya asili, migogoro inayohusisha matumizi ya silaha, unyonyaji, ujinga, njaa na ulemavu na likiridhika kwamba hatua za haraka na muafaka za kitaifa na kimataifa zinahitajika;
Likitambua jukumu la Shirika la Umoja wa Mataifa la Watoto (UNICEF)na lile la Umoja wa Mataifa katika kukuza Ustawi wa Watoto na Maendeleo yao;
Likiridhika kwamba mapatano ya kimataifa kuhusu haki za mtoto, kama sehemu ya mafanikio ya Umoja wa Mataifa katika nyanja ya haki za binadamu, yatatoa mchango muhimu katika kulinda haki za watoto na kuhakikisha ustawi wao,
Likitambua kwamba mwaka wa 1989 yanaadhimisha mwaka wa 30 wa Azimio la haki za watoto na pia mwaka wa 10 wa mwaka wa Kimataifa wa mtoto,
1. Linaishukuru Tume ya Haki za Binadamu kwa kumaliza mjadala kuhusu mapendekezo ya Mapatano kuhusu Haki za Mtoto
2. Linaukubali na kukaribisha utiaji saini, kuridhia na kukubali Mapatano kuhusu Haki za Mtoto uliopo kwenye kiambatanisho kwenye azimio la sasa.
3. Linatilia wito kwa wanachama wote wa Umoja wa Mataifa kufikiria kuyatilia saini na kuyaridhia au kuyakubali mapatano haya kama kipaumbele na Baraza Kuu lina matumaini kwamba utaanza kutumika hivi karibuni.
4. Linamsihi Katibu Mkuu kuhakikisha upatikanaji wa vifaa vyote na msaada unaohitajika katika kutoa taarifa kuhusu mapatano.
5. Linakaribisha taasisi na mashirika ya Umoja wa Mataifa pamoja na mashirika ya kiserikali na yale yasiyo ya kiserikali kuzidisha juhudi zao kwa nia ya kueneza taarifa kuhusu mapatano haya na kusaidia katika kueleweka kwake.
6. Linamsihi Katibu kuwasilisha mbele ya Baraza Kuu katika kikao chake cha 45 taarifa kuhusu hadhi ya mapatano kuhusu Haki za Mtoto.
7. Linaamua kuifikiria taarifa ya Katibu Mkuu katika kikao chake cha 45 chini ya kichwa cha somo “Utekelezaji wa Mapatano kuhusu Haki za Mtoto”
Mkutano wa 61 wa wanachama wote
Novemba 20, 1989
1
Mkataba wa
Haki za WatotoMkataba wa Haki za Mtoto ulipitishwa na kufunguliwa kwa ajili ya kutiwa saini, kuridhiwa na kuzingatiwa kupitia azimio 44/25 la Mkutano Mkuu la Novemba 20, 1989. Ulianza kutekelezwa Septemba 2, 1990, kulingana na kifungu 49. Umeridhiwa na nchi 191.
Dibaji
Nchi Wanachama katika Mkataba wa sasa,
Kwa kuzingatia kwamba, kulingana na kanuni zilizobainishwa katika Mkataba wa Umoja wa Mataifa, kutambua heshima na haki sawa za kimsingi kwa binadamu wote ndio msingi wa uhuru, haki na amani duniani,
Kwa kujua kwamba watu wa Umoja wa Mataifa, katika Mkataba wao, wamethibitisha imani yao kuhusu haki za msingi za binadamu na heshima na thamani ya kila binadamu, na wamedhamiria kukuza maendeleo ya jamii na hali bora ya maisha kwa uhuru zaidi,
Kwa kutambua kuwa Umoja wa Mataifa, kwenye Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu na Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Binadamu, ulitamka na kukubali kwamba kila mtu ana haki ya kupewa haki na uhuru wote ulioelezwa humo bila kutofautishwa kwa namna yoyote kama rangi, jinsia, lugha, dini, siasa au mawazo mengine, taifa au asili ya kijamii, utajiri, kuzaliwa au hadhi nyingine yoyote,
Kwa kurejea katika Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu, Umoja wa Mataifa umetangaza kwamba utoto unapewa matunzo na msaada maalumu,
Kwa kukiri kuwa familia, kama ngazi ya msingi ya jamii na mazingira asili ya ukuaji na ustawi kila mmoja kwenye familia hiyo na hasa watoto, lazima ipewe ulinzi na msaada unaobidi ili iweze kutimiza kwa ukamilifu majukumu yake katika jumuiya,
Kwa kutambua kwamba ili mtoto aweze kuwa na makuzi yaliyo kamili na yenye urari katika haiba yake, lazima akue katika mazingira ya kifamilia kwa hali ya furaha, upendo na uelewa,
Kwa kuzangatia kwamba lazima mtoto ajiandae kikamilifu kuishi maisha yake mwenyewe katika jamii, na kulelewa kulingana na misingi iliyoelezwa kwenye Mkataba wa Umoja wa Mataifa, hususani kwa misingi ya amani, heshima, uvumilivu, uhuru, usawa na mshikamano,
2
Kwa kutambua kuwa haja ya kueneza matunzo maalumu kwa mtoto imeelezwa kwenye Azimio la Geneva la Haki za Mtoto la mwaka 1924 na katika Azimio la Haki za Mtoto lililopitishwa na Baraza Kuu Novemba 20, 1959 na kutambuliwa kwenye Azimio la Ulimwengu la Haki za Binadamu, Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (hasa vifungu 23 na 24), Mkataba wa Kimataifa kuhusu Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni (hasa kifungu 10) na katika sheria na kanuni za taasisi maalum na mashirika ya kimataifa yanayohusika na ustawi wa watoto,
Kwa kutambua kwamba kama inavyodhihirishwa kwenye Azimio la Haki za Mtoto, “mtoto, kutokana na kutokukomaa kwake kimwili na kiakili, anahitaji ulinzi na matunzo maalumu, ikiwa pamoja na ulinzi wa kisheria unaofaa kabla na baada ya kuzaliwa”,
Kwa kurejea vifungu vya Azimio la Kanuni za Kijamii na Kisheria vinavyohusiana na Ulinzi na Ustawi wa Watoto, kwa Kuzingatia Hasa Kuwaweka kwenye Malezi Maalumu na Kuasili Kitaifa na Kimataifa; Kanuni za Kiwango cha Chini za Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Utekelezaji wa Utoaji wa Haki za Kisheria kwa Watoto (Kanuni za Beijing); na Azimio kuhusu Ulinzi wa Wanawake na Watoto walio kwenye Dharura na Migogoro inayotumia Silaha;
Kwa kutambua kuwa, katika nchi zote duniani, kuna watoto wanaoishi katika hali ngumu sana, na kwamba watoto hao wanahitaji kufikiriwa kwa jinsi ya kipekee,
Kwa kujua umuhimu wa mila na utamaduni wa kila kundi la watu katika ulinzi na maendeleo mazuri ya mtoto,
Kwa kutambua umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kuboresha hali za maisha ya watoto katika kila nchi, hasa katika nchi zinazoendelea;
Wamekubaliana kama ifuatavyo:
SEHEMU YA KWANZA
Kifungu 1
Kulingana na Mkataba huu, mtoto ni binadamu yeyote aliye chini ya umri wa miaka 18 isipokuwa, chini ya sheria zinazomhusu mtoto ambapo umri wa ukubwa unatajwa kuwa mapema zaidi.
Kifungu 2
1. Nchi Wanachama zitaheshimu na kuhakikisha haki zilizomo kwenye Mkataba huu kwa kila mtoto aliye katika maeneo yao bila ubaguzi wa aina yoyote, bila kujali rangi, jinsi, lugha, dini, mawazo ya kisiasa au mengineyo, asili ya kikabila au kijamii, utajiri, ulemavu, uzawa au hadhi nyinginezo za mtoto au mzazi ama mlezi wake.
3
2. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa kuhakikisha kwamba mtoto analindwa dhidi ya aina zote za ubaguzi au adhabu kwa misingi ya hadhi, shughuli, mawazo yaliyotolewa au imani ya wazazi, walezi wa kisheria, au wanafamilia wa mtoto.
Kifungu 3
1. Katika vitendo vyote vinavyofanywa kuhusu watoto, viwe vimefanywa na taasisi za ustawi wa jamii zinazoendeshwa na umma au binafsi, mahakama, mamlaka za utawala au vyombo vya kutunga sheria, maslahi ya mtoto yatapewa umuhimu wa kwanza.
2. Nchi Wanachama zitajitahidi kumhakikishia mtoto ulinzi na matunzo yanayohitajika kwa ajili ya ustawi wake, kwa kuzingatia haki na wajibu wa wazazi wake, walezi wake wa kisheria au watu wengine wanaohusika naye kisheria na ili kutimiza azma hii, serikali itachukua hatua zote za kisheria na kiutawala zinazofaa.
3. Nchi Wanachama zitahakikisha kwamba taasisi, huduma na vyombo vinavyohusika na matunzo au ulinzi wa watoto vitafuata viwango vilivyowekwa na mamlaka husika, hasa kwenye maeneo ya usalama, afya, idadi na kufaa kwa watumishi wake, pamoja na usimamizi unaofaa.
Kifungu 4
Nchi Wanachama zitachukua hatua zote za kisheria, kiutawala na nyinginezo kutekeleza haki zinazobainishwa katika Mkataba huu. Kuhusiana na haki za kiuchumi, kijamii na kitamaduni, Nchi Wanachama zitachukua hatua zote kwa kadri ya uwezo wao wa raslimali zilizopo, na inapohitajika, kulingana na misingi ya ushirikiano wa kimataifa.
Kifungu 5
Nchi Wanachama zitaheshimu majukumu, haki na wajibu wa wazazi, au pale inapohusu, ndugu wa karibu au jumuiya kama inavyokubalika na desturi za watu hao, walezi wa kisheria au watu wengine wanaowajibika kisheria na mtoto, kutoa, kulingana na uwezo wa hatua ya makuzi ya mtoto, maelekezo na miongozo ya kuwapatia watoto haki zinazotambuliwa na Mkataba huu.
Kifungu 6
1. Nchi Wanachama zinatambua kwamba kila mtoto ana haki ya msingi ya kuishi.
2. Nchi Wanachama zitahakikisha uhai na maendeleo ya mtoto kwa uwezo wake wote.
Kifungu 7
1. Mtoto atasajiliwa mara tu anapozaliwa na atakuwa na haki ya kuzaliwa ya kupewa jina, haki ya kupata utaifa na, kwa kadri inavyowezekana, haki ya kuwajua na kutunzwa na wazazi wake.
4
2. Nchi Wanachama zitahakikisha utekelezaji wa haki hizi kulingana na sheria za nchi zao na wajibu wao chini ya sheria za kimataifa zinazohusu uwanja huu, hasa pale ambao vinginevyo mtoto angekosa utaifa
Kifungu cha 8
1. Nchi Wanachama zitajitahidi kuheshimu haki ya mtoto kubakia na utambulisho wake, ikiwa ni pamoja na utaifa, jina na uhusiano wa familia kama inayotambulika kisheria bila kizuizi kisichokuwa cha kisheria.
2. Pale ambapo mtoto ananyang’anywa isivyo halali baadhi ya au vipengele vyote vya utambulisho wake, Nchi Wanachama zitatoa msaada na ulinzi mwafaka, kwa nia ya kuurejesha utambulisho wake mapema inavyowezekana.
Kifungu 9
1. Nchi Wanachama zitahakikisha kwamba mtoto hatatenganishwa na wazazi wake kinyume na matakwa yao, isipokuwa pale ambapo mamlaka sahihi yenye dhamana ya kurekebisha sheria imeamua, kulingana na sheria na taratibu zinazohusika, kuwa kutengana huko ni lazima kwa ajili ya maslahi ya mtoto. Uamuzi huo unaweza kuwa wa lazima hasa katika hali maalumu kama vile unyanyasaji au kutekelezwa kwa mtoto na wazazi wake, au kama wazazi wanaishi mbalimbali na uamuzi inabidi ufanywe kuhusu makazi ya mtoto.
2. Katika hatua za kutekeleza aya 1 ya kifungu hiki, pande zote zinazohusika zitapewa nafasi ya kushiriki katika hatua hizo na kutoa maoni yao.
3. Nchi Wanachama zitaheshimu haki ya mtoto aliyetenganishwa na mzazi mmoja au wazazi wote wawili kuwa na uhusiano binafsi na kuonana moja kwa moja na wazazi wote wawili mara kwa mara, isipokuwa kama ni kinyume na maslahi ya mtoto.
4. Pale ambapo kutengana huko kunatokana na hatua yoyote iliyofanywa na Nchi Mwanachama, kama vile kuwekwa kizuizini, kifungo, uhamisho, kufukuzwa nchini au kifo (ikiwa ni pamoja na kifo kinachotokana na sababu yoyote wakati mtu huyo akiwa chini ya ulinzi wa Serikali) dhidi ya mzazi mmoja au wazazi wote wawili wa mtoto, Nchi hiyo itawajibika, ikiombwa, kutoa taarifa muhimu kwa wazazi, mtoto au, inapofaa, kwa mwanafamilia/wanafamilia wengine kuhusu mahali alipo mwanafamilia asiyekuwapo, isipokuwa kama kufanya hivyo kunaweza kuathiri ustawi wa mtoto. Nchi Wanachama zitahakikisha pia kwamba kutolewa kwa ombi hilo hakutakuwa na madhara kwa mhusika/wahusika.
Kifungu 10
1. Kulingana na wajibu wa Nchi Wanachama, chini ya kifungu 9 aya I, maombi ya mtoto au wazazi wake kuingia au kuondoka kwenye Nchi Mwanachama kwa nia ya kuungana tena kwa familia yatashughulikiwa na Nchi Mwanachama kwa nia nzuri, kibinadamu na haraka. Nchi Wanachama zitahakikisha kuwasilishwa kwa maombi kama hayo hakutakuwa na madhara yoyote kwa mwombaji na kwa wanafamilia.
2. Mtoto ambaye wazazi wake wanakaa katika Nchi tofauti atakuwa na haki ya kuendelea kuwa na uhusiano na mawasiliano ya moja kwa moja na ya mara kwa mara na wazazi wake wote wawili, isipokuwa katika hali maalumu itakayozuia kufanya hivyo. Ili kutimiza azma hii, kulingana na wajibu wa Nchi Wanachama chini ya kifungu 9, aya 2, Nchi Wanachama zitaheshimu haki ya mtoto na wazazi wake
5
kuondoka nchi yoyote; ikiwemo nchini yao wenyewe, na kuingia nchini mwao. Haki ya kuondoka katika nchi yoyote itategemea tu masharti yaliyobainishwa na sheria na ambayo ni ya lazima katika kulinda usalama wa taifa, amani ya umma, afya ya umma au maadili ama haki na uhuru wa wengine na ambayo yanaendana na haki nyingine zinazotambuliwa kwenye Mkataba huu.
Kifungu 11
1. Nchi Wanachama zitachukua hatua kupambana na uhamishaji haramu na kuwarudisha watoto kutoka nchi za nje.
2. Ili kutimiza hili, Nchi Wanachama zitaendeleza na kukamilisha makubaliano kati ya nchi mbili au zaidi ama kutekeleza makubaliano yaliyopo.
Kifungu 12
1. Nchi Wanachama zitamhakikishia mtoto mwenye uwezo wa kutoa maoni yake haki ya kutoa maoni hayo kwa uhuru katika masuala yote yanayomhusu, na mawazo ya mtoto yatapewa uzito unaostahili kulingana na umri na ukomavu wake.
2. Kwa ajili hiyo, mtoto atapewa nafasi ya kusikilizwa katika mambo ya kisheria na kiutawala yanayomhusu, kwa kuzungumza yeye mwenyewe moja kwa moja au kupitia mwakilishi au chombo mwafaka, kulingana na taratibu za sheria za nchi husika.
Kifungu 13
1. Mtoto atakuwa na uhuru wa kujieleza; haki hii itajumuisha uhuru wa kutafuta, kupokea na kutoa taarifa na mawazo ya aina zote, bila kujali mipaka, iwe kwa mazungumzo, maandishi au kuchapa, kwa njia ya sanaa, au kwa njia nyingine atakayoichagua mtoto.
2. Utekelezaji wa haki hii unaweza kuwa na mipaka, ambayo itawekwa tu kama inaelekezwa na sheria na kama ni ya lazima katika:
(a) kuheshimu haki au hadhi ya wengine; au
(b) kulinda usalama wa taifa au amani, afya ama maadili ya umma.
Kifungu 14
1. Nchi Wanachama zitaheshimu haki ya mtoto ya uhuru wa kufikiri, dhamira na dini.
2. Nchi Wanachama zitaheshimu haki na wajibu wa wazazi na pale inapohusu, walezi wa kisheria, kumwelekeza mtoto katika kutekeleza haki zake kutegemeana na uwezo wa mtoto kwenye hatua yake ya makuzi.
3. Uhuru wa kudhihirisha dini au imani yake unaweza kuwa na mipaka kama inavyobainishwa na sheria na endapo mipaka hiyo ni muhimu ili kulinda usalama wa umma, amani, afya au maadili au haki za msingi na uhuru wa wengine.
Kifungu 15
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto ya uhuru wa kujumuika na uhuru wa kukutana kwa amani.
6
2. Hakuna mipaka itakayowekwa katika utekelezaji wa haki hizi zaidi ya ile iliyowekwa kulingana na sheria na ambayo ni muhimu katika jamii ya kidemokrasia na ambayo ni ya lazima kwa usalama wa taifa au usalama ama amani ya umma, au kwa ajili ya kulinda afya au maadili ya umma, ama kulinda haki na uhuru wa wengine.
Kifungu 16
1. Hakuna mtoto atakayeingiliwa katika kuwa na usiri, familia, makazi au katika kuwasiliana, wala kuvunjiwa heshima na hadhi yake kinyume cha sheria.
2. Mtoto anayo haki ya ulinzi wa kisheria dhidi ya kuingiliwa au kuvunjiwa heshima huko.
Kifungu 17
Nchi Wanachama zinatambua kazi muhimu inayofanywa na vyombo vya habari na zitahakikisha kwamba mtoto anapata habari na mambo mengine kutoka kwenye vyanzo mbalimbali vya kitaifa na kimataifa, hasa zile zitakazolenga katika kuendeleza ustawi wake wa kijamii, kiroho na wa kimaadili na afya ya mwili na akili. Ili kufikia lengo hili, Nchi Wanachama:
(a) zitahimiza vyombo vya habari kutoa habari na vitu vingine vyenye manufaa kwa mtoto kijamii na kitamaduni kulingana na maelezo ya kifungu 29;
(b) zitahimiza ushirikiano wa kimataifa katika kutoa, kubadilishana na kusambaza habari na vitu vingine vya tamaduni mbalimbali kutokana na vyanzo vya kitaifa na kimataifa.
(c) zitahimiza utoaji na usambazaji wa vitabu vya watoto;
(d) zitahimiza vyombo vya habari kuzingatia mahitaji ya lugha ya mtoto ambaye anatoka katika kundi dogo la jamii au jamii ya asili.
(e) zitahimiza uundaji wa miongozo mwafaka kwa ajili ya kumlinda mtoto kutokana na habari na vifaa vyenye madhara kwa ustawi wake, kwa kuzingatia maelekezo ya vifungu 13 na 18.
Kifungu 18
1. Nchi Wanachama zitajitahidi kwa kadri ziwezavyo kuhakikisha kutambuliwa kwa kanuni kwamba wazazi wote wawili wana majukumu sawa katika malezi na makuzi ya mtoto. Wazazi, ama inapohusu, walezi wa kisheria, wana wajibu wa msingi katika malezi na makuzi ya mtoto. Maslahi ya mtoto yatakuwa ndio zingatio lao kuu.
2. Ili kuhakikisha na kuendeleza haki zilizo katika Mkataba huu, Nchi Wanachama zitatoa msaada unaofaa kwa wazazi au walezi wa kisheria katika utekelezaji wa majukumu yao ya kumlea mtoto na zitahakikisha uundaji wa taasisi na vyombo na utoaji wa huduma za kutunza watoto.
3. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa kuhakikisha kwamba watoto ambao wazazi wao ni wafanyakazi wanapata haki ya kunufaika na huduma na suhula za malezi ya watoto wanazostahili.
7
Kifungu 19
1. Nchi Wanachama zitakuchua hatua zote zinazofaa za kisheria, kitawala, kijamii na kielimu katika kumlinda mtoto dhidi ya aina zote za ukatili, kudhuriwa au kunyanyaswa, kutelekezwa au kutojaliwa, kutendewa visivyo au kunyonywa, ikiwa pamoja na unyanyaswaji wa kingono, wakati akiwa katika malezi ya wazazi, walezi wa kisheria au mtu mwingine yeyote anayemtunza mtoto.
2. Hatua hizo za kumlinda mtoto kwa kadri inavyofaa lazima zijumuishe kuundwa kwa taratibu sahihi za uanzishaji wa mipango ya kijamii ili kutoa msaada unaobidi kutolewa kwa mtoto na wale wanaomlea, pamoja na aina nyingine za kinga, na kwa ajili ya kutambua, kutoa taarifa, rufaa, uchunguzi, matibabu na ufuatiliaji wa matukio ya mtoto kutendewa visivyo kama ilivyokwishaelezwa, na inapobidi, kuhusisha mahakama.
Kifungu 20
1. Mtoto ambaye hayuko katika mazingira ya familia yake, kwa muda au moja kwa moja, au ambaye kwa maslahi yake hawezi kuruhusiwa kubaki katika mazingira ya familia hiyo, atakuwa na haki ya kupata ulinzi na msaada maalumu kutoka Serikalini.
2. Nchi Wanachama kwa kuzingatia sheria za nchi zao zitahakikisha mtoto huyo anapatiwa malezi mbadala.
3. Huduma kama hizo zinaweza kujumuisha kumpatia mtoto walezi, kafala ya Sheria ya Kiislamu, uasili au ikibidi kumkabidhi kwa taasisi mwafaka ya kulelea watoto. Wakati wa kufikiria maamuzi, umuhimu wa kutosha utatolewa katika kuendelea kwa malezi ya mtoto kulingana na kabila, dini, utamaduni na lugha yake.
Kifungu 21
Nchi Wanachama zitakazotambua au/na zitakazoruhusu, uasili wa mtoto zitahakikisha kwamba maslahi ya mtoto yatapewa umuhimu mkubwa na:
(a) zitahakikisha kwamba uasili wa mtoto unaruhusiwa na mamlaka mwafaka yanayoamua, kulingana na sheria na taratibu zilizopo na kwa kuzingatia taarifa zinazohusika na kuaminika, kwamba uasili wa mtoto unaruhusiwa kwa kuzingatia hali ya mtoto kuhusu wazazi, ndugu na walezi wa kisheria na kwamba, kama inahitajika wahusika hao wamekubali uasili huo kwa misingi ya kuwa na taarifa kamili na ushauri nasaha kwa kadiri itakavyobidi.
(b) zitatambua kwamba uasili wa mtoto kwenda nchi nyingine unaweza kuwa njia mbadala ya malezi ya mtoto, endapo mtoto hawezi kupatiwa walezi au familia ya kumwasili au haiwezekani katika mazingira yoyote mtoto huyo kulelewa katika nchi yake.
(c) zitahakikisha kwamba mtoto anayehusika na uasili wa kwenda nchi nyingine anapata ulinzi na kiwango cha maisha kinacholingana na kile cha uasili wa ndani ya nchi.
(d) zitachukua hatua zote zinazofaa kuhakikisha kuwa uasili wa nje ya nchi hauwapatii mapato haramu wale wanaohusika nao.
(e) zitaendeleza, pale inapofaa, madhumuni ya kifungu hiki kwa kuhitimisha mipango au makubaliano ya nchi mbili au zaidi, na zitajithidi, kwa msingi huu,
8
kuhakikisha kwamba upelekaji wa mtoto katika nchi nyingine unafanywa na mamlaka au chombo mwafaka.
Kifungu 22
1. Nchi Wanachama zitachukua hatua zinazofaa kuhakikisha kwamba mtoto anayetafuta hadhi ya ukimbizi au anayechukuliwa kama mkimbizi kulingana na sheria za kimataifa au za ndani ya nchi na taratibu zinazotumika, awe peke yake au amefuatana na wazazi wake au watu wengine, anapata ulinzi na msaada wa kibinadamu unaofaa katika kupata haki zinazobainishwa kwenye Mkataba huu na haki nyingine za binadamu za kimataifa ama mikataba mingine ambayo Nchi inashiriki.
2. Kwa ajili hiyo, Nchi Wanachama zitatoa, kama zinavyoona inafaa, ushirikiano katika jitihada zozote za Umoja wa Mataifa na mashirika mengine mwafaka yanayohusisha serikali mbalimbali au mashirika yasiyo ya kiserikali yanayoshirikiana na Umoja wa Mataifa kumlinda na kumsaidia mtoto wa aina hiyo na kuwatafuta wazazi au ndugu wengine ili kupata taarifa zitakazosaidia katika kumuunganisha tena na familia yake. Pale ambapo wazazi au ndugu wengine hawawezi kupatikana mtoto huyo atapewa ulinzi sawa na mtoto mwingine ambaye ametengwa na familia yake kwa muda au moja kwa moja kwa sababu yoyote ile, kama ilivyokubaliwa kwenye Mkataba huu.
Kifungu 23
1. Nchi Wanachama zinatambua kwamba mtoto mwenye ulemavu wa mwili au akili anastahili kuishi na kufurahia maisha kamili na mazuri, katika hali inayohamkikishia heshima, kuendeleza hali ya kujitegemea na kumwezesha ashiriki kikamilifu katika jamii.
2. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto mwenye ulemavu kupata matunzo maalumu na zitahimiza na kuhakikisha kutolewa huduma hizo, kulingana na raslimali zilizopo, kwa mtoto anayestahili pamoja na wale wanaomlea, pamoja na kuhakikikisha kuwa msaada unaoombwa unaendana na hali ya mtoto na wazazi wake ama watu wengine wanaomlea mtoto.
3. Kwa kutambua mahitaji maalum ya mtoto mwenye ulemavu, msaada unaotolewa kulingana na aya 2 ya kifungu hiki, utatolewa bure, kila inapowezekana, kwa kuzingatia uwezo wa kifedha wa wazazi au watu wengine wanaomlea, na utabuniwa kwa jinsi itakayohakikisha kwamba mtoto huyo anapata kikamilifu elimu, mafunzo, huduma za afya, huduma za kujiandaa na maisha kwenye jamii, maandalizi ya ajira na nafasi ya burudani kwa namna ambayo mtoto huyo anaweza, kulingana na ulemavu wake, kujichanganya na watu wengine na kupata maendeleo binafsi ikiwa ni pamoja na maendeleo ya kitamaduni na kiroho.
4. Nchi Wanachama zitaendeleza, kwa msingi wa ushirikiano wa kimataifa, kubadilishana habari mwafaka kwenye uwanja wa huduma za kinga ya maradhi na tiba, saikolojia na tiba ya kiutendaji ya watoto wenye ulemavu, ikiwa ni pamoja na kueneza na kupata habari kuhusu njia za kumwandaa mtoto kwa maisha kwenye jamii, elimu na mafunzo ya ufundi, kwa nia ya kuziwezesha Nchi Wanachama kuboresha uwezo na stadi zao na kuinua uzoefu wao katika maeneo haya. Ili kufikia lengo hili, umuhimu mkubwa utatolewa kwa mahitaji ya nchi zinazoendelea.
9
Kifungu 24
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto kuwa na kiwango cha juu kabisa cha afya kwa kadri inavyowezekana na kuwa na vyombo vya tiba na urudishaji wa afya katika hali inayotakiwa. Nchi Wanachama zitajitahidi kuhakikisha kwamba hakuna mtoto atakayekosa haki yake ya kupata huduma hizo za afya zinazobainishwa kwenye Mkataba huu na katika mikataba mingine ya kimataifa ya haki za binadamu au ya misaada ya kibinadamu ambayo Nchi zinashiriki.
2. Kwa sababu hiyo, Nchi Wanachama zitatoa, kama zinavyoona inafaa, ushirikiano katika jitihada zote za Umoja na Mataifa na mashirika mwafaka yanayohusisha serikali nyingi au mashirika yasiyo ya kiserikali yanayoshirikiana na Umoja wa Mataifa kumlinda na kumsaidia mtoto wa aina hiyo na kutafuta wazazi au watu wengine wa familia ya mtoto yeyote mkimbizi ili kupata taarifa muhimu zitakazosaidia kumuunganisha na familia yake. Pale ambapo wazazi au ndugu wengine hawawezi kupatikana, mtoto atapewa ulinzi sawa na mtoto mwingine yeyote aliyetenganishwa na familia yake kwa muda au moja kwa moja kwa sababu yoyote ile, kama inavyobainishwa na Mkataba huu.
Nchi Wanachama zitajitahidi kutekeleza kikamilifu haki hii, na hasa, zitachukua hatua zitakazofaa:
(a) kupunguza vifo vya watoto wachanga na watoto wadogo;
(b) kuhakikisha upatikanaji wa msaada muhimu wa tiba na huduma za afya kwa watoto wote hususan uimarishaji wa afya ya msingi;
(c) kupiga vita maradhi na utapiamlo, katika utaratibu wa afya ya msingi, kwa kutumia, pamoja na njia nyingine, teknolojia inayopatikana kwa urahisi na kwa kutoa vyakula vyenye lishe ya kutosha na maji safi ya kunywa, kwa kuzingatia hatari za uchafuzi wa mazingira;
(d) kuhakikisha huduma za afya ya mama kabla na baada ya kujifungua;
(e) kuhakikisha kwamba makundi yote ya jamii, hasa wazazi na watoto, wana taarifa, wanapata elimu na wanasaidiwa kutumia maarifa ya msingi ya afya na lishe ya mtoto, faida za kunyonyesha maziwa ya mama, usafi wa mwili na wa mazingira na kuzuia ajali;
(f) kuendeleza huduma za kinga ya maradhi, mwongozo wa wazazi na elimu na huduma ya uzazi wa mpango.
3. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa na zitakazofanikisha lengo la kukomesha mila na desturi zinazodhuru afya ya watoto.
4. Nchi Wanachama zitajitahidi kuendeleza na kuhimiza ushirikiano wa kimataifa kwa lengo la kufikia kwa utaratibu na kukamilisha malengo ya haki zinazobainishwa katika kifungu hiki. Ili kufikia lengo hili, umuhimu mkubwa utatolewa kwa mahitaji ya nchi zinazoendelea.
Kifungu 25
Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto ambaye amewekwa na mamlaka mwafaka kwa ajili ya kulelewa, kulindwa au kupewa matibabu ya afya yake ya
10
mwili ama akili, kuwa na uangalizi wa mara kwa mara wa tiba inayotolewa kwa mtoto huyo pamoja na hali nyingine zinazohusu kuwekwa kwake huko.
Kifungu 26
1. Nchi Wanachama zitatambua kwa kila mtoto kuwa na haki ya kufaidi hifadhi ya jamii, ikiwemo bima ya jamii, na zitachukua hatua zinazobidi ili kufikia malengo ya haki hii kulingana na sheria za nchi husika.
2. Mafao yatatolewa, pale inapofaa, kwa kuzingatia raslimali na hali ya mtoto na watu wenye wajibu wa kumtunza mtoto huyo, pamoja na kuzingatia mambo mengine yanayohusiana na maombi ya mafao hayo yanayofanywa na mtoto mwenyewe au mtu mwingine kwa niaba yake.
Kifungu 27
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya kila mtoto kuwa na kiwango cha maisha kinachokidhi makuzi ya mtoto kimwili, kiakili, kiroho, kimaadili na kijamii.
2. Wazazi au watu wengine wenye jukumu na mtoto wana wajibu wa msingi wa kuhakikisha, kwa uwezo wao na hali ya fedha, mazingira mwafaka yanayohitajika kwa makuzi ya mtoto.
3. Nchi Wanachama, kulingana na hali ya kitaifa na uwezo walio nao, zitachukua hatua zinazofaa kuwasaidia wazazi na watu wengine wanaohusika na mtoto kutekeleza haki hii na pale inapotakikana zitatoa msaada wa mali na kusaidia mipango hasa inayohusu lishe, mavazi na makazi.
4. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa kupata malipo kwa ajili ya matunzo ya mtoto kutoka kwa mzazi au mtu mwingine anayewajibika kifedha kwa mtoto huyo, iwe ndani au nje ya Nchi husika. Hasa pale ambapo mtu anayehusika na kumgharimia mtoto huyo anapoishi nchi nyingine tofauti na alipo mtoto, Nchi Wanachama zitasaidia kupatikana au kukamilishwa kwa makubaliano ya kimataifa, pamoja na kufanya mipango mingine inayofaa.
Kifungu 28
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto ya elimu, na ili kufikia lengo hili kwa utaratibu na kwa kuzingatia fursa sawa, zitafanya hasa yafuatayo:
(a) elimu ya msingi kuwa ya lazima na kuitoa bure kwa wote;
(b) kuhimiza kuanzishwa kwa aina mbalimbali za elimu ya sekondari, ikiwa pamoja na elimu ya jumla na ya ufundi, kuifanya ipatikane kwa kila mtoto, na kuchukua hatua zinazofaa kama vile kuanzisha elimu ya bure na kutoa msaada wa fedha pale inapohitajika;
(c) kuifanya elimu ya juu ipatikane kwa wote kwa kuzingatia uwezo kwa kila njia inayowezekana;
(d) kuhakikisha kuwepo kwa taarifa na ushauri juu ya elimu ya jumla na ya ufundi kwa watoto wote;
(e) kuchukua hatua za kuhimiza mahudhurio mazuri shuleni na kupunguza idadi ya wanaoacha shule.
11
2. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa kuhakikisha kwamba nidhamu ya shule inafanyika kwa njia ambayo inazingatia heshima ya kibinadamu ya mtoto na kulingana na Mkataba huu.
3. Nchi Wanachama zitaendeleza na kuhimiza ushirikiano wa kimataifa katika masuala yanayohusu elimu, hasa kwa nia ya kuchangia katika kukomesha ujinga na kutokujua kusoma na kuandika duniani kote na kusaidia upatikanaji wa maarifa ya kisayansi na kiufundi na matumizi ya njia za kisasa za kufundishia. Ili kufikia lengo hili, umuhimu mkubwa utatolewa kwa mahitaji ya nchi zinazoendelea.
Kifungu 29
1. Nchi Wanachama zinakubali kwamba elimu ya mtoto italenga katika:
(a) maendeleo ya haiba, vipaji na uwezo wa kiakili na kimwili wa mtoto kwa kiwango cha juu kabisa;
(b) kuendeleza heshima kwa haki za binadamu, uhuru wa msingi na misingi iliyomo katika Mkataba wa Umoja wa Mataifa;
(c) kuendeleza heshima kwa wazazi wa mtoto, utambulisho wake wa kitamaduni, lugha na maadili, kwa maadili ya taifa ambamo mtoto anaishi; nchi ambayo mtoto anatoka na kwa ustaarabu tofauti na wa kwake;
(d) kumwandaa mtoto kwa maisha ya uwajibikaji katika jamii huru, kwa moyo wa uelewano, amani, uvumilivu, usawa wa kijinsi, na urafiki miongoni mwa watu wote, makabila, makundi ya kitaifa na kidini na watu wa jamii za asili;
(e) kuendelea kuheshimu mazingira ya asili.
2. Hakuna sehemu yoyote ya kifungu hiki au kifungu 28 kitakachotumiwa kuingilia uhuru wa watu na mashirika kuanzisha na kuelekeza taasisi za elimu, kwa kuzingatia misingi iliyowekwa kwenye aya 1 ya kifungu hiki na kwa masharti kwamba elimu inayotolewa katika taasisi hizo italingana na viwango vya chini vilivyobainishwa na Serikali.
Kifungu 30
Katika Nchi ambamo kuna kabila, dini au lugha yenye watu wachache, mtoto anayetoka katika kundi lolote kati ya hayo au ambaye anatoka katika jamii ya asili hatanyimwa haki yake kwenye jamii pamoja na watu wa kundi lake, kuzingatia utamaduni wake, kukiri na kushiriki katika dini yake au kutumia lugha yake.
Kifungu 31
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto kupumzika na kustarehe, kushiriki katika michezo na shughuli za burudani zinazolingana na umri wake na kushiriki kwa uhuru katika maisha ya utamaduni na sanaa.
2. Nchi Wanachama zitaheshimu na kuendeleza haki ya mtoto kushiriki kikamilifu katika maisha ya kitamaduni na kisanaa na zitahimiza kutolewa kwa fursa sawa na zinazofaa kwa shughuli za kitamaduni, sanaa, burudani na starehe.
12
Kifungu 32
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya mtoto ya kulindwa dhidi ya kunyonywa kiuchumi na kufanya kazi yoyote inayoonekana kuwa ya hatari au kuingilia elimu yake, ama kuwa na madhara kwa afya yake na maendeleo yake ya kimwili, kiakili, kiroho, kimaadili na kijamii.
2. Nchi Wanachama zitachukua hatua za kisheria, kiutawala kijamii na kielimu kuhakikisha utekelezaji wa kifungu hiki. Ili kufikia lengo hili, na kwa kuzingatia sheria nyingine za kimataifa, Nchi Wanachama zitazingatia yafutayo:
(a) kuweka umri wa chini wa kuanza ajira;
(b) kuweka taratibu zinazofaa kuhusu saa na mazingira ya kazi;
(c) kuweka viwango vinavyofaa vya adhabu au vizuizi vingine kuhakikisha kuwa kifungu hiki kinatekelezwa ipasavyo.
Kifungu 33
Nchi Wanachama zitachukua hatua zinazofaa, ikiwa ni pamoja na za kisheria, kiutawala, kijamii na kielimu, ili kumlinda mtoto dhidi ya matumizi haramu ya madawa ya kulevya kama inavyoelezwa katika mikataba husika ya kimataifa, na kuzuia matumizi ya watoto katika biashara haramu ya kuzalisha na kusafirisha madawa hayo.
Kifungu 34
Nchi Wanachama zinakubali kuwalinda watoto kutokana na aina zote za unyonyaji na unyanyasaji wa kingono. Ili kufikia lengo hili, Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa katika ngazi ya taifa, kati ya nchi mbili na mataifa mbalimbali ili kuzuia.
(a) kumshawishi au kumlazimisha mtoto kufanya ngono isivyo halali;
(b) unyonyaji wa kuwatumia watoto katika ukahaba au vitendo vingine vya ngono kinyume desturi;
(c) unyonyaji wa kutumia watoto katika vitendo na vifaa vya ponografia.
Kifungu 35
Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinaofaa katika ngazi ya taifa, kati ya nchi mbili na mataifa mbalimbali kuzuia utekaji, uuzaji, au usafirishaji wa watoto kwa sababu au kwa njia yoyote ile.
Kifungu 36
Nchi Wanachama zitawalinda watoto kutokana na aina zote za unyonyaji zinazoenda kinyume na masuala yoyote ya ustawi wa watoto.
Kifungu 37
Nchi Wanachama zitahakikisha kwamba:
(a) hakuna mtoto atakayeteswa au kufanyiwa ukatili, unyama ama vitendo vya kudhalilishwa au kupewa adhabu. Wala hatapewa adhabu ya kuchapwa viboko au kifungo cha maisha bila kuwa na uwezekano wa kuachiwa huru kwa makosa aliyoyafanya mtu aliye chini ya miaka 18;
13
(b) hakuna mtoto atakayenyimwa uhuru wake kinyume cha sheria au bila kufuata taratibu. Mtoto atakamatwa, kuwekwa kizuizini au kufungwa kwa kutazingatia sheria na itafanywa hivyo kama hatua ya mwisho na ya muda mfupi iwezekanavyo;
(c) kila mtoto atakayenyimwa uhuru atafanyiwa ubinadamu na kupewa heshima inayomstahili binadamu, na kwa namna ambayo itazingatia mahitaji ya umri wake. Hasa, kila mtoto aliyenyimwa uhuru atatengwa na watu wazima isipokuwa pale inapofikiriwa kwamba ni muhimu kutofanya hivyo kwa maslahi ya mtoto na atakuwa na haki ya kuendeleza mawasiliano na familia yake kwa barua na kutembelewa, isipokuwa katika mazingira maalumu;
(d) kila mtoto aliyenyimwa uhuru wake atakuwa na haki ya kuomba msaada wa kisheria au msaada mwingine unaofaa, pamoja na haki ya kuhoji uhalali wa kunyimwa uhuru huo mahakamani au kwenye mamlaka nyingine mwafaka, iliyo huru na isiyopendelea upande wo wote, na kuomba uamuzi ufanywe dhidi ya kitendo hicho.
Kifungu 38
1. Nchi Wanachama zitaheshimu na kuhakikisha ufuataji wa kanuni za sheria ya kimataifa zinazohusu ubinadamu zinazomlenga mtoto.
2. Nchi Wanachama zitachukuwa hatua zote zinazowezekana kuhakikisha kwamba watu ambao hawajafikia umri wa miaka 15 hawashiriki katika uhasama moja kwa moja.
3. Nchi Wanachama hazitamwingiza mtu yeyote aliye chini ya umri wa miaka 15 katika majeshi yao. Katika kuwaingiza watu waliofika umri wa miaka 15 lakini hawajafika miaka 18, kipaumbele kitatolewa kwa wale wenye umri mkubwa zaidi.
4. Kwa mujibu wa wajibu wao chini ya sheria za kimataifa za ubinadamu katika kulinda raia kwenye migogoro ya kivita, Nchi Wanachama zitachukua hatua zinazowezekana kuhakikisha ulinzi na matunzo ya watoto walioathirika na vita hivyo.
Kifungu 39
Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazofaa kuendeleza hali nzuri ya kimwili na kisaikolojia na kuwaunganisha tena na jamii watoto walioathirika na kutekelezwa, kunyonywa, au kunyanyaswa; mateso ama aina nyingine ya ukatili, vitendo vya kinyama, kudhalilishwa au adhabu; ama vita. Nafuu hiyo ama kuunganishwa huko kutakuwa katika mazingira ambayo yataendeleza afya, kujiheshimu na kuheshimiwa kwa mtoto huyo.
Kifungu 40
1. Nchi Wanachama zinatambua haki ya kila mtoto anayetuhumiwa, kushitakiwa, au anayetambulika kufanya kosa la jinai, kutendewa kwa jinsi ambayo itaendeleza heshima na hadhi ya mtoto, kuimarisha uwezo wake wa kuheshimu haki za binadamu na uhuru wa msingi wa watu wengine na kuzingatia umri wa mtoto na haja ya kumuunganisha tena katika jamii na kumwezesha kutimiza majukumu yake ya ujenzi wa jamii hiyo.
2. Ili kufikia lengo hili na kwa kuzingatia sheria za kimataifa, Nchi Wanachama zitahakikisha kwamba:
14
(a) hakuna mtoto atakayetumiwa, kushtakiwa au kutambuliwa kuwa amefanya kosa la jinai kwa sababu ya kutenda au kutotenda jambo ambalo lilikuwa halijazuiliwa na sheria za nchi au za kimataifa wakati lilipotendwa;
(b) Kila mtoto anayetuhumiwa au kushtakiwa kufanya kosa la jinai atakuwa na hakika ya:
(i) kutambuliwa kuwa hana hatia hadi pale sheria itakapothibitisha vinginevyo;
(ii) kujulishwa kikamilifu na moja kwa moja kuhusu mashtaka dhidi yake, na kama inafaa, kupitia kwa wazazi wake au walezi wake kisheria, na kupewa msaada wa kisheria au misaada mingine katika kuandaa na kuwakilisha utetezi wake;
(iii) suala lake kuamuliwa bila kuchelewa na mamlaka mwafaka iliyo huru na isiyopendelea upande wowote au mamlaka ya kisheria katika itakayoendeshwa kwa uadilifu kulingana na sheria, kukiwa na msaada wa kisheria au aina nyingine ya msaada, ila tu kama inafikiriwa kwamba hautakuwa kwa maslahi ya mtoto, hasa kwa kuzingatia umri wake au hali yake, ya wazazi wake au walezi wake wa kisheria;
(iv) kutolazimishwa kutoa ushahidi au kukiri kufanya kosa; kumsaili shahidi anayempinga na kupata ushiriki na usaili wa shahidi kwa niaba yake katika mazingira ya usawa;
(v) endapo atafikiriwa kufanya uhalifu, uamuzi na hatua zozote zitakazochukuliwa dhidi yake zitaangaliwa na mamlaka mwafaka ya ngazi ya juu, iliyo huru na isiyopendelea upande wowote ama chombo cha mahakama kulingana na sheria;
(vi) kupewa msaada wa bure wa mkalimani kama mtoto haelewi ama haongei lugha inayotumika;
(vii) kuheshimiwa usiri wake katika hatua zote za uendeshaji wa kesi.
3. Nchi Wanachama zitasisitiza uundaji wa sheria, taratibu, mamlaka na taasisi zinazowahusu moja kwa moja watoto wanaotuhumiwa, kushtakiwa ama kutambuliwa kuwa wamefanya uhalifu na hasa:
(a) uwekaji wa umri wa chini ambao watoto watachukuliwa kuwa hawana uwezo wa kufanya kosa la jinai.
(b) pale inapofaa na inapotakiwa kuchukuliwa hatua za kuwashughulikia watoto, ifanywe hivyo bila kutumia mahakama, ili mradi haki za binadamu na kinga za kisheria ziheshimiwe kikamilifu.
4. Mipango kadhaa, kama vile matunzo, miongozo na kanuni za usimamizi, ushauri nasaha, uchunguzi, kuwekwa chini ya walezi, programu za elimu na mafunzo ya ufundi na njia mbadala za malezi zaidi ya vituo zitakuwepo kuhakikisha kwamba watoto wanashughulikiwa kwa namna inayofaa kwa ajili ya ustawi wao na kulingana na hali zao na kosa lililofanywa.
15
Kifungu 41
Hakuna chochote katika Mkataba huu kitakachobadili sheria yoyote ambayo inafaa zaidi katika kutekeleza haki za mtoto na ambayo ipo katika
(a) sheria za Nchi Mwanachama; au
(b) sheria ya kimataifa inayotekelezwa Nchini humo.
SEHEMU II
Kifungu 42
Nchi Wanachama zinakubali kufanya kanuni na vifungu vya Mkataba huu vijulikane kote, kwa njia zinazofaa na za makusudi, kwa watu wakubwa na watoto vilevile.
Kifungu 43
1. Kwa ajili ya kuangalia mafanikio yaliyofanywa na Nchi Wanachama katika kutekeleza majukumu yaliyokubaliwa katika Mkataba huu, itaundwa Kamati ya Haki za Mtoto, ambayo itafanya kazi zitakazobainisha hapo baadaye chini ya kifungu hiki.
2. Kamati itaundwa na watu kumi ambao ni wataalam wenye kiwango cha hali ya juu cha maadili na wanaotambulika kwamba wamebobea katika uwanja inaozingatiwa na Mkataba huu. Wanachama wa Kamati watachaguliwa na Nchi Wanachama kutoka miongoni mwa raia wao na watafanya kazi kwa kadri ya uwezo wao, kwa kuzingatia mgawanyo wa kijiografia na pia mfumo mzima wa sheria
3. Wanachama wa Kamati watachaguliwa kwa kura za siri kutoka katika orodha iliyopendekezwa na Nchi Wanachama. Kila Nchi Mwanachama inaweza kumchagua mtu mmoja miongoni mwa raia wake.
4. Uchaguzi wa kwanza utafanyika katika kipindi kisichozidi miezi sita baada ya Mkataba huu kuanza kutumika, na kila miaka miwili baada ya hapo. Angalau miezi minne kabla ya uchaguzi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atapeleka barua kwa Nchi Wanachama, akiwakaribisha kuwasilisha mapendekezo ya majina katika kipindi cha miezi miwili. Baada ya hapo, Katibu Mkuu ataandaa orodha ya majina ya watu wote waliopendekezwa kwa alfabeti, akionyesha Nchi Wanachama ambazo zimewapendekeza na atawasilisha orodha hiyo kwa Nchi Wanachama za Mkataba huu.
5. Uchaguzi utafanywa katika mikutano ya Nchi Wanachama itakayoitishwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa. Kwenye mikutano hiyo ambayo theluthi mbili ya wajumbe itatosha kuwa akidi, watu watakaochaguliwa katika kamati ni wale watakaopata idadi kubwa ya kura kwa zaidi ya nusu ya Nchi Wanachama zitakazokuwepo na kupiga kura.
6. Wajumbe wa kamati watachaguliwa kwa kipindi cha miaka minne. Wataweza kuchaguliwa kwa kipindi kingine endapo watapendekezwa. Kipindi cha wajumbe watano waliochaguliwa katika uchaguzi wa kwanza kitaisha baada ya miaka miwili, mara baada ya uchaguzi wa kwanza, majina ya wajumbe hao watano yatachaguliwa kwa bahati nasibu na Mwenyekiti wa mkutano.
16
7. Endapo mjumbe wa kamati atafariki au kujiuzulu ama ataeleza kwa sababu yoyote ile kwamba hataweza kuendelea kufanya kazi za kamati, Nchi Wanachama iliyomchagua mjumbe huyo, itamteua mtaalam mwingine kutokana na raia wake kutumikia kwa kipindi kilichobakia iwapo atakubaliwa na kuthibitishwa na Kamati.
8. Kamati itaunda taratibu zake za utendaji.
9. Kamati itachagua maofisa wake kwa kipindi cha miaka miwili.
10. Mikutano ya Kamati kwa kawaida itafanyika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa au katika sehemu nyingine yoyote inayofaa kama itakavyoamuliwa na Kamati. Kwa kawaida Kamati itakutana mara moja kwa mwaka. Muda wa mikutano ya kamati utaamuliwa na kupitiwa, inapolazimika, na mkutano wa Nchi Wanachama wa Mkataba huu, kama itakavyothibitishwa na Baraza Kuu.
11. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atatoa watumishi wanaohitajika na vifaa kwa ajili ya kufanikisha utendaji wa kazi za Kamati chini ya Mkataba huu.
12. Kwa uthibitisho wa Baraza Kuu, wajumbe wa Kamati itakayoundwa chini ya Mkataba huu watalipwa mishahara kutokana na raslimali za Umoja wa Mataifa kwa viwango na masharti yatakayowekwa na Baraza hilo.
Kifungu 44
1. Nchi Wanachama zitawasilisha kwa Kamati, kupitia kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, taarifa kuhusu hatua walizochukua kuhakikisha utekelezaji wa haki zinazobainishwa humu na maendeleo yaliyofanywa katika kutimiza haki hizo:
(a) katika kipindi cha miaka miwili tangu kuanza utekelezaji wa Mkataba huu kwa Nchi Mwanachama inayohusika;
(b) na kila baada ya miaka mitano baada ya hapo.
2. Taarifa itakayoandikwa chini ya kifungu hiki itaonyesha sababu na matatizo, kama yapo, yanayoathiri kiwango cha utekelezaji wa majukumu yaliyobainishwa na Mkataba huu. Taarifa hiyo itakulwa na taarifa za kutosha kuiwezesha Kamati kuelewa kikamilifu utekelezaji wa Mkataba huu katika nchi husika.
3. Nchi Mwanachama ambayo imewasilisha taarifa kamili ya kwanza kwa Kamati haitahitaji kurudia taarifa za msingi katika taarifa zinazofuata zinazowasilishwa kwa mujibu wa aya 1 (b) ya kifungu hiki.
4. Kamati inaweza kuomba Nchi Wanachama kutoa maelezo zaidi kuhusu utekelezaji wa Mkataba huu.
5. Kamati itawasilisha taarifa ya shughuli zake kwa Baraza Kuu, kupitia Baraza la Uchumi na Jamii, kila baada ya miaka miwili.
6. Nchi Wanachama zitasambaza taarifa zao kwa umma kote nchini mwao.
Kifungu 45
Ili kuwezesha utekelezaji wenye ufanisi wa na kuhimiza ushirikiano wa kimataifa katika nyanja zinazoshughulikiwa na Mkataba huu:
(a) Mashirika maalum, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) na vyombo vingine vya Umoja wa Mataifa vitakuwa na haki ya kuwakilishwa wakati wa kufikiria utekelezaji wa vipengele vya Mkataba huu vinavyohusiana na mawanda ya mamlaka yao. Kamati inaweza kualika mashirika maalum, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia
17
Watoto na vyombo vingine, kama itakavyoona inafaa, ili kutoa ushauri wa kitaalamu katika utekelezaji wa Mkataba huu kwenye maeneo yaliyo chini ya mawanda yao ya mamlaka. Kamati inaweza pia kualika mashirika maalumu, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto na vyombo vingine vya Umoja wa Mataifa, kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mkataba huu katika maeneo yaliyo chini ya mawanda ya shughuli zao;
(b) Kamati itapeleka kwa mashirika maalumu, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto na vyombo vingine mwafaka, taarifa yoyote kutoka kwa Nchi Wanachama yenye maombi au inayoonesha haja ya ushauri au msaada wa kiufundi, pamoja na maoni na mapendekezo ya Kamati, kama yapo, kuhusu maombi ama haja hiyo;
(c) Kamati inaweza kupendekeza kwa Baraza kuu kumwomba Katibu Mkuu kufanya utafiti kuhusu masuala mahsusi yanayohusiana na haki za mtoto kwa niaba yake;
(d) Kamati inaweza kutoa maoni na mapendekezo ya jumla kutokana na taarifa zilizopokelewa kwa mujibu wa vifungu 44 na 45 vya Mkataba huu. Ushauri na mapendekezo hayo ya jumla yatapelekwa kwa Nchi Wanachama yoyote inayohusika na kuwasilishwa kwa Baraza Kuu, pamoja na maoni ya Nchi Wanachama, kama yapo.
SEHEMU III
Kifungu 46
Nchi zote zitakuwa huru kutia saini Mkataba huu.
Kifungu 47
Mkataba huu unaweza kuridhiwa. Hati rasmi za kuridhiwa huko zitakabidhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
Kifungu 48
Mkataba huu utakuwa wazi kwa Nchi yoyote kujiunga. Hati rasmi za kujiunga zitakabidhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa
Kifungu 49
1. Mkataba huu utaanza kutekelezwa siku ya thelathini baada ya tarehe ya kukabidhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa hati ya ishirini ya kuridhia au kujiunga.
2. Kwa kila Nchi inayoridhia au kujiunga na Mkataba huu baada ya kukabidhi hati ya ishirini ya kuridhia au kujiunga, itaanza kuutekeleza siku ya thelathini baada ya kukabidhi hati hizo.
18
Kifungu 50
1. Nchi Mwanachama yoyote inaweza kupendekeza marekebisho na kuyapeleka kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Katibu Mkuu atazifahamisha Nchi Wanachama juu ya mapendekezo hayo na kuzitaka kuonyesha kama wanataka kuwepo mkutano wa Nchi Wanachama wa kuyafikiria na kuyapigia kura mapendekezo hayo. Iwapo, katika kipindi cha miezi minne tangu siku ya mawasiliano hayo, angalau theluthi moja ya Nchi Wanachama watataka kuwepo mkutano huo, Katibu Mkuu ataitisha mkutano huo chini ya Umoja wa Mataifa. Marekebisho yoyote yatakayokubaliwa na idadi kubwa ya wajumbe waliopo na wanaopiga kura yatawasilishwa Baraza Kuu kwa uthibitisho.
2. Marekebisho yaliyokubaliwa kulingana na aya 1 ya kifungu hiki yataanza kutumika yatakapothibitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa na kukubaliwa na theluthi mbili ya Nchi Wanachama
3. Marekebisho yanapoanza kutumika, yatahusu Nchi Wanachama zilizoyakubali, Nchi nyingine Wanachama bado zitahusika na vifungu vya Mkataba huu na marekebisho yoyote ya awali ambayo waliyakubali.
Kifungu 51
1. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atapokea na kutuma kwa Nchi Wanachama vifungu vyote vilivyokataliwa na Nchi wakati wa kuridhia au kujiunga.
2. Ukataaji usioendana na malengo na nia ya Mkataba huu hautakubaliwa.
3. Ukataaji huo unaweza kutanguliwa wakati wowote kwa taarifa itakayopelekwa kwa Katiba Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa nia hiyo, naye ataziarifu Nchi zote. Taarifa hiyo itaanza kutekelezwa tarehe ambayo itapokelewa na Katibu Mkuu.
Kifungu 52
Nchi Wanachama inaweza kuukataa Mkataba huu kwa taarifa ya maandishi kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Kukataa huko kutaanza kutekelezwa mwaka mmoja baada ya taarifa kupokelewa na Katibu Mkuu.
Kifungu 53
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anatambuliwa kuwa ndiye kabidhi wa Mkataba huu.
Kifungu 54
Nakala ya asili ya Mkataba huu, ambayo ni pamoja na nakala za Kiarabu, Kichina, Kiingereza, Kifaransa, Kirusi na Kihispania, zenye hadhi sawa ya uasili, itahifadhiwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Kwa ushahidi, maofisa walioandikwa hapa chini wametia saini Mkataba huu kwa mamlaka waliyopewa na Serikali zao.
19
ITIFAKI YA ZIADA YA MKATABA WA
HAKI ZA MTOTO JUU YA KUHUSISHA
WATOTO KWENYE MIGOGORO YA KIVITA
Imepitishwa na Baraza Kuu kwenye azimio lake A/RES/54/ 263 la Mei 25, 2000.
Limeanza Kutekelezwa Februari 12, 2002
Itifaki ya Ziada ya Mkataba wa Haki za Mtoto juu ya kuhusisha Watoto
kwenye migogoro ya kivita
Nchi Wanachama wa Itifaki hii,
Wakiwa wametiwa moyo na jinsi Mkataba wa Haki za Mtoto ulivyoungwa mkono
na mataifa mengi, ikidhihirisha dhamiri iliyoenea ya jitihada za kuendeleza na
kulinda haki za mtoto,
Katika kusisitiza kwamba haki za watoto zinahitaji ulinzi maalumu na kuendelea
kuboresha hali ya watoto bila kuwatenganisha, pamoja na kuwa na makuzi na
elimu katika hali ya amani na usalama,
Kutokana na kusumbuliwa na madhara yaliyosambaa ya migogoro ya kivita kwa
watoto na matokeo ya muda mrefu katika kuwa na amani ya kudumu, usalama
na maendeleo,
Katika kulaani vitendo vya kuwalenga watoto katika migogoro ya kivita na
kushambulia suhula zinazolindwa na sheria za kimataifa, ikiwa ni pamoja na
maeneo ambayo yanatumiwa sana na watoto, kama vile shule na hospitali,
Wakizingatia kupitishwa kwa Sheria ya Roma ya Mahakama ya Jinai ya
Kimataifa, hasa kuchukuliwa kuwa ni kosa la jinai kuandikisha au kuorodhesha
watoto chini ya miaka 15 ama kuwatumia kushiriki kwenye uhasama wa
migogoro ya kivita ya kimataifa na isiyo ya kimataifa,
Kwa hiyo, wakichukulia kwamba kuna haja ya kuongeza ulinzi wa watoto ili
wasihusishwe katika migogoro ya kivita kwa ajili ya kuimarisha utekelezaji wa
haki zinazotambuliwa katika Mkataba wa Haki za Mtoto,
Wakitambua kuwa kifungu 1 cha Mkataba wa Haki za Mtoto kinabainisha,
madhumuni ya Mkataba huo, kuwa mtoto maana yake ni kila binadamu mwenye
umri wa chini ya miaka 18 labda tu, chini ya sheria ya mtoto inayotumiwa, umri
wa ukubwa ni mapema zaidi,
Wakishawishika kuwa itifaki ya ziada ya Mkataba huu inayoongeza umri wa mtu
kuweza kushiriki kwenye majeshi na uhasama itasaidia sana katika utekelezaji
wa msingi kwamba maslahi ya mtoto ni jambo muhimu katika vitendo vyote
vinavyomhusu mtoto,
Wakifahamu kuwa Mkutano wa Ishirini na Sita wa Kimataifa wa Msalaba
Mwekundu na Mwezi Mwekundu uliofanyika Mwezi Desemba 1995 ulipendekeza,
pamoja na mambo mengine, nchi zilizo kwenye migogoro zichukue hatua kwa
kadri inavyowezekana kuhakikisha kuwa watoto chini ya umri wa miaka 18
hawashiriki katika uhasama;
Katika kufurahia kukubaliwa kwa kauli moja, Juni 1999, Mkataba Na. 182 wa
Shirika la Kazi Duniani kuhusu Kupiga Marufuku na Kuchukuliwa kwa Hatua za
Haraka za Kutokomeza Aina Mbaya Kabisa za Ajira za Watoto, ambao unakataza,
pamoja na mambo mengine, kuwaandikisha kwa nguvu au kwa lazima watoto ili
watumike katika migogoro ya kivita;
Wakilaani kwa nguvu zote uandikishaji, ufundishaji na kutumia watoto ndani au
nje ya mipaka ya nchi yao katika uhasama wa makundi yenye silaha, mbali na
majeshi ya Nchi, na kwa kutambua wajibu wa wale wanaowaandikisha,
kuwafunza na kuwatumia watoto kwa namna hii,
Wakikumbuka wajibu wa kila nchi inayohusika na migogoro ya kivita kutii
vipengele vya sheria za ubinadamu za kimataifa,
2
Wakisisitiza kuwa Itifaki hii haipotezi malengo na misingi ya Mkataba wa Umoja
wa Maitafa, ikiwa pamoja na kifungu 51, na kaida zinazohusika na sheria ya
ubinadamu,
Wakijua kwamba masharti ya amani na usalama yanayoheshimu kikamilifu
malengo na misingi iliyomo kwenye Mkataba huo na uzingatiaji wa sheria za haki
za binadamu zinazohusika kuwa ni za lazima kwa ulinzi kamili wa watoto, hasa
wakati wa migogoro ya kivita na uvamizi kutoka nje,
Wakitambua mahitaji maalumu ya watoto ambao wako hatarini kuandikishwa au
kutumiwa katika uhasama kinyume na Itifaki hii kwa sababu ya hadhi yao ya
kiuchumi, kijamii au kijinsia,
Wakijua umuhimu wa kufikiria sababu za msingi za kiuchumi, kijamii na kisiasa
za kuwahusisha watoto katika migogoro ya kivita,
Kwa kukubali haja ya kuimarisha ushirikiano wa kimataifa katika utekelezaji wa
Itifaki hii, pamoja na kuwarudisha watoto katika hali yao ya kawaida ya kimwili
na kisaikolojia kutokana na kuathiriwa na migogoro ya kivita,
Katika kuhimiza ushiriki wa jumuiya na, hasa, watoto na watoto walioathiriwa
na vita katika kusambaza programu za habari na elimu kuhusiana na utekelezaji
wa Itifaki hii,
Wamekubaliana kama ifuatavyo:
Kifungu 1
Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazowezekana kuhakikisha kuwa
askari wa jeshi lao ambao hawajatimiza umri wa miaka 18 hawashiriki moja kwa
moja katika uhasama na uadui wa kivita.
Kifungu 2
Nchi Wanachama zitahakikisha kuwa watu ambao hawajatimiza umri wa miaka
18 hawalazimishwi kuandikishwa katika majeshi yao.
Kifungu 3
3
1. Nchi Wanachama zitapandisha umri wa chini wa mtu kujiandikisha kwa hiari
katika majeshi yake ya taifa, kwa mujibu wa kifungu 38, aya 3 ya Mkataba wa
Haki za Mtoto, kwa kuzingatia misingi ya kifungu hicho na kutambua kuwa chini
ya Mkataba huo watu walio chini ya umri wa miaka 18 wana haki ya kupewa
ulinzi maalumu.
2. Kila Nchi Mwanachama itaweka azimio linaloifunga baada ya kuridhia au
kukubali Itifaki hii ambayo inaweka umri wa chini wa kuruhusu uandikishaji wa
hiari katika majeshi ya taifa lake na maelezo ya hatua za ulinzi ilizozichukua
kuhakikisha kuwa uandikishaji haufanywi kwa shuruti ama kwa kitisho.
3. Nchi Wanachama zinazoruhusu uandikishaji wa hiari wa kuingia kwenye
majeshi yake ya taifa watu walio chini ya umri wa miaka 18 zitachukua hatua za
kuhakikisha kwamba angalau:
(a) uandikishaji huo kweli ni wa hiari;
(b) kuingia huko jeshini kunafanywa kwa kuwa na taarifa kamili kwa wazazi
au walezi wa kisheria wa mtu huyo;
(c) watu hao wanafahamu kikamilifu kazi zinaozohusiana na huduma hizo
za kijeshi;
(d) watu hao wanatoa ushahidi wa umri wao kabla ya kukubaliwa kujiunga
na jeshi.
4. Kila Nchi Mwanachama inaweza kuimarisha azimio lake wakati wowote kwa
kumwarifu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ambaye ataziarifu Nchi zote
Wanachama. Taarifa hiyo itaanza kutumika tarehe ambayo Mkuu ataipokea.
5. Masharti ya kupandisha umri kwa mujibu wa aya 1 ya kifungu hiki haihusu
shule zinazoendeshwa au zilizo chini ya mamlaka ya majeshi ya Nchi
Wanachama, kwa mujibu wa vifungu 28 na 29 vya Mkataba wa Haki za Mtoto.
Kifungu 4
1. Makundi ya kijeshi yaliyo tofauti na majeshi ya Nchi hayaruhusiwi, kwa hali
yoyote ile, kuandikisha au kuwatumia watu walio na umri chini ya miaka 18
kwenye uhasama.
4
2. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazowezekana kuzuia uandikishaji na
matumizi hayo ya watoto, ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua za kisheria
zinazobidi kupiga marufuku na kuvichukulia vitendo hivyo kuwa kosa la jinai.
3. Utekelezaji wa kifungu hiki hautaathiri hadhi ya kisheria ya upande wowote wa
kundi lililo vitani.
Kifungu 5
Hakuna chochote kwenye Itifaki hii kitakachofasiliwa kuzuia kipengele chochote
katika sheria za Nchi Mwanachama au sheria za kimataifa na sheria za kimataifa
zinazohusu ubinadamu ambazo zitamwezesha mtoto kupewa haki zake.
Kifungu 6
1. Kila Nchi Mwanachama itachukua hatua za kisheria, kiutawala na nyinginezo
zinazobidi kuhakikisha utekelezaji wa ufanisi na kusisitizia vipengele vya Itifaki
hii vilivyo chini ya mamlaka yake.
2. Nchi Wanachama zitajitahidi kuieneza misingi na vipengele vya Itifaki hii, kwa
kutumia njia mwafaka, ili vieleweke na watu wakubwa na watoto pia.
3. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazowezekana kuhakikisha watu walio
chini ya mamlaka zao walioandikishwa au kutumiwa katika uhasama kinyume
cha Itifaki hii wanaruhusiwa kuondoka au kuachishwa jeshi. Nchi Wanachama,
ikibidi, zitawapa watu hao misaada inayostahili ili waweze kurudia hali yao ya
kawaida ya kimwili na kisaikolojia na kuunganishwa tena na jamii.
Kifungu 7
1. Nchi Wanachama zitashirikiana katika utekelezaji wa Itifaki hii, ikiwa ni pamoja
na kuzuia kitendo chochote kinachopingana na madhumuni yake na
kuwarudisha tena watu walioathirika katika hali yao ya kawaida na
kuwaunganisha na jamii, ikijumuisha ushirikiano wa kiufundi na msaada wa
fedha. Msaada na ushirikiano huo utatolewa kwa kushauriana na Nchi
Wanachama zinazohusika na mashirika mwafaka ya kimataifa.
2. Nchi Wanachama zinazoweza kufanya hivyo zitatoa msaada huo kupitia
programu zilizopo zinazoshirikisha nchi nyingi, nchi mbili au programu nyingine, 5
ama kutumia mfuko wa hiari utakaoanzishwa kwa kuzingatia kanuni za Baraza
Kuu la Umoja wa Mataifa.
Kifungu 8
1. Kila Nchi Mwanachama, katika kipindi cha miaka miwili tangu kuanza utekelezaji
wa Itifaki hii Nchini humo, itawasilisha ripoti kwa Kamati ya Haki za Mtoto ikitoa
taarifa za kina kuhusu hatua ilizochukua kutekeleza vipengele vya Itifaki hii, ikiwa
ni pamoja na hatua zilizochukuliwa kutekeleza vipengele kuhusu ushiriki na
uandikishwaji jeshini.
2. Baada ya kuwasilisha ripoti hiyo ya kina, kila Nchi Mwanachama itaonyesha
kwenye ripoti zinazowasilishwa katika Kamati ya Haki za Mtoto, kwa mujibu wa
kifungu 44 cha Mkataba wa Haki za Mtoto, taarifa yoyote ya ziada inayohusiana na
utekelezaji wa Itifaki hii. Nchi nyingine Wanachama wa Itifaki hii zitawasilisha
ripoti kila baada ya miaka mitano.
3. Kamati ya Haki za Mtoto inaweza kuiomba Nchi Mwanachama kutoa taarifa zaidi
zinazohusu utekelezaji wa Itifaki hii.
Kifungu 9
1. Itifaki hii inaweza kutiwa saini na Nchi yoyote ambayo imejiunga na Mkataba wa
Haki za Mtoto au imetia saini Mkataba huo.
2. Itifaki hii inaweza kuridhiwa na iko wazi kukubaliwa na Nchi yoyote. Hati rasmi za
kuiridhia au kuikubali zitahifadhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
3. Katibu Mkuu, kwa mamlaka aliyo nayo kama mhifadhi wa Mkataba na Itifaki,
ataziarifu Nchi zote Wanachama wa Mkataba na Nchi zote zilizotia saini Mkataba
huo, kuhusu kila hati rasmi ya azimio atakayoipokea kwa mujibu wa kifungu 3.
Kifungu 10
1. Itifaki hii itaanza kutekelezwa miezi mitatu baada ya kukabidhi hati rasmi ya
kumi ya kuiridhia au kuikubali.
6
2. Kwa kila Nchi inayoridhia au kuikubali Itifaki hii, baada ya kuanza kutekelezwa,
itaanza kuitekeleza mwezi mmoja baada ya tarehe ya Nchi kukabidhi hati rasmi
za kuiridhia au kuikubali.
Kifungu 11
1. Nchi Mwanachama yoyote inaweza kujitoa katika Itifaki hii wakati wowote kwa
kutoa taarifa ya maandishi kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, ambaye
baada ya hapo ataziarifu nchi nyingine Wanachama wa Mkataba wa Haki za
Mtoto na Nchi nyingine zote zilizotia saini Mkataba huo. Kujitoa kutaanza
kutekelezwa mwaka mmoja baada ya Katibu Mkuu kupokea taarifa hiyo. Iwapo,
ndani ya mwaka huo Nchi Mwanachama inayojitoa itakuwa na mgogoro wa kivita,
kujitoa huko hakutatekelezwa hadi mgogoro huo utakapomalizika.
2. Kujitoa huko hakutaiondolea Nchi Mwanachama majukumu yake kwa mujibu wa
Itifaki hii kuhusiana na tendo lolote lililotokea kabla ya tarehe ya utekelezaji wa
kujitoa huko. Wala kujitoa huko hakutaathiri kwa njia yoyote ile suala lolote
lililokuwa likishughulikiwa na Kamati ya Haki za Mtoto kabla ya tarehe ya
kuanza utekelezaji wa kujitoa huko.
Kifungu 12
1. Nchi yoyote Mwanachama inaweza kupendekeza marekebisho na kuyapeleka kwa
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Katibu Mkuu atawasiliana na Nchi zote
Wanachama kuhusu marekebisho yaliyopendekezwa na kuziomba zionyeshe iwapo
zinaafiki kuitishwa kwa mkutano wa Nchi Wanachama kwa lengo la kufikiria na
kupigia kura mapendekezo hayo. Iwapo katika kipindi cha miezi minne kutoka
tarehe ya mawasiliano hayo theluthi moja ya Nchi Wanachama zitapendelea
mkutano huo, Katibu Mkuu ataitisha mkutano chini ya Umoja wa Mataifa.
Marekebisho yoyote yatakayopitishwa na Nchi nyingi Wanachama zilizohudhuria
na kupiga kura kwenye mkutano huo, yatawasilishwa katika Baraza Kuu la Umoja
wa Mataifa ili yaidhinishwe.
2. Marekebisho yaliyoidhinishwa kwa mujibu wa aya 1 ya kifungu hiki yataanza
kutumika baada ya kuidhinishwa na Baraza Kuu la Umoja wa mataifa na
kukubaliwa na theluthi mbili za wingi wa kura za Nchi Wanachama.
7
3. Marekebisho hayo yatakapoanza kutekelezwa, yatahusu Nchi Wanachama
zilizoyakubali, Nchi Wanachama nyingine zitakuwa zitafuata vipengele vya Itifaki hii
na marekebisho yoyote ya awali waliyoyakubali.
Kifungu 13
1. Itifaki hii ambayo matini zake za Kiarabu, Kichina, Kiingereza, Kifaransa, Kirusi na
Kihispania zina uhalisi sawa, itahifadhiwa kwenye nyaraka za Umoja wa Mataifa.
2. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atapeleka nakala zilizothibitishwa za Itifaki hii
kwa Nchi zote Wanachama wa Mkataba wa Haki za Mtoto na Nchi zote zilizotia saini
Mkataba huo.
8
ITIFAKI YA ZIADA YA MKATABA WA HAKI ZA MTOTO
KUHUSU UUZAJI WA WATOTO NA UKAHABA NA
PONOGRAFIA INAYOSHIRIKISHA WATOTO
Imepitishwa na Baraza Kuu kwenye azimio lake A/RES/54/ 263 la Mei 25, 2000.
Limeanza Kutekelezwa Januari 18, 2002
Itifaki ya Ziada ya Mkataba wa Haki za Mtoto kuhusu uuzaji wa
watoto na ukahaba na ponografia inayoshirikisha watoto
Nchi Wanachama wa Itifaki hii,
Kwa kuzingatia kwamba, ili kuendelea kufanikisha malengo ya Mkataba wa
Haki za Mtoto na utekelezaji wa vipengele vyake hususan vifungu 1, 11, 21,
32, 33, 34, 35 na 36, itafaa kuzidisha hatua ambazo Nchi Wanachama
zinaweza kuchukua ili kuhakikisha ulinzi wa mtoto dhidi ya uuzaji wa
watoto na ukahaba na ponografia inayoshirikisha watoto,
Kwa kuzingatia pia kuwa Mkataba wa Haki za Mtoto unatambua haki ya
mtoto kulindwa dhidi ya unyonyaji wa kiuchumi na kufanya kazi yo yote
inayoweza kuwa ya hatari au kuingilia elimu yake, au kuwa na madhara
kwa afya ya mtoto au kuathiri makuzi yake kimwili, kiakili, kiroho,
kimaadili na kijamii,
Wakiwa wamesumbuliwa sana na ukubwa na ongezeko la usafirishaji wa
kimataifa wa watoto kwa nia ya kuwauza na kuwashirikisha katika
ukahaba na ponografia ya watoto,
Wakiwa wamesikitishwa sana na kuenea na kuendelea kwa vitendo vya
utalii wa kingono ambapo watoto ndiyo huathirika sana kwani vitendo hivi
vinaongeza uuzaji wa watoto na ushirikishwaji wa watoto kwenye ukahaba
na ponografia.
Kwa kutambua kuwa idadi ya makundi ya watu walio katika hali hatarishi,
ikiwa pamoja na watoto wa kike, wapo katika hatari kubwa ya kunyonywa
kingono na kwamba kuna watoto wa kike wengi zaidi wanaonyonywa
kingono,
Wakiwa wamesumbuliwa na kuenea kwa upatikanaji wa ponografia za
watoto katika intaneti na teknolojia nyingine zinazochipuka, na kwa
kukumbuka Kongamano la Kimataifa kuhusu Kupambana na Ponografia za
Watoto kwenye Intaneti uliofanyika Vienna mwaka 1999, hususan hitimisho
lake linalotoa wito wa ulimwengu wote kufanya uzalishaji, usambazaji,
usafirishaji nje, uagizaji, umilikaji wa makusudi na utangazaji wa
ponografia ya watoto kuwa kosa la jinai na kusisitiza umuhimu wa
ushirikiano wa karibu baina ya Serikali na tasnia ya Intaneti,
Kwa kuamini kuwa utokomezaji wa uuzaji wa watoto na ukahaba na
ponografia inayoshirikisha watoto unaweza kusaidiwa na kuwa mkabala wa
jumla wa kushughulikia sababu zinazochangia, ikiwa pamoja na maendeleo
duni, umaskini, tofauti za kiuchumi, muundo wa uchumi na jamii usiojali
usawa, kushindwa kwa familia, ukosefu wa elimu, uhamaji toka vijijini
kwenda mjini, ubaguzi wa kijinsia, tabia za watu wakubwa wasiowajibika
kingono, desturi za kitamaduni zenye jadhara, migogoro ya kivita na
usafirishaji wa watoto,
Kwa kuamini pia kuwa juhudi za kuongeza ufahamu wa umma zinatakiwa
katika kupunguza mahitaji ya wateja wa uuzaji wa watoto na ukahaba na
ponografia inayoshirikisha watoto, na kwa kuamini zaidi katika umuhimu
wa kuimarisha ushirikiano ulimwenguni kwa watendaji wote na kuboresha
utekelezaji wa sheria katika ngazi ya taifa,
Kwa kuzingatia vipengele vya sheria za kimataifa vinavyohusu ulinzi wa
watoto, ikiwa pamoja na Mkataba wa Hague juu ya Ulinzi wa Watoto na
Ushirikiano wa Uasili wa Watoto Kati ya Nchi Mbili, Mkataba wa Hague
2
kuhusu Vipengele vya Kiraia vya Utoroshaji wa Watoto Kimataifa, Mkataba
wa Hague juu ya Mamlaka ya Kisheria, Sheria Zinazotumika, Utambuzi,
Utekelezaji na Ushirikiano kuhusiana na Wajibu wa Wazazi na Hatua za
Kuchukuliwa katika Kumlinda Watoto, na Mkataba Na. 182 wa Shirika la
Kazi Duniani kuhusu Kupiga Marufuku na Kuchukua Hatua za Haraka za
Kutokomeza Aina Mbaya zaidi ya Ajira za Watoto,
Wakiwa wametiwa moyo na jinsi Mkataba wa Haki za Mtoto ulivyoungwa
mkono na mataifa mengi, ikidhihirisha dhamiri iliyoenea ya jitihada za
kuendeleza na kulinda haki za mtoto,
Kwa kutambua umuhimu wa kushughulikia vipengele vya Programu ya
Utekelezaji wa Uzuiaji wa Uuzaji wa Watoto na Ukahaba na Ponografia
inayohusisha Watoto na Azimio na Ajenda ya Utekelezaji iliyopitishwa na
Mkutano wa Dunia dhidi ya Unyonyaji wa Biashara ya Ngono inayohusisha
Watoto uliofanyika Stockholm Agosti 27 hadi 31, 1996, na maamuzi na
mapendekezo mengine muhimu ya mashirika husika ya kimataifa;
Kwa kuzingatia umuhimu wa mila na maadili ya kitamaduni ya kila watu
katika ulinzi na makuzi mwafaka ya mtoto;
Wamekubaliana kama ifuatavyo:
Kifungu 1
Nchi Wanachama zitapiga marufuku uuzaji wa watoto, ukahaba na
ponografia inayohusisha watoto kama ilivyoelezwa na Itifaki hii.
Kifungu 2
Kwa lengo la Itifaki hii:
(a) uuzaji watoto maana yake ni kitendo chochote au mapatano yoyote
ambapo mtoto huhamishwa na mtu yeyote au kikundi cha watu
kwenda mahali pengine kwa malipo au kwa sababu yoyote ile;
(b) ukabaha unaohusisha watoto maana yake ni kumtumia mtoto
katika vitendo vya ngono kwa malipo au kwa sababu yoyote ile;
3
(c) ponografia inayohusisha watoto maana yake ni mtoto kushiriki kwa
namna yoyote ile katika vitendo dhahiri vya ngono halisi au vya
kuigiza ama kuonyesha sehemu za siri za mtoto kwa malengo ya
kingono.
Kifungu 3
1. Kila Nchi Mwanachama itahakikisha, kwa kuanzia, kuwa vitendo na
shughuli hizo zimeingizwa kikamilifu katika sheria zake za jinai au
sheria ya adhabu, iwe makosa hayo yamefanywa ndani au nje ya nchi
ama na mtu binafsi au kwa misingi ya magenge mahsusi:
(a) katika muktadha wa uuzaji watoto kama ulivyofasiliwa katika
kifungu 2:
(i) kumtoa, kumpeleka au kumkubali mtoto, kwa njia yoyote ile,
kwa lengo la:
a. kumnyonya mtoto kingono
b. kutoa viungo vya mtoto ili kupata fedha;
c. kumtumikisha mtoto;
(ii) kushawishi ridhaa isivyo halali, kama dalali, kwa ajili ya
uasili wa mtoto kwa kukiuka sheria za kimataifa
zinazotumika katika kuasili mtoto;
(b) kutoa, kupokea, kununua au kumpatia mtu mtoto kwa ajili ya
ukahaba unaohusisha watoto, kama ilivyofasiliwa katika kifungu 2;
(c) kutengeneza, kugawa, kusambaza, kuingiza, kusafirisha nje, kutoa,
kuuza au kuwa na mtoto kwa malengo ya ponografia inayohusisha
watoto kama ilivyofasiliwa katika kifungu 2.
2. Kwa mujibu wa vipengele vya sheria za ndani ya Nchi Mwanachama,
itakuwa ni kosa vilevile kujaribu kufanya vitendo vyovyote vilivyotajwa
na kula njama au kushiriki katika kitendo chochote kati ya vilivyotajwa
hapo juu.
3. Kila Nchi Mwanachama itaweka adhabu zinazostahili kwa makosa hayo
kulingana na uzito wa makosa yenyewe.
4. Kila Nchi Mwanachama itachukua hatua kwa mujibu wa sheria zake,
inapostahili, kuonyesha wajibu wa wataalamu wa sheria kwa makosa
4
yaliyoelezwa katika aya 1 ya kifungu hiki. Kwa mujibu wa kanuni za
kisheria za Nchi Mwanachama, wajibu huo wa wataalamu wa sheria
unaweza kuchukuliwa chini ya makosa ya jinai, madai au utawala.
5. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote za kisheria na kiutawala
zinazofaa kuhakikisha kuwa watu wote wanaohusika na uasili wa
mtoto wanafuata sheria za kimataifa zilizopo.
Kifungu 4
1. Kila Nchi Mwanachama itachukua hatua kwa kadri inavyobidi kuwa
na mamlaka kuhusu makosa yanayoelezwa katika kifungu 3, aya 1,
iwapo makosa hayo yamefanywa nchini au ndani ya meli au ndege
iliyosajiliwa na Nchi hiyo.
2. Kila Nchi Mwanachama itachukua hatua hizo kama inavyobidi kuwa
na mamlaka kuhusu makosa yaliyoelezwa kwenye kifungu 3, aya 1
katika kesi zifuatazo:
a. iwapo mtuhumiwa ni raia wa Nchi hiyo au ni mtu ambaye kwa
kawaida huishi katika nchi hiyo;
b. iwapo mwathiriwa ni raia wa Nchi hiyo.
3. Kila Nchi Mwanachama itachukua hatua kama hizo kadri inavyobidi
kuwa na mamlaka kuhusu makosa yaliyotajwa hapo juu wakati
mtuhumiwa yupo nchini na haimpeleki Nchi nyingine Mwanachama
kwa kuwa kosa limefanywa na mmoja wa raia wake.
4. Itifaki hii haiondoi mamlaka yoyote yanayoshughulikia makosa ya
jinai yaliyopo kwa mujibu wa sheria za nchi.
Kifungu 5
1. Makosa yanayoelezwa katika kifungu 3, aya 1, yatachukuliwa kuwa ni
kati ya makosa yanayoweza kumfanya mtuhumiwa arejeshwe, katika
mkataba wowote wa urejeshwaji wa watuhumiwa baina ya Nchi
Wanachama na yatajumuishwa katika makosa yanayoweza kumfanya
mtuhumiwa arejeshwe kwenye kila mkataba wa urejeshwaji wa
watuhumiwa utakaofanywa katika ya nchi na nchi, kwa mujibu wa
masharti yatakayowekwa kwenye mikataba hiyo.
5
2. Ikiwa Nchi Mwanachama inaweka sharti la kuwa na mkataba katika
urejeshwaji wa mtuhumiwa inapopata ombi la kurejeshwa kwa
mtuhumiwa kutoka Nchi nyingine Mwanachama ambayo haina
mkataba nayo wa urejeshwaji wa watuhumiwa, inaweza kuchukulia
Itifaki hii kuwa msingi wa kisheria wa urejeshwaji huo kwa makosa
yanayotajwa humu. Urejeshwaji huo utafanywa kwa mujibu wa sheria
za nchi inayoombwa.
3. Nchi Wanachama zisizoweka kuwapo kwa mkataba kuwa sharti la
kumrejesha mtuhumiwa zitachukulia makosa haya kuwa ni makosa
yanayoweza kumfanya mtuhumiwa arejeshwe kati zao kwa mujibu wa
masharti yanayotolewa na sheria ya Nchi iliyoombwa.
4. Makosa hayo yatachukuliwa, kwa lengo la urejeshwaji wa
watuhumiwa kati ya Nchi Wanachama, kama vile yamefanyika siyo tu
mahali yalipotendwa bali pia katika himaya ya nchi zinazotakiwa
kuwa na mamlaka hayo kwa mujibu wa kifungu 4.
5. Ikiwa ombi la urejeshwaji wa mtuhumiwa limetolewa kulingana na
kosa lililoelezwa kwenye kifungu 3, aya 1, na Nchi Mwanachama
iliyopewa ombi hilo haimrejeshi au haitamrejesha mtuhumiwa kwa
misingi ya utaifa wa mtuhumiwa huyo, Nchi hiyo itachukua hatua
zifaazo kuiwasilisha kesi kwenye mamlaka zake mwafaka kwa lengo la
kumshtaki.
Kifungu 6
1. Nchi Mwanachama zitapeana msaada mkubwa kuhusiana na taarifa
za upelelezi au jinai ama urejeshwaji wa watuhumiwa zinazoletwa
kwao kulingana na makosa yaliyotajwa katika kifungu 3, aya 1, ikiwa
pamoja na msaada wa kupata ushahidi walionao unaohitajika katika
kesi.
2. Nchi Mwanachama zitatekeleza wajibu wao chini ya aya 1 ya kifungu
hiki kulingana na mikataba yoyote au utaratibu mwingine wa
kupeana msaada wa kisheria unaoweza kuwepo kati yao. Ikiwa
hakuna mikataba au utaratibu kama huo, Nchi Wanachama
zitapeana msaada kwa mujibu wa sheria za nchi zao.
6
Kifungu 7
Nchi mwanachama, kutegemea sheria za nchi zao:
(a) zitachukua hatua za kukamata na kutaifisha, kama itakavyoonekana
inafaa:
(i) bidhaa, kama vifaa, mali na vyombo vingine vilivyotumiwa
kutenda au kuwezesha kosa kutendeka chini ya itifaki hii;
(ii) mapato yanayotokana na makosa hayo.
(b) kutekeleza ombi kutoka Nchi nyingine Mwanachama la kukamata
ama kutaifisha bidhaa au mapato yanayoelezwa kwenye aya ndogo
(a),
(c) kuchukua hatua zinazolenga kufunga kwa muda au kwa kudumu
mahali panapotumika kutendea makosa hayo.
Kifungu 8
1. Nchi Wanachama zitachukua hatua zifaazo kulinda haki na maslahi
ya watoto walioathiriwa kutokana na vitendo vilivyokatazwa chini ya
Itifaki hii katika ngazi zote za mchakato wa kesi ya jinai, hususan
kwa:
(a) kutambua hatari inayowakabili watoto walioathiriwa na kufanya
taratibu za kutambua mahitaji yao mahsusi, ikiwa pamoja na
mahitaji yao maalumu ya kutoa ushahidi;
(b) kuwafahamisha watoto walioathiriwa kuhusu haki na wajibu wao na
mawanda, muda na maendeleo ya mashtaka na mwelekeo wa kesi
zao;
(c) kuruhusu mawazo, mahitaji na wasiwasi wa watoto walioathiriwa
kuwasilishwa na kufikiriwa katika utaratibu ambao maslahi yao
binafsi yanahusika, kwa njia ambayo inaendana na kanuni za
uendeshaji wa sheria za nchi;
(d) kutoa huduma za msaada unaostahili kwa watoto waathiriwa muda
wote wa mchakato wa kisheria;
7
(e) kulinda, inavyostahili, siri na utambulisho wa watoto walioathiriwa
na kuchukua hatua kwa mujibu wa sheria za nchi kuepuka
usaambaaji usiofaa wa taarifa zinazoweza kuwabainisha watoto hao;
(f) kuhakikisha, katika kesi husika, usalama wa watoto walioathiriwa,
pamoja na familia zao na mashahidi dhidi ya vitisho na ulipizaji
kisasi, kwa niaba yao;
(g) kuepuka ucheleweshaji usio wa lazima katika kusikiliza kesi na
utekelezaji wa amri au maagizo ya fidia kwa watoto walioathiriwa.
2. Nchi Wanachama zitahakikisha kutokuwa na uhakika wa umri sahihi
wa mwathiriwa hakutazuia kuanza kwa upelelezi wa kesi, ikiwa
pamoja na upelelezi wenye lengo la kufahamu umri wa mwathiriwa.
3. Nchi Wanachama zitahakikisha kuwa katika kushughulikia kesi
kulingana na mfumo wa taratibu za kesi za jinai zinazohusu watoto
walioathiriwa na makosa yaliyoelezwa katika Itifaki hii, maslahi ya
mtoto yatapewa umuhimu wa juu kabisa.
4. Nchi Wanachama zitachukua hatua za kuhakikisha kuwa watu
wanaoshughulikia waathiriwa wa makosa yaliyokatazwa chini ya
Itifaki hii, wanapewa mafunzo mwafaka, hususan mafunzo ya sheria
na saikolojia.
5. Nchi Wanachama, kwenye kesi zinazostahili, zitachukua hatua za
kulinda usalama na hadhi ya watu na/au mashirika yaliyohusika
katika kuzuia na/au kulinda na kuwarudisha katika hali ya kawaida
waathiriwa wa makosa haya.
6. Hakuna sehemu yoyote ya kifungu hiki itakayofasiliwa kuwa inabadili
au inapingana na haki ya mshtakiwa ya uendeshaji wa mashtaka kwa
haki na bila upendeleo.
Kifungu 9
1. Nchi Mwanachama zitapitisha au kuimarisha, kutekeleza na
kusambaza sheria, hatua za kiutawala, sera za jamii na programu za
kuzuia makosa yaliyotajwa katika Itifaki hii. Umuhimu mkubwa
8
utatolewa katika kuwalinda watoto walio katika hatari kubwa ya
kuathiriwa na vitendo hivi.
2. Nchi Wanachama zitaongeza ufahamu wa umma kwa jumla, ikiwa
pamoja na watoto, kwa kuwapa, kwa njia zote mwafaka, habari, elimu
na mafunzo kuhusu hatua za kuzuia madhara ya makosa
yaliyoelezwa katika Itifaki hii. Katika kutekeleza majukumu yao chini
ya kifungu hiki, Nchi Wanachama zitahimiza ushiriki wa jamii na,
hususan, watoto na watoto walioathiriwa, katika programu hizo za
habari, elimu na mafunzo, ikiwa pamoja na ngazi ya kimataifa.
3. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zinazowezekana kuhakikisha
walioathiriwa na makosa haya wanapata msaada wote wanaostahili,
ikiwa ni pamoja na kuunganishwa tena kikamilifu na jamii na
kurudishwa kwenye hali yao ya kawaida ya kimwili na kisaikolojia.
4. Nchi Wanachama zitahakikisha kuwa watoto walioathiriwa na makosa
yaliyoelezwa kwenye Itifaki hii wanapewa fursa ya kutosha ya kupata,
bila ubaguzi, fidia kwa madhara waliyoyapata kutoka kwa
wanaohusika kisheria.
5. Nchi Wanachama zitachukua hatua mwafaka kwa lengo la kupiga
marufuku kikamilifu utengenezaji na usambazaji wa vifaa
vinavyotangaza makosa yaliyoelezwa katika Itifaki hii.
Kifungu 10
1. Nchi Wanachama zitachukua hatua zote zifaazo kuimarisha
ushirikiano wa mataifa mengi, kikanda na kati ya nchi mbili kwa
ajili kuzuia, kugundua, kupeleleza, kushtaki na kutoa adhabu kwa
wale wanaohusika na vitendo vinavyohusu uuzaji wa watoto,
ukahaba na ponografia inayohusisha watoto na utalii wa kingono
unaohusisha watoto. Nchi Wanachama pia zitaongeza ushirikiano wa
kimataifa na uratibu kati ya mamlaka zao, mashirika yasiyo ya
kiserikali ya kitaifa na kimataifa na mashirika ya kimataifa.
2. Nchi Wanachama zitaongeza ushirikiano wa kimataifa kusaidia
watoto walioathiriwa ili waweze kurudia hali yao ya kawaida ya
9
kimwili na kisaikolojia, kuunganishwa tena na jamii na kurejeshwa
kwao.
3. Nchi Wanachama zitaimarisha ushirikiano wa kimataifa ili
kushughulikia sababu za msingi, kama umaskini na maendeleo
duni, zinazochangia katika kuwaweka watoto hatarini kuuzwa,
kuingizwa kwenye ukahaba na ponografia na utalii wa kingono
unaohusisha watoto.
4. Nchi Wanachama zenye uwezo wa kufanya hivyo, zitatoa msaada wa
fedha, ufundi au msaada wowote mwingine kupitia programu
zilizopo za kimataifa, kikanda, za nchi mbili au nyinginezo.
Kifungu 11
Hakuna chochote katika Itifaki hii kitakachobadili sheria yoyote ambayo inafaa zaidi katika kutekeleza haki za mtoto na ambayo ipo katika
(a) sheria za Nchi Mwanachama;
(b) sheria ya kimataifa inayotekelezwa Nchini humo.
Kifungu 12
1. Kila Nchi Mwanachama, katika kipindi cha miaka miwili tangu kuanza
utekelezaji wa Itifaki hii Nchini humo, itawasilisha ripoti kwa Kamati
ya Haki za Mtoto ikitoa taarifa za kina kuhusu hatua ilizochukua
kutekeleza vipengele vya Itifaki hii
2. Baada ya kuwasilisha ripoti hiyo ya kina, kila Nchi Mwanachama
itaonyesha kwenye ripoti zinazowasilishwa katika Kamati ya Haki za
Mtoto, kwa mujibu wa kifungu 44 cha Mkataba wa Haki za Mtoto,
taarifa yoyote ya ziada inayohusiana na utekelezaji wa Itifaki hii. Nchi
nyingine Wanachama wa Itifaki hii zitawasilisha ripoti kila baada ya
miaka mitano.
3. Kamati ya Haki za Mtoto inaweza kuiomba Nchi Mwanachama kutoa
taarifa zaidi zinazohusu utekelezaji wa Itifaki hii.
10
Kifungu 13
1. Itifaki hii inaweza kutiwa saini na Nchi yoyote ambayo imejiunga na
Mkataba wa Haki za Mtoto au imetia saini Mkataba huo.
2. Itifaki hii inaweza kuridhiwa na iko wazi kukubaliwa na Nchi yoyote
iliyojiunga na Mkataba wa Haki za Watoto. Hati rasmi za kuiridhia au
kuikubali zitahifadhiwa kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa.
Kifungu 14
1. Itifaki hii itaanza kutekelezwa miezi mitatu baada ya kukabidhi hati
rasmi ya kumi ya kuiridhia au kuikubali.
2. Kwa kila Nchi inayoridhia au kuikubali Itifaki hii, baada ya kuanza
kutekelezwa, itaanza kuitekeleza mwezi mmoja baada ya tarehe ya
Nchi kukabidhi hati rasmi za kuiridhia au kuikubali.
Kifungu 15
1. Nchi Mwanachama yoyote inaweza kujitoa katika Itifaki hii wakati
wowote kwa kutoa taarifa ya maandishi kwa Katibu Mkuu wa Umoja
wa Mataifa, ambaye baada ya hapo ataziarifu nchi nyingine
Wanachama wa Mkataba wa Haki za Mtoto na Nchi nyingine zote
zilizotia saini Mkataba huo. Kujitoa kutaanza kutekelezwa mwaka
mmoja baada ya Katibu Mkuu kupokea taarifa hiyo
2. Kujitoa huko hakutaiondolea Nchi Mwanachama majukumu yake kwa
mujibu wa Itifaki hii kuhusiana na tendo lolote lililotokea kabla ya
tarehe ya utekelezaji wa kujitoa huko. Wala kujitoa huko hakutaathiri
kwa njia yoyote ile suala lolote lililokuwa likishughulikiwa na Kamati
ya Haki za Mtoto kabla ya tarehe ya kuanza utekelezaji wa kujitoa
huko.
11
Kifungu 16
1. Nchi yoyote Mwanachama inaweza kupendekeza marekebisho na
kuyapeleka kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa. Katibu Mkuu
atawasiliana na Nchi zote Wanachama kuhusu marekebisho
yaliyopendekezwa na kuziomba zionyeshe iwapo zinaafiki kuitishwa
kwa mkutano wa Nchi Wanachama kwa lengo la kufikiria na kupigia
kura mapendekezo hayo. Iwapo katika kipindi cha miezi minne
kutoka tarehe ya mawasiliano hayo theluthi moja ya Nchi Wanachama
zitapendelea mkutano huo, Katibu Mkuu ataitisha mkutano chini ya
Umoja wa Mataifa. Marekebisho yoyote yatakayopitishwa na Nchi
nyingi Wanachama zilizohudhuria na kupiga kura kwenye mkutano
huo, yatawasilishwa katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ili
yaidhinishwe.
2. Marekebisho yaliyoidhinishwa kwa mujibu wa aya 1 ya kifungu hiki
yataanza kutumika baada ya kuidhinishwa na Baraza Kuu la Umoja
wa mataifa na kukubaliwa na theluthi mbili za wingi wa kura za Nchi
Wanachama.
3. Marekebisho hayo yatakapoanza kutekelezwa, yatahusu Nchi
Wanachama zilizoyakubali, Nchi Wanachama nyingine zitakuwa
zitafuata vipengele vya Itifaki hii na marekebisho yoyote ya awali
waliyoyakubali.
Kifungu 17
1. Itifaki hii ambayo matini zake za Kiarabu, Kichina, Kiingereza,
Kifaransa, Kirusi na Kihispania zina uhalisi sawa, itahifadhiwa kwenye
nyaraka za Umoja wa Mataifa.
2. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa atapeleka nakala zilizothibitishwa
za Itifaki hii kwa Nchi zote Wanachama wa Mkataba wa Haki za Mtoto
na Nchi zote zilizotia saini Mkataba huo.
12