mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa kiswahili: mifano

95
The University of Dodoma University of Dodoma Institutional Repository http://repository.udom.ac.tz Humanities Master Dissertations 2020 Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano kutoka Kichomi na Dhifa Machimu, Josephine Chuo Kikuu cha Dodoma Machimu, J. (2020). Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano kutoka Kichomi na Dhifa (Tasnifu). Chuo Kikuu cha Dodoma, Dodoma. http://hdl.handle.net/20.500.12661/2858 Downloaded from UDOM Institutional Repository at The University of Dodoma, an open access institutional repository.

Upload: others

Post on 28-Oct-2021

15 views

Category:

Documents


0 download

TRANSCRIPT

Page 1: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

The University of Dodoma

University of Dodoma Institutional Repository http://repository.udom.ac.tz

Humanities Master Dissertations

2020

Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa

Kiswahili: Mifano kutoka Kichomi na Dhifa

Machimu, Josephine

Chuo Kikuu cha Dodoma

Machimu, J. (2020). Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano kutoka Kichomi

na Dhifa (Tasnifu). Chuo Kikuu cha Dodoma, Dodoma.

http://hdl.handle.net/20.500.12661/2858

Downloaded from UDOM Institutional Repository at The University of Dodoma, an open access institutional repository.

Page 2: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

MDHIHIRIKO WA UTANZIA KATIKA USHAIRI WA

KISWAHILI: MIFANO KUTOKA KICHOMI NA DHIFA

JOSEPHINE MACHIMU

SHAHADA YA UMAHIRI KATIKA FASIHI YA

KISWAHILI

CHUO KIKUU CHA DODOMA

DISEMBA, 2020

Page 3: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

MDHIHIRIKO WA UTANZIA KATIKA USHAIRI WA

KISWAHILI: MIFANO KUTOKA KICHOMI NA DHIFA

NA

JOSEPHINE MACHIMU

TASINIFU ILIYOWASILISHWA KWA AJILI YA KUTUNUKIWA

SHAHADA YA UMAHIRI KATIKA FASIHI YA KISWAHILI

CHUO KIKUU CHA DODOMA

DISEMBA, 2020

Page 4: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

i

IKIRARI NA HAKIMILIKI

Mimi, Josephine Machimu, ninathibitisha kwamba tasinifu hii ni kazi yangu halisi;

na kwamba, haijawahi kuwasilishwa na wala haitawasilishwa katika Chuo Kikuu

kingine chochote kwa ajili ya kutunukiwa Shahada ya Umahiri au Shahada nyingine

yoyote.

Hairuhusiwi kuiga, kuchapisha, kutoa nakala, kutafsiri wala kusambaza sehemu

yoyote ya tasinifu hii kwa namna yoyote ile bila ya kibali cha maandishi kutoka kwa

mwandishi au Chuo Kikuu cha Dodoma.

Page 5: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

ii

ITHIBATI YA MSIMAMIZI

Aliyesaini hapa chini anathibitisha kwamba, ameisoma tasinifu hii inayoitwa

“Mdhihiriko wa Utanzia katika Ushairi wa Kiswahili: Mifano Kutoka Kichomi

na Dhifa” na anapendekeza ikubaliwe kwa ajili ya kutunukiwa Shahada ya Umahiri

katika Fasihi ya Kiswahili ya Chuo Kikuu cha Dodoma.

-

Page 6: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

iii

SHUKURANI

Awali ya yote, ninashukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema kipindi

chote cha masomo yangu mpaka kuniwezesha kukamilisha tasinifu hii kwa wakati.

Najua sio kwa nguvu zangu ila ni kwa baraka na neema zake alizonijalia nimefika

hapa.

Kwanza, ninapenda kumshukuru msimamizi wangu, Dkt. Aginiwe Nelson Sanga,

ambaye alijitoa sana katika kuniongoza kwa kipindi chote tangu naanza kazi hii.

Ijapokuwa alikuwa na majukumu mengi ya kikazi na kifamilia lakini alijitoa katika

kuniongoza na kunishauri kuanzia hatua ya pendekezo la utafiti mpaka kukamilika

kwa tasinifu hii. Ninakushukuru sana Dkt. Sanga, mwenyezi Mungu akujalie afya

njema ili uendelee kutimiza wajibu wako.

Pili, ninatoa shukurani zangu za dhati kwa walezi wangu, shemeji yangu, Bw.

Leonard Lwabuzala, na dada yangu mpendwa Bi. Jane Machimu, kwa moyo wao wa

ukarimu. Kwa sababu waliacha majukumu yao mengine na kuchukuwa jukumu la

kuwa wazazi kwangu kwa kunisomesha, kunilea, kuniongoza na kunishauri katika

hatua zangu zote za malezi na makuzi mpaka sasa. Sina cha kuwalipa ila nazidi

kuwaombea afya njema na miaka mingi zaidi, Mungu awabariki sana na pale

mlipopungukiwa Mungu awazidishie zaidi.

Tatu, shukurani zangu za dhati ziwafikie wahadhiri wote walionifundisha kozi

mbalimbali kwa kuniongoza na kunishauri katika kipindi chote cha masomo. Pia,

ninawashukuru wanafunzi wenzangu wa umahiri katika fasihi ya Kiswahili mwaka

2018/2020 kwa ushirikiano wao wa dhati kwa kipindi chote cha masomo.

Nne, shukurani za pekee ziende wa ndugu zangu Joachimu Machimu, Deogratias

Machimu, Salome Machimu, Janeth Machimu, Justa Machimu, Suzan Kafuje,

mtumishi Everson Rweramila pamoja na Paul Shayo kwa kunitia moyo pale

nilipokuwa na wakati mgumu na kuniombea.

Page 7: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

iv

TABARUKU

Natabaruku kazi hii kwa marehemu wazazi wangu wapendwa baba yangu mzazi,

Henry Kassian Machimu, na mama yangu mzazi, Magreth Jeremiah Blackwell. Pia,

kwa pacha wangu Justina Henry Machimu pamoja na marehemu dada zangu Juliana

Henry Machimu na Judith Henry Machimu siku zote mpo moyoni mwangu,

inawakumbuka na kuwaombea daima. Mungu azilaze roho zao mahali pema peponi,

Amina.

Page 8: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

v

IKISIRI

Tasinifu hii ilijikita katika kujadili mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa

Kiswahili. Diwani zilizochunguzwa ni Kichomi na Dhifa. Dhana ya utanzia katika

tasinifu hii imetumika kama mbinu bunilizi inayotumia vipengele mbalimbali

vizuavyo huzuni, masikitiko, machungu, majonzi pamoja na maumivu ya mwili,

roho na akili kwa hadhira. Utafiti umeongozwa na malengo mahususi matatu ambayo

ni: kubainisha matukio ya utanzia yaliyodhihirika katika diwani teule, kufafanua

dhima za matumizi ya utanzia katika diwani teule na kufafanua athari za matumizi ya

mbinu ya utanzia kwa wasomaji kupitia diwani teule. Utafiti ulifanyika maktabani na

uwandani. Data ambazo zimetupatia majibu ya tasinifu hii zilikusanywa toka kwa

wataalamu wa fasihi kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma na Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam kwa njia mbili, usaili na uchanganuzi matini. Matokeo yaliyopatikana ni:

kubainika kwa matukio ya utanzia katika diwani teule. Matukio hayo ni: hali ngumu

ya maisha, ulemavu wa viungo, vifungo, maradhi, ukatili, majanga na vifo. Vilevile,

tumebainisha dhima za matumizi ya utanzia katika kazi za fasihi. Dhima hizo ni:

hujenga hisia za woga, hufikirisha, hujenga uhalisia wa maisha na kuibusha majonzi

kwa hadhira lengwa. Utanzia kama mbinu ya utunzi huwa na athari hasi au chanya

katika matumizi yake katika fasihi ya Kiswahili. Athari chanya ni pamoja na:

kufikisha ujumbe, kuakisi uhalisia wa maisha, kuweka karibu msomaji na mwandishi

na kuitafakarisha hadhira. Athari hasi ni: kupunguza wasomaji, ugumu katika

kueleweka na huwapa wasomaji hali ya kukata tamaa kuhusu maisha. Kupitia

tasinifu hii, wasomaji na wahakiki wataweza kufahamu sababu za waandishi kutumia

utanzia katika kazi zao za kiutunzi. Halikadhalika, imeonesha namna mbinu hii

inavyoweza kutumika katika kujenga maudhui, hasa katika utanzu wa ushairi. Zaidi,

tasinifu imebainisha kwamba mbinu ya utanzia inaweza kutumiwa na washairi katika

kujenga maudhui yao, tofauti na hapo mwanzo ambapo utanzia ulizoeleka kuonekana

kwenye tamthiliya pekee.

Page 9: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

vi

YALIYOMO

IKIRARI NA HAKIMILIKI ......................................................................................... i

ITHIBATI YA MSIMAMIZI ...................................................................................... ii

SHUKURANI ............................................................................................................. iii

TABARUKU .............................................................................................................. iv

IKISIRI ......................................................................................................................... v

ORODHA YA VIFUPISHO VILIVYOTUMIKA ...................................................... x

SURA YA KWANZA ................................................................................................. 1

UTANGULIZI ............................................................................................................ 1

1.1 Utangulizi ............................................................................................................... 1

1.2 Ufafanuzi wa Istilahi Muhimu ............................................................................... 1

1.2.1 Tanzia .................................................................................................................. 1

1.2.2 Utanzia ................................................................................................................ 2

1.2.3 Ushairi ................................................................................................................. 2

1.3 Usuli wa Tatizo la Utafiti ....................................................................................... 3

1.4 Tamko la Tatizo la Utafiti ...................................................................................... 5

1.5 Malengo ya Utafiti ................................................................................................. 6

1.5.1 Lengo la Jumla .................................................................................................... 6

1.5.2 Malengo Mahususi .............................................................................................. 6

1.6 Maswali ya Utafiti .................................................................................................. 6

1.7 Manufaa ya Utafiti ................................................................................................. 7

1.8 Mawanda ya Utafiti ................................................................................................ 7

1.9 Historia ya Euphrase Kezilahabi ............................................................................ 7

1.10 Muhtasari wa Sura ya Kwanza ........................................................................... 10

SURA YA PILI ......................................................................................................... 11

MAPITIO YA MAANDIKO NA KIUNZI CHA NADHARIA ........................... 11

2.1 Utangulizi ............................................................................................................. 11

2.2 Mapitio ya Maandiko ........................................................................................... 11

2.2.1 Maandiko kuhusu Utanzia................................................................................. 11

2.2.2 Maandiko kuhusu Ushairi wa Euphrase Kezilahabi ......................................... 15

Page 10: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

vii

2.2.3 Mapengo Yaliyojitokeza Kutokana na Mapitio ya Maandiko .......................... 18

2.3 Kiunzi cha Nadharia ............................................................................................. 18

2.4 Muhtasari wa Sura ya Pili .................................................................................... 21

SURA YA TATU ...................................................................................................... 22

METHODOLOJIA YA UTAFITI .......................................................................... 22

3.1 Utangulizi ............................................................................................................. 22

3.2 Usanifu wa Utafiti ................................................................................................ 22

3.3 Mkabala wa Utafiti ............................................................................................... 22

3.4 Eneo la Utafiti ...................................................................................................... 23

3.5 Walengwa wa Utafiti............................................................................................ 23

3.5.1 Wango Tafitiwa ................................................................................................. 23

3.5.2 Usampulishaji na Sampuli ya Watafitiwa ......................................................... 24

3.5.2.1 Usampulishaji ................................................................................................. 24

3.5.2.2 Sampuli ya Watafitiwa ................................................................................... 24

3.6 Ukusanyaji wa Data ............................................................................................. 26

3.6.1 Njia na Zana za Kukusanyia Data ..................................................................... 26

3.6.1.1 Usaili .............................................................................................................. 26

3.6.1.2 Uchanganuzi Matini ....................................................................................... 26

3.6.2 Mchakato wa Ukusanyaji wa Data .................................................................... 27

3.7 Uchanganuzi wa Data .......................................................................................... 27

3.8 Itikeli ya Utafiti .................................................................................................... 28

3.9 Uhalali na Uthabiti wa Matokeo ya Utafiti .......................................................... 28

3.10 Changamoto za Utafiti na Utatuzi Wake ........................................................... 29

3.11 Muhtasari wa Sura ya Tatu ................................................................................ 29

SURA YA NNE ......................................................................................................... 31

UWASILISHAJI NA MJADALA WA MATOKEO YA UTAFITI .................... 31

4.1 Utangulizi ............................................................................................................. 31

4.2 Utanzia katika Ushairi wa Euphrase Kezilahabi .................................................. 31

4.2.1 Muhtasari wa Diwani Teule .............................................................................. 31

4.2.1.1 Muhtasari wa Diwani ya Kichomi ................................................................. 31

4.2.1.2 Muhtasari wa Diwani ya Dhifa ...................................................................... 33

Page 11: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

viii

4.2.2 Utanzia katika Diwani Teule ............................................................................. 33

4.2.3 Hali Ngumu ya Maisha ..................................................................................... 33

4.2.4 Ulemavu wa Viungo ......................................................................................... 36

4.2.5 Kifungo ............................................................................................................. 37

4.2.6 Maradhi ............................................................................................................. 38

4.2.7 Ukatili ................................................................................................................ 39

4.2.8 Majanga ............................................................................................................. 42

4.2.9 Kifo ................................................................................................................... 44

4.2.10 Mateso ............................................................................................................. 46

4.3 Dhima za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule .......................................... 47

4.3.1 Kujenga Hisia za Woga kwa Hadhira ............................................................... 47

4.3.2 Kufikirisha Hadhira ........................................................................................... 48

4.3.3 Kujenga Uhalisi wa Maisha .............................................................................. 50

4.3.4 Kuibua Majonzi kwa Hadhira ........................................................................... 53

4.3.5 Kujenga Upekee wa mtunzi .............................................................................. 54

4.3.6 Nyenzo ya Kuhuzunisha Hadhira...................................................................... 56

4.4 Athari za Matumizi ya Mbinu ya Utanzia ............................................................ 57

4.4.1 Athari Chanya za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule .......................... 57

4.4.1.1 Nyenzo ya Kufikisha Ujumbe kwa Hadhira .................................................. 57

4.4.1.2 Huakisi Uhalisi wa Maisha ............................................................................ 58

4.4.1.3 Humweka Karibu Mwandishi na Msomaji .................................................... 59

4.4.1.4 Kuitafakarisha Hadhira .................................................................................. 60

4.4.1.5 Kumpambanua Mtunzi ................................................................................... 61

4.4.2 Athari Hasi za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule ............................... 63

4.4.2.1 Kutopata Wasomaji ........................................................................................ 63

4.4.3 Ugumu katika Kueleweka kwa Kazi ya Fasihi ................................................. 64

4.4.4 Athari za Utumizi wa Mbinu za Kisanaa kwa Watunzi Wengine .................... 65

4.4.5 Kukata tamaa ..................................................................................................... 66

4.5 Muhtasari wa Sura ya Nne ................................................................................... 67

Page 12: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

ix

SURA YA TANO ..................................................................................................... 69

MUHTASARI, HITIMISHO NA MAPENDEKEZO ........................................... 69

5.1 Utangulizi ............................................................................................................. 69

5.2 Muhtasari ............................................................................................................. 69

5.3 Hitimisho .............................................................................................................. 70

5.3.1 Utoshelevu wa Nadharia ................................................................................... 70

5.3.2 Mchango Mpya wa Tasinifu ............................................................................. 70

5.4 Mapendekezo kwa Tafiti Zijazo........................................................................... 71

MAREJELEO .......................................................................................................... 72

VIAMBATISHO ...................................................................................................... 77

Page 13: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

x

ORODHA YA VIFUPISHO VILIVYOTUMIKA

BAKITA Baraza la Kiswahili la Taifa

BAKIZA Baraza la Kiswahili Zanzibar

Bi. Bibi

BK Baada ya Kristo

Bw. Bwana

Dkt Daktari (Ph.D)

Ht Hakuna tarehe

Khj Kama hapo juu

Ltd Limited

S. A. W Swalallahu Alaihi Wasalaam

TATAKI Taasisi ya Taaluma za Kiswahili

TUKI Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili

Uk. Ukurasa

UKIMWI Upungufu wa Kinga Mwilini

UWAKI Ukatili wa Kijinsia

Page 14: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

1

SURA YA KWANZA

UTANGULIZI

1.1 Utangulizi

Utafiti wetu ulihusu Mdhihiriko wa Utanzia katika Ushairi wa Kiswahili: Mifano

Kutoka Kichomi na Dhifa. Sura hii ya kwanza inawasilisha taarifa za utangulizi

kuhusiana na mada iliyotafitiwa ili kumpa msomaji picha ya nini kilisukuma utafiti

huu na muundo wa jumla wa tasinifu yenyewe. Hivyo, sura hii ina sehemu tisa (9).

Sehemu hizo ni ufafanuzi wa istilahi muhimu zilizotumika, usuli wa tatizo la utafiti,

tamko la tatizo la utafiti na malengo ya utafiti. Sehemu nyingine ni maswali ya

utafiti, manufaa ya utafiti, mawanda ya utafiti, historia fupi ya mwandishi pamoja na

muhtasari wa sura ya kwanza.

1.2 Ufafanuzi wa Istilahi Muhimu

Tumefafanua istilahi ili kuweka msingi kwa wasomaji na kurahisisha uelewa. Istilahi

zilizofafanuliwa katika sehemu hii ni tanzia, utanzia na ushairi.

1.2.1 Tanzia

TUKI (2004) na BAKITA (2017) wanafasili tanzia kuwa ni habari ya kifo

inayotolewa kwa lengo la kuwafikia watu walio mbali. Katika fasihi, dhana ya tanzia

imekuwa ikihusishwa na utanzu wa tamthiliya ambayo inahusu kuanguka kwa nguli

au mhusika mkuu na kuishia kwa kifo (Wamitila, 2003). Kwa mujibu wa Semzaba

(1997), tanzia ni tamthiliya yenye huzuni kutokana na hatima ya mhusika mkuu

kuwa ya kupatikana na janga. Katika historia yake, tanzia hutokea kutokana na

udhaifu au dosari fulani ya shujaa ambayo inasababisha anguko lake.

Wamitila (2002) anasema, tanzia ni aina ya tamthiliya ambayo huwa na suala la

matendo ya malengo ya dhati. Utanzu wa tamthiliya kama mwigo au uigaji wa tendo

ambalo lina udhati, ukamilifu, ubora na ukuu fulani. Tendo hilo lazima liwe na

uwezo wa kuwaathiri watazamaji na kuwafanya waingiwe na huzuni au kihoro

pamoja na kuwa na uwezo wa kuzitakasa hisia za woga au huzuni. Hapa Wamitila

(khj) amebainisha kuwa tanzia ni yale matendo ya dhati katika tamthiliya. Matendo

hayo ya dhati ni halisi kwa sababu yanatendwa na wanadamu (wahusika). Matendo

hayo huibua hali ya huzuni, masikitiko machungu na woga ndani yake. Kutokana na

Page 15: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

2

dhana ya tanzia ndipo tunaipata dhana ya utanzia ambayo itachunguzwa katika utafiti

huu.

1.2.2 Utanzia

Dhana ya utanzia imetokana na dhana ya tanzia, yaani mambo yanayoibua huzuni au

masikitiko katika tamthiliya. Utanzia ni mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele

mbalimbali vizuavyo majonzi, msawajiko, jitimai na mateso kwa hadhira yake.

Utanzia katika tasinifu hii inamaanisha hali ijengwayo na maneno, matukio au

mazingira yoyote yenye kuwafanya watu kuingiwa na simanzi, wasononeke na

kupata uchungu. Utafiti unaitofautisha dhana ya utanzia na tanzia kutokana na

ukweli kwamba, tanzia kwa kiasi kikubwa hujiegemeza katika utendaji, hususani

matendo ya jukwaani pamoja na kuonesha anguko la mhusika mkuu. Lakini, utanzia

siyo lazima ujitokeze katika matendo ya jukwaani pekee. Kwa mantiki hiyo, utanzia

huweza kujitokeza katika tanzu anuwai za fasihi (simulizi na andishi) na si katika

tamthiliya peke yake (Ponera, 2014; Mazongela, 2016).

1.2.3 Ushairi

Kwa mujibu wa Mulokozi na Kahigi (1982), ushairi ni sanaa inayopambanuliwa kwa

mpangilio maalumu wa maneno fasaha na yenye muwala, kwa lugha ya mkato,

picha, sitiari au ishara, katika usemi, maandishi au mahadhi ya wimbo ili kuleta wazo

au mawazo, kufunza au kueleza tukio au hisi fulani kuhusu maisha au mazingira ya

binadamu kwa njia inayogusa moyo. Kutokana na fasili hiyo, tunaweza kueleza

kuwa ushairi, tofauti na nathari, hauelezi tu, bali huonesha, husawiri na hutupa picha

ya hisi, wazo, hali, kitu au tukio fulani papo hapo huvuta au kuathiri hisia zetu.

Usawiri huo unaofafanuliwa na Mulokozi (2017) unaweza kufanywa kwa mpangilio

wa kijadi wa urari wa vina na mizani na beti, au kwa mpangilio tofauti usiozingatia

urari wa vina na mizani.

Ushairi wa Kiswahili umetokana na nyimbo mbalimbali za kazi. Kabla ya kuja kwa

wageni, hasa Waarabu, ushairi wa Kiswahili ulitolewa kama nyimbo katika matukio

mbalimbali kama vile wakati wa kuwinda, kulima, kuvua, harusi, vita, kubembeleza

watoto na matambiko. Ushairi huo haukuzingatia arudhi za vina na mizani (Senkoro,

1988; Mulokozi, 1996).

Page 16: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

3

Ujio wa Waarabu na dini ya Kiislamu katika Pwani ya Afrika Mashariki katika karne

ya 7BK uliathiri kwa kiasi kikubwa utamaduni wa Waswahili. Waarabu

waliwafundisha Waswahili dini ya Kiislamu, nyimbo za kumsifu Mtume Muhammad

(SAW) na hati ya maandishi ya Kiarabu. Nyimbo hizo (kasda) zilitungwa kwa

kufuata arudhi za vina na mizani. Arudhi za vina na mizani ziliwezesha kasda

kuimbika kwa kufuata midundo maalum na kukaririwa kwa urahisi. Kutokana na

athari hiyo, taratibu Waswahili nao walianza kutunga nyimbo zao mbalimbali kwa

kuzingatia arudhi za vina na mizani. Baada ya muda mrefu, hiyo ikawa sehemu ya

kaida katika utunzi wa ushairi wao. Mashairi ya kale kama Fumo Liyongo, Utenzi wa

Hamziyya, Utenzi wa Siri La’sirari, Utendi wa Tambuka, Utenzi wa Shufaka yana

athari za ushairi wa Kiarabu (TUKI, 1983; Senkoro, 1988).

1.3 Usuli wa Tatizo la Utafiti

Kwa muda mrefu ulimwengu wa fasihi umekuwa ukihusishwa na matumizi ya mbinu

ya utanzia. Mbinu hii ambayo mtunzi hutumia vipengele vinavyozua huzuni

imekuwa maarufu katika tanzu mbalimbali za fasihi ulimwenguni (Soileau, 2006).

Utanzia ni mbinu kongwe na imechipuka kutokana na dhana ya tanzia, yaani matukio

yanayoibua huzuni au masikitiko katika tamthiliya (Wamitila, 2003; Mazongela,

2016). Kwa upande wa tanzia (kama dhana mama) ilianza kushughulikiwa na

Aristotle. Kwa mujibu wa Semzaba (1997), Aristotle alikuwa mtu wa kwanza

ambaye baada ya kuyatazama maandishi ya tamthiliya ya Kigiriki aliandika maana

ya tanzia katika kitabu chake cha Poetics. Kutokana na uchunguzi wake, Aristotle

aliiona tanzia kuwa tamthiliya yenye huzuni ambayo inagusa hisia za watazamaji

kiasi cha kuogopesha na kumwonea huruma mhusika mkuu ambaye hupata janga

(Semzaba, 1997; Wamitila, 2003; Mulokozi, 2017).

Kiusuli, dhana ya tanzia ambayo katika utafiti huu tunairejelea kama dhana mama

imekuwa ikihusishwa na utanzu wa tamthiliya pekee (Semzaba, 1997; Wamitila,

2003). Katika utanzu wa tamthiliya kwa mujibu wa Semzaba (khj), dhana ya tanzia

imegawika katika matapo makuu manne ambayo ni tanzia ya urasimi, tanzia ya

urasimi mpya, tanzia ya kisasa na tanzia ya uhalisia wa ujamaa. Kila tapo la tanzia

lina sifa na mwelekeo wake ambao unaitofautisha na tapo lingine.

Page 17: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

4

Hata hivyo, dhana ya tanzia ni tofauti na utanzia. Utanzia ni mbinu ya ubunilizi

ambayo ni kinyume cha ufutuhi (Ponera, 2014). Mbinu hii hutumika kufafanua

ukosefu wa furaha ambayo mtu huuhisi maishani. Ukosefu huo wa furaha ndio

ambao husababisha hali ya huzuni na masikitiko kwa mtu. Kila mwanadamu

hukumbwa na hali ya huzuni kutokana na mambo mbalimbali anayokumbana nayo.

Mazongela (2016) anatanabahisha kuwa huzuni ni jambo la kawaida kwa

mwanadamu na hivyo ni vizuri na muhimu kutofautisha baina ya ukosefu wa furaha

ya maisha ya kawaida na dalili za hali ya huzuni.

Katika maisha, watu wengi hukumbwa na hali ya jitimai, mateso, sononeko, huzuni

na masikitiko kiasi cha kuwaathiri kisaikolojia na kimaisha. Muathirika wa hali hizo

hukosa hamu ya kuishi na hata kufanya mambo yake kwa makini na ari (Shahid,

1980). Watu hawa huwa na hali ya lawama, hukosa tumaini na kufikia hata hatua ya

kujiua. Hii ni kutokana na ukweli kuwa mawazo yanayoambatana na sononeko la

nafsi au huzuni huwakosesha raha kiasi cha kukata tamaa ya maisha.

Kwa upande wa jamii za ulimwengu, utanzia unaonekana kuchomoza katika nyanja

mbalimbali za maisha, yaani kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni. Mazongela (khj)

anatueleza kuwa katika siasa kuna matukio mengi yanayoibua utanzia kwa jamii.

Matukio haya tunaweza kuyaona katika kampeni za chaguzi mbalimbali za viongozi.

Kiuchumi, kuna matukio ya kitanzia yanayoibuka siku hadi siku na kusababisha

utanzia kwa jamii na taifa kwa jumla. Mfano mzuri, nchini Tanzania kumekuwa na

mapigano ya mara kwa mara baina ya wafugaji na wakulima katika mikoa

mbalimbali, kwa mfano Morogoro. Mapigano hayo husababisha vifo, huzuni na

kukosekana kwa utulivu katika eneo na nchi kwa jumla. Suala hili hurudisha nyuma

maendeleo ya shughuli za kiuchumi kwa wahusika ambazo ni kilimo na ufugaji.

Aidha, kiutamaduni matukio ya utanzia yameweza kusawiriwa kwa namna

mbalimbali. Hapa tunaweza kuona kupitia matukio kama vile unyanyasaji wa

wanawake na ndoa za utotoni. Matendo hayo kwa jumla huwafanya wenye

kutendewa kuwa mbali na furaha na kuwa na huzuni muda wote.

Katika ulimwengu wa fasihi, matumizi ya utanzia yana mizizi madhubuti. Hii ni

kutokana na watunzi mbalimbali kuitumia mbinu hii katika kusawiri hali halisi ya

maisha Soileau (2006). Mathalani, katika fasihi ya Kiarabu, Shahid (khj) anautaja

Page 18: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

5

ushairi wa kasida wa Waarabu kama moja ya fani inayohusisha utanzia. Kupitia

kasida hizo, watunzi huelezea vita, hali ngumu ya maisha, vifo, maombolezo na

mateso aliyoyapata Mtume Muhammad katika kusimamisha dini ya Uislamu.

Katika fasihi ya Kiswahili, halikadhalika, utanzia unaonekana kujitokeza katika

tanzu zote simulizi na andishi (Senkoro, 2011). Kwa mfano, katika fasihi andishi ya

Kiswahili zimepatikana kazi ambazo zimetumia mbinu hii. Hapa tunaweza kuziona

kazi kama vile, Utenzi wa Fumo Liyongo (Muhammed Kijumwa), Utenzi wa Al -

Inkishafi (Seyyid Abdallah bin Ali bin Nassir), Utenzi wa Vita vya Wadachi

Kutamalaki Mrima (Hemed Abdallah El-Buhry), na Sauti ya Dhiki (Abdilatif

Abdalla). Kazi hizo kwa kiasi kikubwa zimebeba utanzia katika kujenga maudhui

yake. Kwa upande wa riwaya, tunaziona riwaya kama Uhuru wa Watumwa (James

Mbotela), Mzimu wa Watu wa Kale (Muhammed Said Abdulla), na Simu ya Kifo

(Faraji Katalambulah) nazo zikitumia utanzia kama kiunzi cha kujenga maudhui

yake.

Kwa yakini, utanzia umekuwa ukijitokeza kwa muda mrefu katika fasihi ya

Kiswahili. Haji (2015) na Moh’d (2016) wamechunguza matumizi ya utanzia katika

riwaya na kasida na kubainisha namna mbinu hii ilivyojitokeza katika kazi za hizo za

kifasihi. Hata hivyo, hadhira imekuwa ikiona ni jambo la kawaida kwa sababu

hakuna misingi imara iliyowekwa kuhusu mbinu hii. Jambo hili linaonesha na

kudhihirisha wazi kuwa mbinu ya utanzia haijashughulikiwa vya kutosha na

wataalamu wa fasihi, hasa katika utanzu wa ushairi. Hivyo basi, hali hii ilimchochea

mtafiti kuchunguza mdhihiriko wa utanzia katika diwani teule za Euphrase

Kezilahabi ikiwa ni kiwakilishi cha kazi anuwai za kishairi.

1.4 Tamko la Tatizo la Utafiti

Utanzia ni mbinu ambayo mtunzi hutumia vipengele mbalimbali vizuavyo huzuni,

masikitiko, jitimai na mateso kwa hadhira (Ponera, 2014). Utanzia ni suala

lisiloepukika katika maisha ya jamii yoyote ile. Kwa kuwa fasihi ni zao la jamii,

suala hili limekuwa likidhihirishwa kupitia kazi mbalimbali za fasihi. Katika fasihi

ya Kiswahili, mbinu ya utanzia imeweza kujitokeza zaidi katika kazi za tamthiliya na

riwaya tofauti na utanzu wa ushairi. Watunzi wa kazi za fasihi wamekuwa

wakiitumia mbinu hii katika kuwasilisha maudhui yao kwa jamii. Baadhi ya

Page 19: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

6

wahakiki na watafiti wameweza kuchunguza mbinu ya utanzia katika kazi za fasihi

ambao ni Haji (2015), Mazongela (2016) na Moh’d (2016) wamechunguza kwa kiasi

kikubwa utanzia katika tamthiliya na riwaya ambapo pengo limejitokeza kwenye

utanzu wa ushairi. Hivyo, mbinu hii katika fasihi ya Kiswahili bado haijatafitiwa vya

kutosha katika utanzu wa ushairi; yumkini, hii ni kutokana na hali na sifa za utanzu

wenyewe kuonekana mgumu kwa wasomaji. Kwa kiasi kikubwa, kutochunguzwa

kwa mbinu hii kunawaathiri wasomaji wa kazi za fasihi. Hii ni kwa sababu,

wasomaji husoma kazi ya fasihi na kushindwa kufahamu hisia za mtunzi kuhusiana

na matukio ya kazi hiyo ya kifasihi. Pia, wanashindwa kufahamu utanzia katika kazi

husika na athari za utanzia kwani kutomakiniwa kwa dhana ya utanzia huweza kuwa

kizuizi cha kuelewa kazi ya fasihi (Soileau, 2006). Utafiti huu ulikusudia

kuchunguza mdhihiriko wa utanzia katika diwani teule za Euphrase Kezilahabi ili

kubainisha vipengele vya utanzia vilivyotumika katika diwani hizo. Aidha,

kubainisha dhima iliyomsukuma mtunzi kutumia utanzia katika diwani zake pamoja

na kuchambua athari za utanzia kwa jamii.

1.5 Malengo ya Utafiti

Utafiti huu ulikuwa na lengo la jumla moja na malengo mahususi matatu.

1.5.1 Lengo la Jumla

Lengo la jumla la utafiti huu ni kuchunguza mdhihiriko wa utanzia katika diwani za

Euphrase Kezilahabi.

1.5.2 Malengo Mahususi

Malengo mahususi ya utafiti huu ni:

a) Kubainisha utanzia katika diwani teule;

b) Kufafanua dhima za utanzia uliotumika katika diwani teule; na

c) Kufafanua athari za utanzia kwa wasomaji wa diwani teule.

1.6 Maswali ya Utafiti

Maswali yaliyouongoza utafiti huu ni:

a) Utanzia unajitokezaje katika diwani teule?

b) Je, utanzia unaotumika katika diwani teule una dhima gani?

Page 20: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

7

c) Utanzia uliotumika katika diwani teule una athari gani kwa msomaji wa

diwani hizo?

1.7 Manufaa ya Utafiti

Utafiti huu unatarajiwa kuleta manufaa yafuatayo: Kwanza, kuwasaidia wahakiki na

wachambuzi wa fasihi, hususani wataalamu wa ushairi, kuelewa na kuitumia mbinu

ya utanzia katika kazi za kifasihi hasa ushairi. Pili, utafiti huu utasaidia kuikuza na

kuendeleza mbinu bunilizi ya utanzia katika kazi za fasihi. Tatu, matokeo ya utafiti

huu yataongeza marejeleo muhimu katika uwanja wa fasihi hususani utanzu wa

ushairi. Nne, utafiti huu utasaidia kukuza na kuendeleza ya fasihi Kiswahili hasa

katika matumizi ya nadharia ya upokezi kwa kufaa kwake katika uchambuzi wa kazi

za kifasihi.

1.8 Mawanda ya Utafiti

Utafiti huu ulijikita katika kuchunguza mdhihiriko wa utanzia katika diwani za

Euphrase Kezilahabi. Utafiti ulichunguza jumla ya diwani mbili zilizoandikwa na

Euphrase Kezilahabi ambazo ni Kichomi (1974) na Dhifa (2008). Uteuzi wa diwani

hizo ulitokana na uchunguzi wa awali kuonesha kuwa matumizi ya mbinu ya utanzia

imetumika kwa kiasi kikubwa katika diwani teule. Diwani nyingine za Euphrase

Kezilahabi kama vile Karibu Ndani (1988) na kazi zake nyinyine za kifasihi,

hazikuchunguzwa kwa namna ya kuzamiwa kwa kina bali zilisomwa na kutazamwa

kwa jicho la jumla katika kutafuta ushikamani kuhusiana na mbinu ya utanzia.

Vilevile, utafiti huu ulishughulikia utanzia katika diwani teule. Mbinu nyingine

mbali na dhana hiyo hazikushughulikiwa ingawa zimerejelewa hapa na pale ili

kujenga hoja na kuweka mkazo katika ufafanuzi.

1.9 Historia ya Euphrase Kezilahabi

Tumeona ni bora kuelezea historia fupi ya Euphrase Kezilahabi kwa sababu ni

muhimu kumwelewa mwandishi wa kazi za fasihi ili kuwa katika nafasi nzuri ya

kuzielewa kazi zake.

Euphrase Kezilahabi alizaliwa kijiji cha Namagondo wilaya ya Ukerewe, mkoani

Mwanza Tanzania tarehe 13/04/1944. Euphrase Kezilahabi ni mtoto wa nane kati ya

watoto tisa wa familia hiyo ya jamii ya Kikerewe. Alipata elimu ya msingi katika

Page 21: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

8

shule ya Nakasahenge mwaka 1952 hadi 1956 na kujiunga na elimu ya sekondari

katika shule ya Seminari ya Mtakatifu Maria, Jijini Mwanza mwaka 1957. Mnamo

mwaka 1967 alijiunga na Chuo Kikuu cha Afrika Mashariki, Dar es Salaam na

kupata shahada ya kwanza. Pia, alitunukiwa Shahada ya Uzamivu katika Chuo Kikuu

cha Wisconcin - Madison huko Marekani mwaka 1985. Euphrase Kezilahabi

aliajiriwa katika ngazi ya Mkufunzi Msaidizi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam

mwaka 1971. Aliendelea na kuwa, Mhadhiri na kuendelea kupanda hadi kufikia

kuwa profesa mshiriki mwaka 1987. Pia, alikuwa mwanachama wa vyama

mbalimbali vya kitaaluma na mtafiti ambaye ameshughulikia nyanja mbalimbali za

fasihi na lugha ya Kiswahili. Kezilahabi amekuwa mhadhiri wa fasihi katika vyuo

mbalimbali ndani na nje ya nchi ya Tanzania. Miongini mwa vyuo hivyo ni Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu Huria cha Tanzania na Chuo Kikuu cha

Botswana (Fuluge, 2013).

Kiimani, Euphrase Kezilahabi alikuwa na msingi wa mafundisho ya dini ya

Kikatoliki kutokana na kupata elimu katika shule ya Seminari. Kutokana na msingi

wa Kikatoliki aliweza kuwa na maadili bora ijapokuwa baadae aliachana na masuala

ya kiseminari. Malezi na makuzi aliyoyapata yamempelekea kuandika kazi za

kifasihi kutokana na mazingira halisi anayoyafahamu. Kwa mfano, katika diwani ya

Kichomi, Dhifa na Karibu Ndani kuna mashairi ya Namagondo I, II, III ambayo

yanaonesha namna mwandishi alivyokuwa akithamini na kuonesha rasilimali

zinazopatikana katika nchi ya Tanzania. Pia, kuonesha asili yake na namna kijiji cha

Namagondo kilivyobadilika kutokana na uhalibifu wa mazingira.

Katika fani ya utungaji, alianza kutunga bunilizi katika fasihi ya Kiswahili mwaka

1960. Kazi yake ya kwanza iliyomtambulisha ni Rosa Mistika (1971). Baada ya hapo

aliendelea kutunga kazi nyingine katika tanzu za riwaya, tamthiliya, ushairi na

hadithi fupi. Mwandishi Euphrase Kezilahabi ametunga kazi mbalimbali za kifasihi

kama riwaya, ushairi, tamthiliya na hadithi fupi kazi hizo ni:

i) Riwaya

a) Rose Mistika (1971) Gamba la Nyoka (1979)

b) Kichwa Maji (1974)

c) Dunia Uwanja wa Fujo (1975)

Page 22: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

9

d) Gamba la Nyoka (1979)

e) Nagona (1990)

f) Mzingile (1991)

ii) Ushairi

a) Kichomi (1974)

b) Karibu Ndani (1988)

c) Dhifa (2008)

iii) Tamthiliya

a) Kaptula la Marx (1996)

Pia, alitunga hadithi fupi kama; Magwanda Kubilya na Vyama Vingi, Mayai Waziri

wa Maradhi, Utapiamlo, Balenzi, Ulingo wa Uchaguzi, Cha Mnyonge Utakitapika

Hadharani na Wasubiri Kifo.

Euphrase Kezilahabi amewahi kupata tuzo mbalimbali kuhusiana na uandishi wake.

Tuzo hizo ni pamoja na tuzo ya Kiitaliano iitwayo Edwardo Sanguinett Memorial

Prize mwaka 1990; tuzo ya Shaaban Robert Memorial Prize, iliyotolewa na Baraza la

Kiswahili la Taifa mwaka 1995, na tuzo ya Zeze ambayo hutolewa na Mfuko wa

Utamaduni kila mwaka kwa ajili ya kuwathamini watu mbalimbali waliotoa

mchango wao katika fasihi ya Kiswahili (Malugu, 2011; Faustine, 2012 na Ponera,

2014).

Kupitia uandishi wake, Euphrase Kezilahabi katika fasihi ya Kiswahili alisaidia

kuleta mapinduzi ya uandishi kwa mtindo mpya katika utanzu wa ushairi, hivyo

kupelekea kuongezeka kwa waandishi wapya ambao walitunga kazi za kishairi na

kuleta maendeleo makubwa katika ushairi wa Kiswahili (Malugu, 2011; na Ponera,

2014).Euphrase Kezilahabi aliaga dunia akiwa na umri wa miaka sabini na sita (76)

mnamo tarehe 09/01/2020. Katika Fasihi ya Kiswahili, atakumbukwa daima

kutokana na mchango wake mkubwa alioutoa katika kuleta mapinduzi ya uandishi

wa kazi za fasihi.

Page 23: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

10

1.10 Muhtasari wa Sura ya Kwanza

Sura hii imefafanua vipengele mbalimbali vya utangulizi. Vipengele hivyo ni usuli

wa tatizo la utafiti, tamko la tatizo la utafiti na malengo ya utafiti. Aidha, sura hii

imebainisha maswali ya utafiti, manufaa ya utafiti, mawanda ya utafiti na historia ya

mwandishi. Katika sura inayofuata tutachambua mapitio ya maandiko na kiunzi cha

nadharia.

Page 24: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

11

SURA YA PILI

MAPITIO YA MAANDIKO NA KIUNZI CHA NADHARIA

2.1 Utangulizi

Utafiti huu ulihusu Mdhihiriko wa Utanzia katika Ushairi wa Kiswahili, ambapo

mifano imedondolewa kutoka katika diwani za Euphrase Kezilahabi za Kichomi na

Dhifa. Sura ya pili inaweka misingi ya kinadharia na kubainisha kilichokwisha

kufanywa na watafiti waliotangulia. Hivyo, sura hii imeshughulikia mapitio ya

maandiko na kiunzi cha nadharia. Pia, imebainisha mapengo yaliyojitokeza kutokana

na mapitio ya maandiko. Kutokana na hilo, sura hii imegawanyika katika sehemu

kuu tatu: Sehemu ya kwanza ni mapitio ya maandiko. Katika sehemu hiyo

tumefafanua maandiko mbalimbali yanayohusiana na mada iliyoshughulikiwa.

Sehemu ya pili ni mapengo ya utafiti. Katika sehemu hiyo tumebainisha mapengo ya

maarifa yaliyotokana na mapitio na maandiko na jinsi yatakavyoshughulikiwa.

Sehemu ya tatu ni kiunzi cha nadharia, ambapo tunafafanua nadharia iliyoongoza

utafiti wetu.

2.2 Mapitio ya Maandiko

Mapitio ya maandiko yamegawanywa katika makundi mawili. Kundi la kwanza

linajumuisha maandiko kuhusu dhana ya utanzia. Kundi la pili linajumuisha

maandiko kuhusu na ushairi wa Euphrase Kezilahabi. Pia, sehemu hii imeyabainisha

mapengo yaliyojitokeza kutokana na kupitia maandiko.

2.2.1 Maandiko kuhusu Utanzia

Mganga (2019) anafafanua matumizi ya ramsa na tanzia katika utenzi wa Al-

Inkishafi Katika utafiti wake, amebaini kuwa ramsa na tanzia kama dhana pacha

zinajitokeza katika utenzi huo. Utafiti huu wa Mganga umefungua njia kwa namna

ulivyoishughulia dhana ya tanzia ambayo ndiyo dhana mama ya utanzia. Utafiti huu

umetusukuma zaidi kuuchunguza utanzia katika mashairi ili kuonesha namna

unavyodhihirika kwa kuchunguza matukio ya utanzia, dhima na athari zake kwa

wasomaji.

Mwangi na wenzake (2017) anafafanua vigezo vya ki-Aristotle vya kitanzia katika

utendi wa Fumo Liyongo. Katika uhakiki wao wamebaini kuwa utendi wa Fumo

Liyongo umejengwa katika misingi ya kitanzia kutokana na mhusika Fumo Liyongo

Page 25: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

12

kuchomwa sindano ya shaba kitovuni na mtoto wake, jambo lililosababisha anguko

lake. Uhakiki huu ulikuwa na nia ya kutaka kudhihirisha kuwa utanzia kama mbinu

ya kiutunzi haijitokezi katika tamthiliya pekee. Kwa hakika, andiko hili lilimsaidia

mtafiti kwa kuweza kufahamu vigezo vya kitanzia vya ki-Aristotle vilivyojitokeza

katika utendi wa Fumo Liyongo. Aidha, andiko hili limeweza kubainisha kuwa

utendi wa Fumo Liyongo umejengwa kitanzia jambo ambalo lilituchochea katika

kuzamia mashairi huru ya Kezilahabi ili kuweza kuchunguza utanzia uliomo ndani

yake.

Mazongela (2016) anafafanua matumizi ya utanzia katika riwaya pendwa ya

Kiswahili. Anabainisha kuwa utanzia upo katika kazi mbalimbali za fasihi (simulizi

na andishi). Aidha, amebainisha aina tatu za utanzia ambazo ni utanzia wa kimwili,

utanzia wa kisaikolojia na utanzia wa kimaumbile. Vilevile, andiko hili limechambua

matukio mbalimbali ya utanzia yanayopatikana katika riwaya teule

zilizoshughulikiwa pamoja na ulinganisho wa riwaya hizo. Andiko hili lilimpa

mwanga mtafiti na kumchochea kuutafiti utanzia katika ushairi wa Kiswahili kama

utanzu mmojawapo wa fasihi ili kuonesha jinsi unavyodhihirika kupitia mashairi ya

Euphrase Kezilahabi. Hivyo, utafiti huu ulisaidia kubainisha matukio ya utanzia

kupitia mashairi teule au vitabu teule pamoja na athari zinazojitokeza na namna

mbinu hii ilivyotumika.

Ponera (2014) anajadili kuhusiana na fasihi na ubunilizi. Katika mjadala wake

anatueleza kuwa ubunilizi huweza kufanywa kwa kutumia mbinu mbalimbali.

Miongoni mwa mbinu hizo ni utanzia. Anaendelea kufafanua kuwa, utanzia ni

kinyume cha ufutuhi. Mbinu hii ya utanzia imekuwa ikitumia vipengele mbalimbali

vizuavyo huzuni, masikitiko, jitimai na mateso kwa hadhira. Andiko hili ni la

muhimu katika utafiti huu kwani lilitupa hamasa ya kuchunguza dhana ya utanzia

jinsi inavyodhihirika katika ushairi wa Kiswahili. Katika andiko hilo, Ponera (khj)

amebainisha tu mambo yanayopelekea utanzia lakini hajaelezea dhima na athari

zinazotokana na mbinu ya utanzia katika kazi za kifasihi.

Haji (2015) anajadili kuhusiana na matumizi ya utanzia katika riwaya teule za Said

Ahamed Mohamed. Katika uchunguzi wake anabainisha kuwa utanzia unapatikana

katika kazi za kifasihi (riwaya, tamthiliya na ushairi). Aidha, uchunguzi wake

Page 26: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

13

unaelezea dhana ya utanzia kwa ujumla na vipengele vya utanzia kama vile, vifo,

ajali, vifungo, mabalaa, ulemavu, vilio, maradhi njaa na mateso kama vilivyotumika

katika riwaya teule. Andiko hili limetupa mwanga katika kuutafiti utanzia katika

ushairi wa Euphrase Kezilahabi kwani limedhihirisha wazi kuwa utanzia

haujajitokeza tu kwenye tamthiliya bali hata katika riwaya na ushairi. Hivyo, kuna

haja ya kubainisha matukio, kufafanua dhima na kufafanua athari za utanzia katika

diwani teaule za Euphrase Kezilahabi.

Chiraka (2011) anahakiki riwaya ya Takadini na kusema kuwa miongoni mwa mbinu

aliyoitumia mwandishi katika kuunda riwaya yake ni mbinu ya utanzia. Mhakiki

anaeleza kuwa riwaya hii ni ya mwendo wa taratibu kutokana na kujaa maudhui

yaliyojaa utanzia mwingi. Ameonesha matukio anuwai yaliyozua utanzia katika

riwaya hii kama vile ugumba wa Sekai kwa muda wa miaka tisa, ulemavu wa

Takadini, vita, upweke wa Sekai na kuuawa kwa walemavu na mapacha katika jamii

ya Sekai. Tahakiki hii ni muhimu katika utafiti huu kwa sababu ilionesha baadhi ya

matukio yaliyoibua utanzia kwa jamii. Zaidi, andiko hili lilitusaidia kuchunguza

utanzia katika ushairi wa Kiswahili ili kubainisha vipengele vya utanzia na athari

zake kwa wasomaji.

Soileau (2006) anatafiti kuhusiana na tanzia katika riwaya za karne ya kumi na tisa.

Katika utafiti wake, ametuonesha tofauti baina ya tanzia na utanzia katika fasihi.

Akitoa tofauti hiyo anasema kuwa tanzia ni kazi ya fasihi hasa katika tamthiliya

ambayo kwa sasa inajitokeza hata katika riwaya, ambayo inatoa maana halisi ya

maisha ya mwanadamu au mateso (anguko) pamoja na kuibua hisia fulani. Wakati

“utanzia” ni mbinu ya kisanaa inayoonesha tabia ya kiutamaduni inayoenea katika

dunia ya fasihi inayojulikana na kuhusiana na taratibu za maisha. Andiko hili

lilitusaidia, kwani limeweza kutoa tofauti ya dhana ya tanzia na utanzia katika fasihi.

Hivyo, andiko hili lilitupa hamasa ya kuangalia mbinu ya utanzia ili kuweza

kuthibitisha kuwa mbinu hii inapatikana hata katika utanzu wa ushairi.

Sengo (1992) anaandika kuhusiana na utamaduni wa Kiswahili wilaya ya Kusini

Unguja. Katika maelezo yake anavitaja vipengele anuwai vya kitamaduni kwa

Waswahili wa Kusini Unguja. Kipengele kimojawapo kinachotajwa ni mazishi.

Anaeleza kuwa, mazishi ni taasisi ya kuwarejesha waja walikotoka, ama

Page 27: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

14

kuwakumbusha walio hai juu ya marejeo hayo kwa Mola. Msiba wa kufiwa huwa ni

faradhi-kifaya kwa Waislamu wote ujiranini. Anaendelea kutueleza kuwa, huzuni za

kufiwa huwa ni za wote na kazi kubwa ya majirani na marafiki ni kuwafariji

wanandugu waliofiwa. Katika andiko hili, Sengo ametuelezea kuhusiana na suala la

kifo na mazishi kama kipengele cha kitamaduni. Kupitia vipengele hivyo, tunaona

jinsi jamii inavyoingia simanzi na masikitiko kutokana na kuondokewa na mwenza

wao. Hivyo basi, tunaona umuhimu wa kubainisha matukio hayo ya utanzia na

namna yanavyodhihirika katika jamii, dhima na athari zake kwa jamii.

Mackeon (1974) anasema kuwa tanzia ni aina ya tamthiliya yenye uzito

unaodhihirika kihisia au kifikra. Tanzia huwa na suala, matendo na malengo ya dhati.

Aristotle alikuwa mtu wa kwanza ambaye baada ya kuyatazama maandishi ya

tamthiliya za Kigiriki aliandika maana ya tanzia katika kitabu chake cha Poetics.

Kutokana na uchunguzi wake aliona tanzia kuwa ni tamthiliya yenye huzuni ambayo

inagusia hisia za watazamaji kiasi cha kuogopesha na kumwonea huruma mhusika

mkuu ambaye hupata janga. Andiko hili lilitupatia dira kuwa hali ya huzuni kwa

mtazamaji au msomaji haipo katika tamthiliya peke yake, bali hata kwenye riwaya na

ushairi. Hivyo, mtaalamu Mackeon ametupa mwongozo juu ya utanzia katika

tamthiliya na kuchunguza matumizi ya mbinu ya utanzia katika ushairi wa Kiswahili.

Moh’d (2016) anashughulikia utanzia katika Kasida za Kiswahili kwa kutumia

mifano kutoka Mkoa wa Mjini Magharibi, Unguja. Anabainisha kuwa utanzia

umedhihirika katika Kasida za Kiswahili. Pia amebainisha maana ya utanzia na

kusema kuwa ni maneno au mazingira yanayozua huzuni, jitimai, majonzi,

masikitiko, majuto na maumivu ya mwili, roho au akili kwa hadhira. Anabainisha

dhima na kuchambua sifa za utanzia zilizojitokeza katika Kasida za Kiswahili.

Andiko hili limeweza kuleta hamasa tulitumie kutokana na kwamba limeelezea

utanzia kwa kina kwa sababu ameelezea dhima na vipengele vya utanzia. Hivyo,

kumchochea mtafiti kuutafiti utanzia katika diwani teule za Euphrase Kezilahabi.

Vilevile, andiko hili limesaidia katika kubainisha dhima za utanzia kupitia diwani

teule na athari zinazojitokeza katika kutumia mbinu ya utanzia.

Page 28: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

15

2.2.2 Maandiko kuhusu Ushairi wa Euphrase Kezilahabi

Wamitila (2016) anaandika kuhusiana na jazanda katika mashairi ya Kiswahili.

Katika maelezo yake, anahakiki mashairi ya Kezilahabi yaliyomo katika diwani ya

Kichomi na Karibu Ndani. Wamitila anatueleza kuwa Kezilahabi ni stadi katika

kutumia jazanda ndani ya tungo zake. Kwa kutumia njia hii, mshairi ameweza

kujenga taswira ya picha kutokana na maelezo yake. Miongoni mwa shairi

lililohakikiwa na Wamitila ni “Chai ya Jioni”. Kupitia shairi hili, msomaji anajiwa na

picha au taswira ya mtu na mwenzake ambao wameketi wakielekea jua linakozama

huku wakinywa chai. Andiko hili lina umuhimu katika utafiti huu kwa kuwa

limeweza kutoa picha ya jumla kuhusiana na mashairi ya Euphrase Kezilahabi

kuhusiana na matumizi ya jazanda. Hata hivyo, halikushughulikia suala la utanzia,

jambo ambalo limetupa hamasa kuchunguza mdhihiriko wake katika diwani teule za

Euphrase Kezilahabi.

Senkoro (1988) anahakiki diwani ya Kichomi ya Euphrase Kezilahabi. Mhakiki huyu

ameonesha dhamira anuwai zilizojitokeza katika diwani hii ikiwa ni pamoja na

harakati za ujenzi wa jamii mpya, ukoloni mamboleo, falsafa ya maisha na ndoa na

mapenzi. Aidha, amehakiki matumizi ya vipengele vya kifani kama matumizi ya

taswira, muundo, mtindo na matumzi ya lugha. Uhakiki wa Senkoro ulikuwa na tija

katika utafiti huu, kwani umeweza kutufungulia njia ya kuyaelewa maudhui ya

diwani ya Kichomi pamoja na mbinu zake za kifani zilizotumika katika diwani hiyo.

Kutokana na uhakiki huu kuwa ni wa jumla mno, tulihamasika kuishughulikia mbinu

ya utanzia na kuona jinsi inavyodhihirika katika diwani teule za Euphrase

Kezilahabi.

Wamitila (2008) anaandika kuhusu mbinu ya ucheshi katika fasihi. Katika andiko

lake ameeleza kuwa ucheshi ni mbinu pana ambayo huweza kuelezwa katika namna

mbalimbali. Kwa kutumia diwani ya Dhifa, Wamitila (khj) anabainisha kuwa

mashairi mengi yaliyomo ndani ya diwani hii yametumia mbinu hii ya ucheshi.

Miongoni mwa ucheshi unaodhihirika humu ni ucheshi wa kibwege ambao

unapatikana katika shairi la ‘Mahojiano na Kifo’ (uk.42). Maelezo haya ya Wamitila

yamekuwa na umuhimu mkubwa katika utafiti huu. Hii ni kutokana na Wamitila

kujikita kuuchambua ucheshi katika mashairi ya Kezilahabi jambo ambalo limeacha

kinyume chake huzuni (utanzia) ambao umeshughulikiwa katika utafiti huu.

Page 29: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

16

Wafula na Njogu (2007) wanasema kuwa kazi za ushairi za Kezilahabi zimetawaliwa

na mawazo ya kidhanaishi hasa kwenye diwani za Karibu Ndani (1988) na Kichomi

(1974). Katika mashairi hayo wameweza kubainisha msimamo wa mwandishi juu ya

maisha, ambapo anaona kuwa maisha hayana maana na hapa dunia tunapita tu.

Wametumia shairi la “Kisu Mkononi” (Kichomi uk. 13) ambalo wameliona

linasawiri ukosefu wa haki, na hatimaye, kujiamulia kwa mwanadamu kutenda

anavyotaka kabla ya kunaswa na mauti. Hivyo, andiko hili lilitusaidia katika kutafiti

zaidi kuhusiana na mbinu ya utanzia katika ushairi wa Kiswahili.

Senkoro (2011) anahakiki taswira katika baadhi ya mashairi ya Euphrase Kezilahabi.

Katika uhakiki wake, Senkoro anatueleza kuwa Kezilahabi amefaulu sana katika

kutumia taswira kwenye mashairi yake. Pia, mhakiki huyu ametushauri kuwa ili

kuweza kuyaelewa mashairi ya Kezilahabi basi hapana budi kwanza kuifahamu

falsafa yake. Akihakiki shairi la “Nimechoka” ambalo linapatikana katika diwani ya

Kichomi, anasema kuwa limezungumzia falsafa ya mwandishi kuhusu maisha.

Mshairi ameonesha ubaya wa maisha na vile ambavyo mtu hachagui wala hajiamulii

mwenyewe kuzaliwa. Tahakiki hii imemjulisha mtafiti kuhusiana na mambo

yanayopaswa kuzingatiwa katika uchunguzi wa mashairi ya Kezilahabi na

kumhamasisha kuichunguza zaidi diwani ya Kichomi ili kuweza kubaini matukio ya

utanzia, dhima za utanzia na athari zake kwa jamii vitu ambavyo

havikushughulikiwa katika tahakiki ya Senkoro.

Gaudioso (2018) anaandika kuhusiana na mikondo ya mtiririko wa ushairi wa

Kezilahabi na Mulokozi. Kwa upande wa Kezilahabi, mwandishi ametumia diwani

ya Kichomi katika kuthibitisha data zake. Gaudioso amebainisha kuwa kupitia diwani

ya Kichomi, Kezilahabi ana mchango mkubwa katika ushairi wa Kiswahili. Hii ni

kwa sababu ushairi wa Kiswahili uliweza kupata mkondo au mwelekeo mpya kupitia

tungo za mtiririko zilizomo ndani ya diwani teule. Makala hii ni muhimu katika

utafiti huu kwani imejadili mikondo mbalimbali ya ushairi wa Euphrase Kezilahabi

na mbinu mbalimbali za kibunilizi zilizotumika. Kwa kuwa Gaudioso

hakushughulikia utanzia, utafiti huu ulijikita kushughulikia utanzia kwa kubainisha

matukio ya utanzia na athari zake kwa jamii.

Page 30: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

17

Mwakibete (2014) alichunguza kejeli na dhihaka katika mashairi ya Euphrase

Kezilahabi. Anabainisha sababu za kutumia kejeli na dhihaka katika mashairi yake

pamoja na kufafanua athari zinazotokana na mbinu hizo za kibunilizi. Pia, amebaini

kwamba kuna taswira, sitiari, ishara na picha zinazojenga mbinu ya kejeli na dhihaka

katika ushairi wa Euphrase Kezilahabi. Andiko hili ni muhimu kwa utafiti huu

kutokana na kuchunguza ushairi wa Euphrase Kezilahabi na kutoa uelekeo kwa

mtafiti kutumia katika utafiti wake. Mwakibete (khj) hakuchunguza utanzia bali

anachunguza kejeli na dhihaka katika mashairi ya Euphrase Kezilahabi ambazo

zimetoa mchango katika kueleweka kwa mashairi yanadhihirisha utanzia. Hivyo,

andiko hili limetupa hamasa ya kuangalia mbinu ya utanzia katika diwani teule za

Euphrase Kezilahabi.

Acquaviva (2004) anaandika kuhusiana na jazanda za njozi katika mashairi ya

Euphrase Kezilahabi. Anabainisha sitiari na mafumbo yanayojitokeza katika diwani

ya Kichomi (1974) na Karibu Ndani (1988). Anaendelea kuelezea namna njozi za

ulimwengu zinavyotokeza katika ushairi wa Kezilahabi zinafanana sana na zile za

mtu anayeweweseka akiwa usingizini. Jazanda za njozi hizo zinadhihirika katika

diwani ya Kichomi kwenye shairi la “Wimbo wa Mlevi” (uk.64). Makala hii imetupa

mwanga kwa sababu inajadili juu ya sitiari na mafumbo yalivyojitokeza katika

mashairi ya Euphrase Kezilahabi. Acquaviva hajazungumzia utanzia ila anatoa picha

ya jumla ya ushairi wa Euphrase Kezilahabi, hivyo utafiti utajikita katika kubainisha

matukio, dhima na athari ya utanzia katika diwani teule.

Gaudioso (2014) anajadili kuhusiana na kuwako na wakati, mipaka ya lugha kama

hatua za falsafa katika mashairi ya Euphrase Kezilahabi. Vilevile, anashughulikia

namna lugha ilinavyotumika katika mashairi ya Kezilahabi na namna yanavyoendana

na wakati husika. Anaelezea umuhimu wa lugha katika mashairi ya Kezilahabi

pamoja na mgogoro katika lugha ya kishairi. Pia, anafafanua falsafa ya mtunzi na

kulinganisha na wanafalsafa wa Magharibi kama Martin Heidegger na Friederich

Nietzsche. Makala hii ina umuhimu katika utafiti huu kwa sababu imeonyesha

falsafa ya mwandishi ambayo imetusaidia kufahamu mbinu ya kitanzia ilivyojitokeza

kwa mwandishi Euphrase Kezilahabi. Hivyo, andiko hili limetupa mwanga katika

kuchunguza zaidi juu ya utanzia katika diwani teule.

Page 31: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

18

2.2.3 Mapengo Yaliyojitokeza Kutokana na Mapitio ya Maandiko

Kwa jumla, maandiko tuliyoyapitia hapo juu yamejikita katika kushughulikia mambo

mbalimbali yanayohusiana na dhana ya utanzia pamoja na ushairi wa Euphrase

Kezilahabi. Hata hivyo, kutokana na mapitio ya maandiko hayo tumebaini kuwa

utanzia katika fasihi ya Kiswahili si toshelevu kwa sababu imejitokeza katika utanzu

wa tamthiliya na riwaya licha ya mbinu hii kuwaathiri sana watunzi wa kazi za

fasihi. Pia, kwa utanzu wa ushairi imekuwa shida sana kwa wasomaji na wahakiki

kuielewa mbinu ya utanzia katika kazi kwa urahisi na kuonekana kuwa ni ngumu.

Kutokana na maandiko tuliyoyapitia tulibaini mapengo yafuatayo: Mosi,

kutobainishwa kwa matukio ya utanzia katika ushairi wa Kiswahili. Pili,

kutofafanuliwa kwa kina dhima za matumizi ya utanzia katika ushairi wa Kiswahili.

Tatu, kutochunguzwa kwa athari za utanzia katika ushairi wa Kiswahili. Hivyo,

kutokana na mapengo hayo, tasinifu hii imekusudia kuyaziba kwa kubainisha

matukio ya utanzia yanavyodhihirika katika diwani teule. Pia, utafiti umebainisha

dhima za utanzia katika diwani teule. Na mwisho, tumefafanua athari za utanzia kwa

wasomaji kupitia diwani teule.

2.3 Kiunzi cha Nadharia

Utafiti huu uliongozwa na nadharia ya Upokezi. Uteuzi wa nadharia hii ulitokana na

ukweli kwamba, mihimili yake inaumana na malengo ya utafiti wetu. Hivyo,

ukusanyaji wa data, uchambuzi na uwasilishaji wake ulifanywa kwa kuzingatia

mihimili ya nadharia ya upokezi.

Kwa mujibu wa Wafula na Njogu (2007), upokezi ni nadharia inayoshughulikia

upokeaji wa matini za fasihi zinayohusiana na ulimbwende na mitazamo ya

kisaokolojia. Kimapokeo, msomaji huwa na mawazo juu ya matini anayoipitia.

Kutokana na tajriba ya usomaji, msomaji hupata hisi maalumu. Utunzi na upokeaji

wa sanaa hushirikishwa sana na hisi kwa mujibu wa imani na nadharia za

kilibwende. Hisi ndizo humpa mwanasanaa msukumo wa kutunga. Vilevile, msomaji

anatazama kuipokea kazi ya fasihi kwa kuzingatia mielekeo yake binafsi.

Nadharia hii imeanza kupata mashiko zaidi kuanzia miaka ya sabini ya karne ya

ishirini. Waasisi wake wakuu ni Wolfgang Iser (1974, 1978), Stanley Fish (1980),

James Tompkins (1980), na Haus Robert Jauss (1982). Nadharia hii inayohusisha

Page 32: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

19

upokeaji wa sanaa na inanuia kubainisha na kufafanua kadhia zinazomkutanisha

msomaji na kazi ya fasihi. Wanafasihi wa nadharia hii hujishughulisha na maswali

manne ya msingi ambayo ni;

(i) Kuna uwiano wowote kati ya maana ya kazi inayosomwa na jinsi

msomaji anavyohakiki?

(ii) Je, kila kazi ya fasihi ina maana kufuatana na msomaji binafsi na jinsi

msomaji anavyoichukulia?

(iii) Kuna wasomaji ambao husoma na kufasiri kazi ya fasihi vizuri zaidi

kuliko wasomaji wengine?

(iv) Msomaji hutumia vigezo gani kujijulisha iwapo mawazo yake juu ya kazi

fulani yanafaa au hayafai?

Baada ya msomaji kujiuliza maswali ya muhimu katika nadharia ya upokezi katika

kazi ya sanaa, hufuata hatua tatu ili kuelewa kazi ya fasihi. Hatua hizo ni:

(a) Kurejelea kazi hiyo inayosomwa kwa tafsiri ili ithibitishwe kwamba kazi

hiyo inaafikiana na yale yanayokumbukwa na msomaji.

(b) Kubainisha jinsi miktadha ya matini isiyohusika moja kwa moja na

maandishi inavyoweza kuhusishwa na kutenganishwa na msomaji.

(c) Kudhihirika kwa maoni ya msomaji yanayofungamana na mada muhimu za

hadithi.

Adena Rosmarin (katika Murfin, 1991) anasema, kazi ya fasihi ni kama kinyago

ambacho hakijakamilika. Mchongaji wa kinyango hiki kisichokuwa kamili hujaribu

kukikamilisha. Hata katika kazi ya fasihi, msomaji huikamilisha kazi ya sanaa kwa

kuijaliza kwa usomaji makini au huidhalilisha kazi hiyo kwa usomaji wa kiholela.

Nadharia inasisitiza athari za kazi ya kifasihi juu ya akili na maarifa ya mwandishi.

Athari zinaweza kufasiriwa na wasomaji mbalimbali kwa namna tofauti tofauti. Fish

anasema, sanaa ya maneno haichanganuliwi kwa kutumia mikakati ya jambo la

kisayansi katika maabara. Jaribio la kisayansi laweza kuonyesha ujuzi uliofanikiwa

au ambao haujafanikiwa. Anayefanya jaribio la kisayansi ameweka mpaka wa kihisia

na kimawazo kati ya nafsi yake na jambo linalomshughulisha. Tofauti na hayo

Page 33: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

20

mhakiki wa kazi ya fasihi hawezi kujitenga na riwaya, tamthiliya au ushairi

aliousoma.

Iser na Fish wanadai kwamba kazi ya fasihi mara kwa mara ina mapengo mengi,

msomaji anapaswa kuyaziba mapengo hayo. Kutokana na kujiuliza, msomaji

ulazimika, kutunga matini mpya ambazo zimechochewa na kuzalika kutokana na

matini asili zilizopo kwenye kurasa. Maneno na sentensi zilizomo kwenye matini

asilia humsukuma msomaji kuandika maneno mengine mapya na sentensi nyingine

mpya. Hivyo, msomaji anajukumu kubwa na gumu la kuandika kazi mpya

iliyotokana na matini asilia. Jukumu hili ni kujizatiti kufahamu kazi ya fasihi kadiri

ya uwezo wake. Kwa mujibu wa Ponera (2014), mihimili ya nadharia ya upokezi

kama ifuatavyo:

Mosi, nadharia hii inamlenga moja kwa moja msomaji wa matini ya kifasihi,

msomaji anapaswa kuijenga upya kazi ya fasihi kulingana na kile alichokielewa

kutoka kwenye hiyo matini asilia. Pili, nadharia hii hushughulikia uhusiano uliopo

kati ya fanani wa kazi ya fasihi, msomaji wa kazi, mchakato wa usomaji pamoja na

maana ya matini.

Hivyo basi, mihimili hiyo ndiyo iliyotumika katika ukusanyaji wa data, uchambuzi

na uwasilishaji wa matokeo ya utafiti. Vipengele vya kitanzia vilichunguzwa kwa

kuhusishwa na vipengele vingine vya maisha ya mtunzi kama vile, matukio ya

kihistoria yaliyojiri kabla au wakati wa utunzi, tabia na mwenendo halisi, hali halisi

ya maisha tangu kipindi cha baada ya kazi husika kutungwa hadi sasa na jografia ya

alipokuwa mtunzi (kurejelea maana ya kazi iliyosomwa). Aidha, uchunguzi

ulihusisha mabunio na fikra binafsi za mtafiti kuhusiana na lugha na mawazo

mbalimbali yaliyojitokeza katika diwani teule (hapa tuliweza kubainisha miktadha ya

matini inayohusiana na maandishi). Vilevile, uchambuzi wa data ulizingatia mtindo

mahususi wa lugha ambao mtunzi aliutumia katika kuwasilisha mawazo yake kwa

kutumia mbinu ya utanzia (hapa kudhihirisha maoni ya msomaji yanavyofungamana

na mada husika).

Page 34: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

21

2.4 Muhtasari wa Sura ya Pili

Sura hii imebainisha maandiko mbalimbali yanayohusiana na mada ya utafiti.

Maandiko hayo yamegawanywa katika makundi mawili. Kundi la kwanza

limejumuisha maandiko kuhusu dhana ya utanzia; kundi la pili limejumuisha

maandiko kuhusiana na ushairi wa Euphrase Kezilahabi. Pia, sura hii imeyabainisha

mapengo yaliyojitokeza kutokana na kupitia maandiko. Aidha, katika sura hii

tumefafanua nadharia ya upokezi ambayo ndiyo ilituongoza katika utafiti wetu. Sura

inayofuata inafafanua methodolojia ya utafiti, ambapo vipengele anuwai vya

kimethodolojia vimejadiliwa kwa kina.

Page 35: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

22

SURA YA TATU

METHODOLOJIA YA UTAFITI

3.1 Utangulizi

Sura hii ya tatu katika utafiti uliohusu Mdhihiriko wa Utanzia katika Ushairi wa

Kiswahili: Mifano Kutoka Kichomi na Dhifa inawasilisha namna utafiti

ulivyofanyika ili kupata data stahiki. Hivyo, katika sura hii tumefafanua

methodolojia1 ya utafiti.Katika sura hii tumevifafanua vipengele vya methodolojia ya

utafiti ambavyo ni: usanifu wa utafiti, mkabala wa utafiti, eneo la utafiti, walengwa

wa utafiti, ukusanyaji wa data, njia na zana za kukusanyia data na mchakato wa

ukusanyaji wa data. Vipengele vingine ni uchanganuzi wa data, itikeli za utafiti,

uhalali na uthabiti wa matokeo ya utafiti na changamoto za utafiti na utatuzi wake.

3.2 Usanifu wa Utafiti

Kwa mujibu wa Kothari (2004), usanifu wa utafiti ni mpango wa kazi wa jumla wa

namna ya kufanya utafiti. Hii ni hoja ya kifikra kabla ya mtafiti hajaanza kufanya

utafiti wake. Utafiti huu ulihusisha usanifu wa kifenomolojia. Usanifu huu

hujihusisha na kusaka data za uyakini wa fenomena husika kwa kujigeza sana katika

uelewa, mtazamo na tajiriba za watafitiwa. Hii humaanisha kuwa, mtafiti hutakiwa

kutengeneza mazingira ya kuwa na muda unaomwezesha kuonana ana kwa ana na

watafitiwa wake ili kupata data sahihi na za kina kuhusu jambo analolitafiti (Ponera,

2019).

3.3 Mkabala wa Utafiti

Utafiti huu ulitumia mkabala wa kitaamuli. Ponera (2016) anasema kuwa, katika

mkabala wa kitaamuli, utafiti hutumia zaidi tafakuri katika kuhusisha taarifa

mbalimbali za kitafiti, kisha kutoa ufafanuzi kwa kuzingatia misingi ya nadharia

husika pamoja na ithibati bayana zipatikanazo uwandani.

Utafiti huu ulikuwa wa maktabani na uwandani ambapo data zake zilikusanywa kwa

kufuata mkabala wa kitaamuli. Enon (1998) anabainisha kuwa mkabala wa kitaamuli

ni njia ya ukusanyaji wa data zinazolenga kupata data kwa njia ya maelezo. Naye

Kothari (2004) anatueleza kuwa, mkabala wa kitaamuli unaleta matokeo yasiyoweza

1 Methodolojia ni jumla ya seti na taratibu zinazofuatwa katika ufanyaji wa jambo fulani. Hivyo,

methodolojia huangazia sayansi nzima ya kuteua, kutumia na kuhusisha mbinu na hatua mbalimbali

zinazotumika kuendesha utafiti (Ponera, 2019).

Page 36: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

23

kupimwa na yasiyoonesha idadi au kiasi na unalenga kutoa maelezo zaidi. Hivyo

basi, katika utafiti huu data hazikuwasilishwa kitakwimu. Hii ni kwa sababu mkabala

huu unahusika na ukusanyaji wa data kwa njia ya maelezo bila ya kuhusisha

takwimu. Mkabala huu unafaa zaidi kutumika katika tafiti zinazohusu masuala ya

sayansi ya jamii kama vile fasihi. Aidha, haufungwi na kanuni na huweza kutumika

pamoja na njia zingine kama vile mahojiano na udurusu wa maandiko ambazo

zimetumika katika utafiti huu. Data zipatikanazo kwa kutumia mkabala huu

hupambanuliwa kiimani, kiitikadi au kimtazamo. Hivyo, zinaweza kuwa na tafsiri

nyingi (Enon, 1998; White, 2002) Kwa mantiki hiyo, ukusanyaji wa data,

uchanganuzi wa data na utoaji wa matokeo ya utafiti vilifanywa kwa kutumia

mkabala wa kitaamuli.

3.4 Eneo la Utafiti

Utafiti huu ulifanyika katika mikoa ya Dar es Salaam na Dodoma. Sababu ya

kuuchagua mkoa wa Dar es Salaam ni kwa kuwa kuna maandiko ya kimaktaba

kutoka makavazi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam pamoja na ukongwe wa chuo

hicho. Makavazi hayo yalimsaidia mtafiti kudurusu machapisho mbalimbali kama

vile vitabu, majarida na tasnifu zilizohusiana na mada yetu ya utafiti. Pia,

walipatikana wataalamu waliojishughulisha na uhakiki au utafiti kuhusiana na diwani

za Euphrase Kezilahabi. Mkoa wa Dodoma tuliuchagua kwa sababu ya kuwapo kwa

matini yanayohusiana na fasihi ya Kiswahili pamoja na wataalamu wa fasihi ya

Kiswahili kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma ambao walisailiwa na mtafiti ili kupata

data zinazoendana na utafiti wetu.

3.5 Walengwa wa Utafiti

Walengwa wa utafiti ni wale wote watakaohusika katika utafiti husika (Ponera,

2014). Katika utafiti huu, walengwa wa utafiti waligawanyika katika makundi

mawili ambayo ni wango tafitiwa na sampuli ya watafitiwa.

3.5.1 Wango Tafitiwa

Kwa mujibu wa Ponera (2014), wango tafitiwa ni vitu vyote ambavyo mtafiti

anaweza kuvitumia kwa ajili ya kupata data za utafiti wake. Jamii ya watafitiwa

huweza kuwa kundi la watu, eneo fulani la kijografia, aina ya miti au aina fulani ya

Page 37: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

24

maandiko. Hivyo, taarifa za utafiti huu zilipatikana kutoka katika makundi

yafuatayo:

i. Vitabu anuwai vya ushairi vilivyoandikwa na Euphrase Kezilahabi: Kupitia

diwani hizi tuliweza kuona utanzia jinsi ulivyodhihirika;

ii. Wataalamu wa fasihi ya Kiswahili waliozisoma au kuzihakiki diwani za

Euphrase Kezilahabi;

iii. Wasomaji wa diwani teule za Euphrase Kezilahabi ambao ni wanafunzi wa

shahada ya umahiri na uzamivu na wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dodoma

na Dar es Salaam. Hawa walisaidia katika kutuelezea namna

wanavyoathirika na utanzia uliomo katika diwani teule za Eupharse

Kezilahabi.

3.5.2 Usampulishaji na Sampuli ya Watafitiwa

Usampulishaji na sampuli ni istilahi muhimu katika mchakato wa utafiti kutokana na

mada ya utafiti. Maelezo kuhusu istilahi hizi ni kama ifuatavyo:

3.5.2.1 Usampulishaji

Usampulishaji ni mchakato wa kuteua sehemu ndogo ya kundi kubwa la watafitiwa

kwa lengo kumpatia mtafiti taarifa ambazo anazitumia kutoa majumuhisho

yanayowakilisha kundi la watafitiwa (Trochim, 2006). Pia, Sanga (2018) anasema

usampulishaji ni mbinu ya kuteua sehemu ndogo ya wanajamii katika jamii kubwa ili

watumike kama kiwakilishi cha sifa, mienendo, mawazo, hisia na mitazamo ya jamii

nzima. Sanga (khj) anaendelea kusema kwamba, idadi ya watafitiwa inaweza

kupatikana kwa kuzingatia malengo ya utafiti, data zinazokusanywa na sifa za

watafitiwa. Mara kwa mara katika utafiti wa kitaamuli watafitiwa huwa wachache

tofauti na utafiti wa kitakwimu ambao huhitaji majibu kutoka kwa watafitiwa. Utafiti

wa kitaamuli uhitaji mtafiti kutumia muda mwingi kuwahoji watafitiwa ili kuweza

kupata maelezo yao kwa kina.

3.5.2.2 Sampuli ya Watafitiwa

Sampuli ni sehemu ya jamii ya watu iliyochaguliwa ili kutoa taarifa zitakazokuwa

kiwakilishi cha jamii nzima. Katika utafiti huu, mtafiti alitumia sampuli lengwa.

Kwa mujibu wa Kombo na Tromp (2006), usampulishaji lengwa ni mbinu ambayo

mtafiti hulenga kundi fulani la watu, vitu au dhana zinazoaminika na kuwa na

Page 38: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

25

uhakika juu ya utafiti husika. Sababu ya kuchagua mbinu hii ni kwamba, inampa

uhuru mtafiti wa kuteua watafitiwa kwa mujibu wa kusudio na malengo ya utafiti

wake. Prewitt (1985) anasema kuwa idadi ya sampuli haihitaji kuwa sawa na watu

waliolengwa katika utafiti lakini sifa ya sampuli itakiwayo katika idadi ni muhimu

kufikiwa. Vilevile, mbinu ya sampuli lengwa husaidia kupata data zenye ukubalifu

na utoshelevu na husaidia katika kuokoa muda pamoja na kupunguza gharama.

Aidha, mbinu hii hufaa zaidi katika utafiti wa kitaamuli kama huu, yaani usiotumia

takwimu.

Watafitiwa walichaguliwa kutokana na ufahamu wao na jinsi walivyotosheleza

matakwa na malengo ya utafiti huu. Sampuli hiyo ilichaguliwa kutoka katika

makundi yote yaundayo wango la watafitiwa ili kutoa fursa sawa kwa kila mlengwa

kutafitiwa. Katika kufanikisha hili, vigezo vilivyotumika kuwapata ni viwili

ambavyo ni asili ya utafiti ambao ni wa kitaamuli na miongozo ya kinadharia kuhusu

tafiti za kitaamuli kutoka kwa wataalamu wa utafiti kama vile Kothari (2004) na

Ponera (2019) Hivyo, sampuli yetu katika utafiti huu ilikuwa kama ifuatavyo:

i) Diwani mbili za ushairi zilizotungwa na Euphrase Kezilahabi ambazo ni

Kichomi na Dhifa. Uteuzi wa diwani hizi ulitokana na ukweli kwamba

zimetumia mbinu ya utanzia kwa kiasi kikubwa;

ii) Wataalamu wanne waliosoma au kuzihakiki diwani teule. Hawa walisaidia

katika kueleza maana ya mashairi ya Kezilahabi na mbinu zake; na

iii) Wasomaji wanane wa diwani teule za Euphrase Kezilahabi ambao ni

wahadhiri pamoja na wanafunzi wa shahada ya uzamivu. Hawa walisaidia

katika kutuelezea namna wanavyoathirika na utanzia uliomo katika diwani

teule.

Sampuli hii ilipatikana kwa kutumia usampulishaji sinasibu ambapo mchakato wa

kuwateua watafitiwa ulifanywa na mtafiti kwa kuelekeza fikra kwa baadhi ya

watafitiwa kulingana na wanavyoweza kukidhi data za utafiti. Mara nyingi, aina hii

ya usampulishaji inahusu tafiti zinazihitaji sampuli ndogo na hutumika hasa kwa

tafiti za kitaamuli. Usampulishaji huo umefanywa kwa kutumia mbinu ya uchaguzi

lengwa. Uchaguzi lengwa unahusiana na kuchagua watafitiwa kwa kujiegemeza

katika kuwapo kwa sifa za kipekee zinazofanya ufaafu na uhusika wao katika utafiti

Page 39: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

26

husika kuwa wa upekee. Mtafiti ameweza kuwateua watafitiwa kutokana na ufahamu

maarifa waliyonayo kuhusiana na mada ya utafiti pamoja ubobevu wao katika kazi

za Euphrase Kezilahabi.

3.6 Ukusanyaji wa Data

Sehemu hii inafafanua njia na zana mbalimbali zilizotumika katika ukusanyaji wa

data pamoja na mchakato wa kukusanya data.

3.6.1 Njia na Zana za Kukusanyia Data

Ukusanyaji wa data ulifanyika kwa kutumia zana mbalimbali kama vile kompyuta

pakatwa, simu kwa ajili ya kurekodi, kamera ndogo ya picha za mgando, mwongozo

wa usaili, mwongozo wa uchanganuzi wa matini, kalamu na daftari dogo. Njia

zilizotumika kukusanyia data ni usaili na uchanganuzi wa matini. Mtafiti alitumia

njia zaidi ya moja kwa sababu ya kuleta uhalali na uthabiti wa matokeo ya utafiti

wake. Pia, kutokana na ukweli kuwa hakuna njia moja ya ukusanyaji wa data

inayojitosheleza (Cohen na wenzake, 2007).

3.6.1.1 Usaili

Kombo na Tromp (2006) wanafafanua usaili kuwa ni njia ya kukusanya data kwa

kuhusisha mazungumzo baina ya mtafiti na mtafitiwa kuhusu jambo ambalo mtafiti

anakusudia kulipata. Hii ni njia inayotumika sana katika tafiti zinazotumia mkabala

wa kitaamuli (Kothari, 2004). Kwa mujibu wa King’ei na Kisovi (2005), usaili

unaweza kuwa wa ana kwa ana au kwa nyenzo za kielektroniki kama vile simu kwa

ajili ya kuendesha mazungumzo. Njia hii ni muhimu sana kwani ilimwezesha mtafiti

kupata data za awali na za kina. Pia, mtafiti aliweza kuuliza maswali ya ziada iwapo

kuna haja ya kufanya hivyo (Kothari, 2004; Hays na Sigh, 2012; Maxwell, 2013).

Mtafiti aliuliza maswali kwa wataalamu mbalimbali wa taaluma ya Fasihi kwa

kutumia mwongozo wa maswali ya usaili ulioandaliwa.

3.6.1.2 Uchanganuzi Matini

Uchanganuzi wa matini ni njia ya kukusanya data ambapo taarifa hukusanywa

kutoka kwenye vyanzo mbalimbali vya maandishi (Maxwell, 2013). Hivyo, humpa

mtafiti undani wa suala linalotafitiwa kwa kulinganisha na kupatanisha ushahidi

uliopatikana katika vyanzo vya awali. Vilevile, taarifa za njia hii ya uchanganuzi

Page 40: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

27

matini huwa hazibadiliki na zinaweza kupitiwa na wengine. Uchanganuzi wa matini

unahusisha vitabu teule. Kwa kutumia mwongozo wa uchanganuzi wa matini, mtafiti

alidurusu na kuchanganua matini zinazohusiana na mada ya utafiti ili kupata data na

kushadidia hoja na data za msingi. Katika kufanikisha hili, mtafiti alitumia maktaba

ya Chuo Kikuu cha Dodoma na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili kusoma

machapisho yaliyohusiana na mada ya utafiti ili kupata data za upili.

3.6.2 Mchakato wa Ukusanyaji wa Data

Ukusanyaji wa data za utafiti ulizingatia taratibu zinazoongoza mchakato wa kufanya

utafiti. Mosi, tuliomba rihusa ya kufanya utafiti kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma.

Pili, tuliomba ridhaa ya kufanya utafiti katika mamlaka husika kabla ya kuanza

shughuli ya ukusanyajiwa data za uwandani na maktabani. Tatu tuliomba ridhaa kwa

watafitiwa na kuwaeleza malengo na makusudio ya utafiti huu, muda tutakaotumia

katika utafiti pamoja faidi na athari zitakazojitokeza tusipopata ushirikiano wao.

Data zilikusanywa kutoka maktabani na uwandani. Data za maktabani zilikusanywa

kutoka katika tasinifu, majarida vitabu, makala na data za mtandaoni. Mchakato wa

ukusanyaji data uliongozwa na mwongozo wa uchanganuzi matini na ulitumia

mwezi mmoja katika kukusanya data. Mwongozo wa usaili ulitumika kukusanyia

data za uwandani. Data zilikusanywa kutoka kwa wataalamu wa fasihi kwa njia ya

mahojiano. Ukusanyaji wa data za uwandani ulifanyika kwa majuma matatu katika

mikoa ya Dar es Salaam tulitumia jumamoja na Dodoma majuma mawili.

3.7 Uchanganuzi wa Data

Uchanganuzi wa data ni mchakato wa kuzishughulikia data zitakazopatikana katika

mchakato wa ukusanyaji ili ziweze kueleweka zaidi (Kothari, 2004). Data za utafiti

huu zilichanganuliwa kwa kutumia mbinu ya kusimbisha maudhui. Kwa mujibu wa

Ponera (2019), mbinu hii ni maarufu katika kufafanua ujuzi, tajriba, maana na uhalisi

wa watafitiwa. Data zilichanganuliwa kwa kutathmini jinsi matukio yalivyotokea

pamoja na maingiliano ya vilongo na vionjo vya kijamii. Aidha, data za utafiti huu

zimewasilishwa kwa njia ya maelezo. Mbinu hii hutumika kuchanganua data bila ya

kutumia mahesabu (Kombo na Tromp, 2006). Katika hatua hii, mtafiti alifafanua na

kuchanganua maelezo ya msingi yaliyotolewa na watafitiwa kulingana na

yanavyohusiana na mada kwa kuzingatia mahitaji ya malengo ya utafiti. Mtafiti

Page 41: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

28

alizipanga data zake kulingana na malengo ya utafiti na kuzitolea maelezo. Data

ziliwasilishwa kwa njia ya maelezo ambayo yalihusiana na lengo mahususi husika na

kisha kutoka katika dondoo hilo ambapo maelezo ya kiuchambuzi yalitolewa. Kwa

kufanya hivyo, aliweza kukamilisha malengo ya utafiti kwa namna ambayo

inatakiwa.

3.8 Itikeli ya Utafiti

Utafiti huu uliendeshwa kwa mujibu wa maadili yaongozayo mchakato mzima wa

utafiti. Katika hatua hii, mtafiti alizingatia mambo muhimu kama vile kuomba ridhaa

kutoka katika mamlaka zinazohusika ili zimruhusu kukusanya data za kimaktaba

katika maeneo au taasisi zao; kuomba ridhaa ya watafitiwa ili wakubali kutafitiwa,

utunzaji wa siri za taarifa na uhifadhi wa majina ya watoa taarifa kadiri ya matakwa

ya watafitiwa. Itikeli ya utafiti ni dhana inayorejelea mazingatio ya haki ya mtafitiwa

na kuzuia madhara dhidi yake (Hays na Sigh, 2012).

Katika kuhakikisha itikeli ya utafiti inazingatiwa, kabla ya kuanza mchakato wa

kukusanya data, mtafiti aliomba kibali kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma na mamlaka

zinazohusika katika utafiti huu, pia kuomba idhini ya kufanya utafiti katika Chuo

Kikuu cha Dar es Salaam. Vilevile, mtafiti alijitambulisha kwa watafitiwa na

kuomba utayari wao ili kuweza kushirikiana nao katika mchakato wa ukusanyaji

data. Baada ya hapo, mtafiti alijenga mahusiano mazuri na watafitiwa uwandani

ikiwa ni pamoja na kuwaeleza lengo la utafiti huu kuwa ni la kitaaluma tu na si

vinginevyo. Pia, mtafiti aliomba ridhaa ya kurekodi na kupiga picha za mnato,

vielelezo vilivyokuwa na uhusiano na utafiti huu ili kusaidia katika kuhifadhi

kumbukumbu katika uchanganuzi wa data. Vilevile, mtafiti alitunza siri za

watafitiwa.

3.9 Uhalali na Uthabiti wa Matokeo ya Utafiti

Sanga (2018) anasema utafiti uliosanifiwa vizuri huweza kuyafikia malengo ya

utafiti kwa namna iliyo wazi na inayoeleweka, ubora wa utafiti hutokana na sifa ya

uhalali na uthabiti wake katika matokeo ya utafiti. Maxwell (1996) na Dey (2005)

wanafafanua kuwa uhalali wa matokeo katika mkabala wa kitaamuli huhusisha hali

ya kuaminika kwa maelezo, hitimisho, ufafanuzi, ufasili na aina yoyote ya maelezo

yaliyotolewa. Uhalali wa matokeo hudhihirika wakati mbinu, vifaa na njia za utafiti

Page 42: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

29

zinaleta matokeo yasiyo badilikabadilika katika muktadha au mazingira husika.

Uthabiti wa utafiti ni uhalisi wa matokeo ya utafiti na hupatikana ikiwa taarifa za

utafiti zitatokana na vyanzo sahihi vya tatizo la utafiti (Patton & Michael 2002).

Uhalali wa matokeo ya utafiti huu ulifikiwa kwa mtafiti kuweka bayana mipaka ya

utafiti kwa watafitiwa. Pia, mtafiti alitumia lugha nyepesi na ya moja kwa moja

katika kukusanya data ili sampuli isipate tabu kuelewa kinachotafitiwa. Vilevile,

mtafiti alitumia njia zaidi ya moja katika kukusanya data za utafiti. Hivyo,

utekelezaji huu, ulipelekea matokeo ya utafiti kuwa ni halali na thabiti.

3.10 Changamoto za Utafiti na Utatuzi Wake

Ijapokuwa kumekuwa na mafanikio katika utafiti huu, lakini mtafiti amekumbana na

changamoto mbalimbali katika ukusanyaji wa data za uwandani na maktabani.

Kwanza, ni mlipuko wa Ugonjwa wa Virusi vya Korona 2019 (UVIKO-19) na

kupelekea mtafiti kuchelewa kukusanya data kwa wakati aliopanga. Hii ilitokana na

kuwa, kwa muda wa miezi mitatu vyuo vilifungwa nchi nzima kutokana na ugonjwa

wa virusi vya korona. Changamoto hii ilitatuliwa kwa kuwatafuta watafitiwa

wachache waliopatikana na kuweza kukidhi malengo ya utafiti. Pili, kutofahamika

kwa urahisi kwa dhana ya utafiti huu kwa watafitiwa na kusababisha ugumu katika

upatikanaji wa data. Kutofahamika kwa mbinu ya utanzia kutokana na kutotafitiwa

vya kutosha na kufahamika kwa wataalamu wengi hasa katika utanzu wa ushairi.

Changamoto hii ilitatuliwa kwa mtafiti kuwaelewesha kuhusuiana na dhana ya

utanzia na utumikaji wake katika ushairi. Tatu, kutosomwa kwa kina kazi za ushairi.

Watafitiwa wengi walishindwa kukidhi malengo ya utafiti huu kwa kuwa

waliposoma diwani teule hawakusoma kwa kina zaidi, hivyo kushindwa kukidhi

malengo husika. Changamoto hii, ilitatuliwa kwa mtafiti kujikita kwenye mawazo ya

wataalumu wachache na kuyahusisha na yale yaliyopatikana kutoka kwenye matini

mbalumbali.

3.11 Muhtasari wa Sura ya Tatu

Katika sura hii tumevifafanua vipengele vya methodolojia ya utafiti. Vipengele hivyo

ni usanifu wa utafiti katika kipengele hicho tunapata mchakato mzima wa namna ya

ukusanyaji data na namna ya kuzichanganua data. Eneo la utafiti katika kipengele

hiki mtafiti anapaswa kuelezea eneo la kijografia ambapo anakwenda kufanyia utafiti

na kuelezea sababu ya kuchagua eneo hilo kwa kuzingatia vigezo vya upatikanaji wa

Page 43: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

30

watafitiwa na eneo la kupata nyaraka za kusoma. Walengwa wa utafiti, ukusanyaji

wa data, njia na zana za kukusanyia data na mchakato wa ukusanyaji wa data.

Vipengele vingine ni uchanganuzi wa data, itikeli za utafiti, uhalali na uthabiti wa

matokeo ya utafiti na changamoto za utafiti na utatuzi wake. Sura inayofuata

inawasilisha na kujadili matokeo ya utafiti.

Page 44: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

31

SURA YA NNE

UWASILISHAJI NA MJADALA WA MATOKEO YA UTAFITI

4.1 Utangulizi

Sura hii inawasilisha na kujadili matokeo ya utafiti uliohusu Mdhihiriko wa Utanzia

katika Ushairi wa Kiswahili: Mifano Kutoka Kichomi na Dhifa. Utafiti huu

ulifanyika kutokana na kuchunguza mdhihiriko wa utanzia katika diwani teule na

ulikusudiwa kutimiza malengo matatu mahususi kama ifuatavyo: kubainisha utanzia

katika diwani teule, kufafanua dhima za utanzia uliotumika katika diwani teule na

kufafanua athari za utanzia kwa wasomaji wa diwani teule. Ili kupata data

zilizohitajika, mtafiti alitumia mbinu zifuatazo kukusanya data ambazo ni usaili na

uchaganuzi matini. Data hizo zilichanganuliwa kwa kutumia mbinu ya maelezo na

mkabala wa kitaamuli, ambapo nadhari ya upokezi iliongoza ukusanyaji, uchambuzi

na ufasiri wa data. Hivyo, ili kuwasilisha mjadala wa matokeo ya utafiti, sura

imegawanyika katika sehemu tano. Sehemu ya kwanza imeelezea muhtasari wa

diwani teule za Kichomi na Dhifa. Sehemu ya pili inabainisha matukio ya utanzia

katika diwani teule ambalo ni lengo la kwanza la utafiti. Sehemu ya tatu inafafanua

kuhusu dhima za utanzia katika diwani teule ambalo ni lengo la pili la utafiti.

Sehemu ya nne inafafanua athari za utanzia kwa wasomaji ambalo ni lengo la tatu la

utafiti. Sehemu ya tano inatoa muhtasari wa sura ya nne.

4.2 Utanzia katika Ushairi wa Euphrase Kezilahabi

Sehemu hii inawasilisha mjadala wa matokeo ya utafiti kwa kulichambua lengo letu

la kwanza la utafiti wetu ambalo ni kubainisha matukio ya utanzia yaliyodhihirika

katika diwani teule. Sehemu hii itaundwa na vijisehemu vinne ambavyo ni muhtasari

wa diwani ya Kichomi, muhtasari wa diwani ya Dhifa na matukio ya utanzia katika

diwani teule.

4.2.1 Muhtasari wa Diwani Teule

Sehemu hii inatoa muhtasari wa diwani teule zilizotumika katika utafiti huu. Diwani

hizo ni Kichomi na Dhifa.

4.2.1.1 Muhtasari wa Diwani ya Kichomi

Diwani ya Kichomi imetungwa mnamo mwaka 1974 na kuchapishwa na Heinemann

Educational Books (E.A) L.t.d Nairobi, Kenya. Katika diwani hii kuna jumla ya

Page 45: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

32

mashairi arobaini na mbili (42) yaliyo katika sehemu mbili. Mashairi tisa ya mwanzo

yameandikwa kwa lugha ya Kiingereza na baadaye kutafsiriwa kwa lugha ya

Kiswahili, na sehemu ya pili yaliandikwa kwa lugha ya Kiswahili. Katika diwani ya

Kichomi kumejadiliwa mambo mbalimbali yanayoikumba jamii kwa njia ya ushairi.

Kichomi ndio diwani ya kwanza ya mwandishi Euphrase Kezilahabi ambayo imeleta

mapinduzi makubwa katika uga wa ushairi wa Kiswahili kwa kutunga bila kuzingatia

arudhi za vina na mizani. Mashairi katika diwani ya Kichomi si guni kwa kuwa

hayajafuata kanuni za kutunga mashairi za Amri Abedi. Euphrase Kezilahabi

ametunga mashairi yake kwa kufuata mtindo mpya wa kuandika mashairi ya

Kiswahili na kusaidia kukuza fasihi ya Kiswahili kwa kuiletea mtindo mpya wa

kutunga mashairi.

Topan (1973), katika dibaji ya diwani ya Kichomi, anasema:

Muundo alioutumia Kezilahabi haukufungika upande wa mistari: si

lazima kila ubeti wa shairi uwe na idadi maalumu ya mistari;

haikufungika upande wa vina; si lazima mistari yenyewe iwe na vina

haikufungika upande wa mizani: si kila mstari uwe na idadi sawa ya

mizani. Mashairi yale (yaani ya kimapokeo) yaimbwa, haya hayaimbwi

Maudhui yaliyomo katika mashairi ya Euphrase Kezilahabi ni mawazo ya kisasa,

aliyoandika kijana aliyezungukwa na mazingira ya kisasa, kielimu, kijamii na kidini.

Diwani ya Kichomi ilileta mapinduzi katika umbo, miundo na mitindo ya utunzi wa

ushairi kulikuwa na lengo la kupanua uhuru wa kisanaa na kirahisisha uelewa wa

ushairi kutokana na matumizi ya lugha ya kawaida. Mtindo mpya wa utunzi

unaotumia lugha ya watu wa kawaida ulijibu changamoto iliyotokana na

kutoeleweka kwa mashairi ya wanamapokeo ambayo yalitumia lugha ngumu ya

kimafumbo, methali na taswira ambazo hazikuwa rahisi kutafirika.

Diwani hii imeelezea mambo mbalimbali yanayoikabili jamii kwa ujumla. Mfano ni:

matabaka, uongozi mbaya, mgawanyo wa matabaka, ukombozi wa kifikra usaliti,

masuala ya dini, ndoa na mapenzi. Hivyo, kutokana na mawazo na fikra zilizoelezwa

katika diwani hii vimetumika ili kuonyesha mdhihiriko wa utanzia katika diwani ya

Kichomi.

Page 46: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

33

4.2.1.2 Muhtasari wa Diwani ya Dhifa

Hii ni diwani ya tatu kutungwa na Euphrase Kezilahabi mnamo mwaka 2005 na

kuchapishwa na Vide-Muwa Publishers Nairobi, Kenya. Diwani ya Dhifa imejikita

katika kuelezea masuala ya kisiasa na ujenzi wa jamii mpya. Katika diwani ya Dhifa

kuna mashairi hamsini na mawili (52) yaliyoandikwa kwa lugha ya Kiswahili. Dhifa

ina maana ya sherehe rasmi ya chakula iliyoandaliwa kwa watu maalumu, hasa

viongozi. Katika diwani hii mwandishi ameonesha namna viongozi wanavyoweza

kutumia rasilimali za nchi kwa matakwa yao binafsi na kuwasahau wananchi

waliowapa dhamana hiyo. Hali hiyo inawafanya wananchi kuwa katika hali duni ya

kimaisha na kupelekea kukosa huduma muhimu za kijamii kama vile elimu, haki ya

kisheria, huduma za afya na maji. Amefichua uchafu unaofanywa na viongozi

walioaminiwa na wananchi kwa ajili ya kuleta maendeleo. Mwandishi ametumia

sauti ya ukali ili kuibua hisia kwa wasomaji wake katika kutazama maisha ya jamii

kwa ujumla na kukemea uovu unafanywa na viongozi dhidi ya wananchi. Wamitila

(2008), katika utangulizi wa diwani hii, anasema kuwa dhamira zinazojadiliwa katika

diwani “zinawataka wasomaji wake wadadisi, wahoji, wachunguze na kujichokonoa

nafsi zao, mazingira yao, siasa yao, nchi yao, utambulisho wao, ulimwengu wao na

maisha yao wenyewe.”

4.2.2 Utanzia katika Diwani Teule

Kabla ya kuelezea matukio ya utanzia yaliyojitokeza katika diwani teule za Euphrase

Kezilahabi, tunaweza kuyagawa matukio ya utanzia kwa kuzingatia makundi matatu

ya utanzia. Mazongela (khj) anabainisha makundi matatu ya utanzia kama ifuatavyo:

utanzia wa kisaikolojia ambao unahusisha zaidi ufahamu na utendaji wa akili, hapa

tunapata matukio ya kifo na kifungo. Utanzia wa kimwili ni ule unaosababishwa na

magonjwa pamoja na maumivu ya mwili, hapa tunapata matukio kama; hali ngumu

ya maisha, magonjwa na mateso. Utanzia wa kimaumbile unahusisha upungufu wa

viungo katika mwili wa mwanadamu hapa tunapata matukio ya ulemavu wa viungo,

majanga, ukatili na ugumba au utasa. Utafiti umebaini kuwa katika diwani teule kuna

matukio mbalimbali yanayoonesha utanzia. Matukio hayo ni haya yafuatayo:

4.2.3 Hali Ngumu ya Maisha

Said (2016) anabainisha kuwa hali ngumu ya maisha inaweza kusawiriwa sana katika

kazi za kifasihi ijapokuwa uhalisia huo huambatana na ubunifu. Hivyo, tunaona hali

Page 47: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

34

ngumu ya maisha ni moja ya tukio la kitanzia. Kwa kawaida, mtu mwenye hali

ngumu ya maisha huandamwa na simanzi na masikitiko ya mara kwa mara. Hii

inatokana na ukweli kwamba mtu huyo hushindwa kuyamudu maisha yake kwa

kushindwa kujikimu kimaisha. Utafiti umebaini tukio hili la huzuni likijitokeza

katika mashairi ya Euphrase Kezilahabi. Mathalani, katika diwani ya Dhifa, kuna

shairi liitwalo “Kwa Walimu Wote” (uk. 1). Katika shairi hili, Euphrase Kezilahabi

ameonesha hali ngumu ya maisha inayomkabili mwalimu katika mazingira yake ya

kazi mpaka atakapostaafu. Kupitia shairi hili, tunaona utanzia ukijitokeza kwa namna

ya mwalimu alivyosawiriwa na kuchimuza utanzia. Mwandishi anasema:

Huu utakuwa wimbo wako

Utakapostaafu urudipo nyumbani

Umelewa kangara na nyayo zako

Zikishindwa kulenga njia nyembamba vijijini

Utakuwa kichekesho cha watoto

Watakaokuita, Ticha! popote upitapo

Kumbuka mwalimu utakapostaafu

Mijusi watataga mayai ndani ya viatu

Vyako vilivyokwisha visigino

Na ndani ya sidiria chakavu

Zilizoshikizwa kamba kwa pini

Mende watazaliana ndani ya chupa tupu

Za marashi na bia.

Mwandishi anaonesha hali ya maisha ya walimu na watumishi wengine wa serikali

yalivyo sasa na hatima yake baaada ya kustaafu. Walimu ambao ndio walezi wa taifa

wanaishi maisha duni na ya kusikitisha. Katika beti hizo tunaona hali ngumu ya

maisha ikisawiriwa kupitia maisha ya mwalimu atakapostaafu. Kwa hakika, shairi

hili linaibua hisia ya huzuni, machungu na masitikito makubwa kwa walimu, kwa

sababu mwalimu amekuwa kama kichekesho kwa jamii baada ya kustaafu. Hii

inatokana na maisha yao kuwa duni huku wakifanya kazi muhimu ya kufuta ujinga

kwa vijana wa taifa lao. Ujira wao ni mdogo ukilinganishwa na kazi kubwa na

muhimu wanayoifanya. Hali hii inaibua masikitiko makubwa anayoyapata mwalimu

kutokana na kupata ujira mdogo hata kushindwa kuweka akiba kwa ajili ya maisha

ya baadaye. Atwood (1982) anashadidia hoja kwa kusema kuwa, usomaji ni

mfanyiko unaombadilisha mtu. Hatuwezi kuwa wale wale tuliokuwa kabla na baada

ya kuisoma kazi fulani ya fasihi. Katika kazi hiyo kuna maarifa anayobakia nayo

Page 48: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

35

msomaji ambayo yanaweza kubadili maisha yake kwa kupata funzo juu ya hali

ngumu ya maisha na kupelekea kuondokana na hali ya huzuni, masikitiko, machungu

na hata simanzi zilizomkumba kutokana na utanzia.

Pia, katika diwani ya Kichomi mwandishi anaendelea kuelezea hali ngumu ya maisha

anayoyapitia mwanadamu katika maisha yake ya kila siku. Changamoto za kimaisha

zinazowakabili wanajamii husababisha hali ya huzuni na masikitiko ambayo

huchochea ugomvi au vifo kwa wanajamii. Haya yanadhihirika katika shairi la

“Nimechoka” (uk. 34) mwandishi anasema:

Mikono inaniuma na waya imekwishanikata vidole

Damu imetiririka hadi kwapani kujipanguza siwezi

Nimechoka. Kadiri niendeleavyo kuning’inia, ndivyo

Sura yangu ionyeshavyo vizuri alama za uchovu

Ninatazama huku na huko kuwatafuta wenye huruma

Lakini wanadamu wote wazima wanainamisha vichwa

Chini kama kwamba hawajui hata jamaa zangu!

Ninaendelea kuning’inia kama picha iliyotundikwa

Katika shamba la mawele, na mwenye shamba

Huvuta waya kutoka nyumbani, itingishike kuwatisha ndege

Machozi yananitoka, kuyapangusa siwezi

Ninajitahidi kutoa sauti kwa nguvu

Jamani e! Nisaidie Ng’oeni hivyo vitimbo!

Lakini wanadamu wameinama. Wanaanza sasa kusali.

Katika shairi hili mwandishi anaelezea falsafa ya maisha na kuonesha kuwa maisha

ni adhabu na tanzia anayokumbana nayo mtu, kwani maisha yanaonesha upweke

mkubwa aliona mwanadamu. Hali hiyo ya upweke inampelekea mwanadamu kukata

tamaa ya kuendelea kuishi. Beti hizi zinadhihirisha hali ngumu ya maisha

anayoyapitia mwanadamu kutokana na mfumo wa maisha ya jamii yake. Katika

shairi hili, tunaona maumivu, uchungu na huzuni aliyonayo mtu ambaye yupo katika

hali ngumu ya maisha anayehitaji msaada kwa ndugu na marafiki lakini anaona

hakuna msaada wowote. Kutokana na maumivu anayoyapitia, anaona ni bora

apumzike kwa sababu amechoka kupambana na misukosuko katika maisha.

Changamoto anazozipitia zinamfanya aone kuwa yupo peke yake lakini ni wazi

kuwa changamoto hizo, zinazoikabili jamii kwa ujumla na kuona kuwa zitamalizwa

kwa kumwomba mwenyezi Mungu.

Page 49: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

36

4.2.4 Ulemavu wa Viungo

Ali (2015) anasema kuwa, ulemavu ni sehemu ya mwili yenye kuonesha kasoro

fulani katika maumbile ya kiumbe hai. Kutokana na maelezo hayo tunaona kuwa,

ulemavu wa viungo ni hali ya mwanadamu kuwa na dosari katika viungo vyake.

Ulemavu upo wa aina mbalimbali kama vile: ulemavu wa ngozi, ulemavu wa macho

(upofu), ububu, ulemavu wa miguu na ulemavu wa mikono. Aina zote hizi za

ulemavu huibua hali ya majonzi na huzuni kwa wahusika na hata jamii

inayowazunguka kwa jumla. Mwandishi Eupharase Kezilahabi ameionesha hali hii

katika shairi lake liitwalo “Ukucha wa Mbwa” (uk.25) ndani ya diwani ya Kichomi.

Shairi hili la kihadithi linasimulia kuhusu kisa cha mama aliyekuwa kipofu na

matatizo yaliyomkumba. Katika ubeti wa kwanza, mshairi anatudokeza hali ya upofu

wa mama huyo kwa kusema:

Palikuwa na mama mmoja

Mama mjane kipofu na masikini

Aliishi shamba karibu na kilima

Haoni mvua haoni chakula

Akawa masikini wa kijiji

Majirani kumsaidia.

Akitembea fimbo yake

Yenye vijikengele hulia

Umasikini na kuomba msaada

Watoto humkimbilia fimbo

Kuchukua na kumwongoza

Miji mbali mbali kuongea.

Katika shairi hili mwandishi anazungumzia changamoto zinazowapata watu wenye

tatizo la ulemavu kutokana na madhila wanayofanyiwa katika jamii, maradhi pamoja

na umasikini. Nukuu hii inaonesha hali ya mama mwenye upofu inayomfanya

atembee kwa tabu. Alikuwa anatumia fimbo anapotembea (ubeti wa 3). Kutokana na

hali yake ya ulemavu wa macho, mama huyu alijikuta akitendewa maovu kama vile:

kubakwa na kunajisiwa (ubeti 4). Hali hii inamfanya mtu awe katika hali ya

masononeko na masitiko makubwa yanayopelekea kuwa na huzuni. Kutokana na

kushindwa kufanya vitu vyake mwenyewe kwa sababu ya ulemavu ulipelekea kuishi

maisha ya shida yenye machungu na masikitiko yaliyosababishwa na vitendo

alivyofanyiwa na baadhi ya wanajamii.

Page 50: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

37

4.2.5 Kifungo

TUKI (1981) wanaeleza kifungo ni adhabu ya mtu kuwekwa mahabusu au rumande

au katika kizuizi. Kifungo pia huleta utanzia kwa wafungwa. Mtu anapofungwa

huwa anakosa uhuru wa kujiamulia na kutenda matendo yake kama ilivyo kawaida.

Kipengele hiki cha kifungo nacho kinajitokeza kama tukio linaloonyesha mbinu ya

utanzia. Maisha ya kufungwa gerezani yanazua huzuni na majonzi kwa mfungwa na

watu waliyokaribu yake. Mwandishi Euphrase Kezilahabi ameonesha hali ya kifungo

katika shairi lake la “Fungueni Mlango” katika diwani ya Kichomi (uk.23).

Mwandishi anasema:

Hewa kuikosa

Na jasho kunitoka ndani ya chumba

Kwa upweke

Ninajiona nimefungiwa

Sioni madirisha lakini

Mlango wa karatasi uko mbele yangu

Ninaugonga kwa mkono

Kichwa na mabega

Mlango unatoa mlio kilio

Lakini mwanadamu hatanifungulia

Damu

Damu puani, damu mdomoni

Damu kichwani itumikayo kama wino

Mikono, kichwa, mabega uchovu

Kwa kichwa kama cha mbuni

Mchangani, tena ninaugonga

Lakini mwanadamu hatanifungulia

Ninaona kizunguzungu

Ninapiga kelele kama

Ng’ombe machinjioni

Fungueni mlango

Mlango fungueni

Lakini mwanadamu hatanifungulia

Katika shairi hili, mwandishi anaelezea hali inayompata mhusika ambaye yupo

katika hali ya kutoeleweka, upweke na kifungo, huku akiomba msaada lakini hakuna

anayemsaidia. Kupitia beti hizi, tunaona jinsi majonzi na masikitiko yakijengwa

kupitia kifungo. Shairi linaelezea kilio cha mtu aliyefungwa na kusababishwa akose

hewa na jasho kumtiririka kwa sababu amewekwa kwenye chumba chenye dirisha

moja dogo linaloingiza hewa kidogo. Mtu huyu ingawa anaomba msaada wa

kufunguliwa mlango ili atoke ndani lakini hakuna anayemsaidia. Tunasoma shairi

hili tunaona hisia za kitanzia zikiibuliwa kutokana na tukio hilo la kifungo. Kwa

Page 51: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

38

sababu ya kukosa uhuru anaoutaka mwanadamu kutokana na kifungo kunampelekea

kuwa na masikitiko, majonzi na simanzi kubwa.

4.2.6 Maradhi

Maradhi ni ile hali inayosababisha mtu kuwa katika hali ambayo hushindwa kufanya

kazi au kuishi katika hali asiyoizoea na kupungukiwa nguvu za utendaji wa kazi za

kila siku. TUKI (2013) wanasema maradhi ni kitu kinachosababisha mtu, mmea, au

mnyama kuwa katika afya mbaya. Maradhi hayo yanapelekea mtu au watu kuwa na

hali ya kuingiwa na huzuni kubwa kutokana na kukosa raha na furaha kwa sababu ya

kusumbuliwa na maradhi. Hali hii inapelekea hata ndugu kushindwa kuwahudumia

wagonjwa kutokana na maradhi yanayowasumbua. Hivyo, hufikia hatua kwa

mgonjwa kutengwa na jamii yake na kukosa mtu au watu wa kumfariji. Hapa

inapelekea kuwa na simanzi, huzuni na masitikiko makubwa, kama alivyodhihirisha

na mwandishi Euphrase Kezilahabi katika diwani ya Kichomi katika shairi la

“Ukucha wa Mbwa” (uk. 28-29) mwandishi anasema:

Kidonda kikawa kidonda

Maumivu yakawa maumivu

Siku tatu kupita

Naye kama mbwa akajifia

Wanawake kutaka mali

Uchumi wakamzika

Watoto, wanawake, wapishi

Wote wakachomwa na ukucha

Nao wasiuvumbue

Wakafa wameashama kwa kulia

Mali ya bure kuacha

Wakazikwa shimo moja kama taka

Kupitia shairi hili mwandishi anaelezea hali ya umasikini na maradhi yanayoleta

madhara makubwa katika jamii kama vile kifo. Katika ubeti huu tunaona namna

mwandishi alivyoonesha maradhi yanavyotesa na kumsumbua mtu mpaka kupelekea

kifo chake. Maradhi hayo yanaacha mafarakano makubwa baina ya wale wanaobakia

hasa kutokana na kuondokewa na ndugu yao waliyompenda. Hali ya kusumbuliwa

na magonjwa mbalimbali kunapelekea mtu kuwa katika majonzi, machungu na

wakati mwingine kukata tamaa ya kuishi kutokana na kuchoka kuvumilia maumivu

makali anayoyapitia.

Page 52: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

39

Vilevile, katika diwani ya Dhifa mwandishi ameweza kuonesha namna maradhi au

magonjwa yanavyofupisha maisha ya wanajamii. Katika shairi la “Wazo Nje ya

Wakati” (uk. 23) anasema:

Umezoea watoto kuwavizia

Au wazee wanojikongoja

Uonapo mwenye kansa

Wanyatia kummalizia

Na kisha wajitapa

Uonapo watu wanalia.

Wachukia penye dawa

Waambaa penye chakula bora

Wasubiri kosa la dereva

Na magari yagonganapo

Wanong’oneza waloku

Wamekufa!

Hapa mwandishi anatoa mtazamo wake juu ya maradhi yanayowakumba watoto na

wazee ambao wapo kwenye hatari kubwa ya kupoteza maisha yao kutoka na

magonjwa mbalimbali. Ijapokuwa watu wanatumia dawa kupunguza makali ya

maumivu lakini wanakuwa katika huzuni, uchungu na masitiko makubwa kwa

sababu maradhi yanaingia kwa haraka lakini huchukua muda kutoka. Kushindwa

kupata lishe bora kutokana na hali ngumu ya maisha husababisha wagonjwa kukata

tamaa ya kupona. Hivyo, kuwa katika hali ya masikitiko na simanzi zinazopelekea

kukosa matumaini ya kuendelea kuishi mwisho wake huwa ni kifo.

4.2.7 Ukatili

Ni hali ya kuleta hofu, kitisho kwa mtu au mnyama kwa lengo la kumkandamiza kwa

maslahi ya mtu binafsi au kikundi fulani cha watu. UWAKI (2013) wanasema,

ukatili ni matumizi ya nguvu yanayompa mtu fursa ya kumtumia au kumkandamiza

mtu mwingine, ikiwamo kumsababishia kifo, woga au hofu, madhara ya mwili,

kifikra na kisaikolojia. Baadhi ya wafuasi wa nadharia ya upokezi wanaamini kuwa

kazi ya sanaa humwaathiri msomaji, msomaji hurushwa katika ulimwengu mpya na

mgeni na kukengeushwa katika maisha yake. Zaidi ya hayo, msomaji hufinyangwa

upya na akachukuana ipasavyo na matini anayoipitia. Ukatili unaweza kuwa na

madhara makubwa sana katika jamii kwa sababu huweza kumuathiri mtu kiakili,

kimwili hata kihisia kutokana na matendo aliyofanyiwa. Athari ambazo anaweza

kuzipata mtu aliyefanyiwa ukatili ni kama kukosa furaha, kuwa na masikitiko na

Page 53: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

40

jitimai. Hali hii ya ukatili inaweza ikapelekea kifo na hata mtu kukata tamaa ya

kuishi kabisa. Vitendo vya ukatili vinaweza kuanzia katika ngazi ya familia hadi

katika jamii kwa ujumla. Ukatili unaweza kudhihirika katika makundi mbalimbali:

ukatili katika mapenzi, mauaji, ubakaji, uhalifu, dhuluma na ukatili wa kijinsia.

Endapo mtu atafanyiwa ukatili anapata madhara ya kudumu kwa sababu anakuwa

ameathirika kisaikolojia, hivyo, kupelekea hata kushindwa kumuamini mtu kutokana

na athari alizozipata baada ya kufanyiwa ukatili.

Katika diwani ya Kichomi, mwandishi Euphrase Kezilahabi amedhihirisha hali ya

ukatili katika mapenzi kama inavyooneshwa katika shairi la “Hutonihadaa” (uk.21)

mwandishi anasema:

Barua ameandika anasema hampendi tena

Naye kitandani anaisoma akicheka

Maringo ya bure nimemuweza mjinga

Jina lake nimeharibu hana la kujivunia

Kesho yake njiani kwa raha anatembea

Mara nyuma chapuchapu hatua anasikia.

Nani huyo anyatiaye nyuma yangu?

Sauti inasema ni mimi

Unafuata nini nami yote nimeona?

Barua umepata na yote umesoma

Sauti inasema lazima nikuage

Nimesema sikupendi tena yote nimeona

Sauti inasema mpenzi njoo tuagane.

Katika shairi hili, mwandishi anaelezea mapenzi yaliyochujuka baina ya watu wawili

waliokuwa wanapendana. Anatunaonesha namna wapenzi wawili waliokuwa na

mahusiano walivyoachana na mmoja wao kubaki na majonzi makubwa baada ya

kufanyiwa ukatili wa kimapenzi. Mapenzi hayo yaliyochujuka yalisababisha

mgogoro mkubwa baina ya wapenzi hao na kupelekea kuachana ijapokuwa mmoja

kati yao hakuridhika na maamuzi hayo. Hali hiyo ilipelekea simanzi, machungu na

majonzi makubwa kwa yule aliyeachwa na kuingiwa na woga wa kuona hatoweza

kuishi mwenyewe. Hapa, mwandishi ameonyesha hali halisi ya namna mtu

alivyofanyiwa ukatili katika mapenzi na kuachwa bila ya kuelewa hatima yake.

Ukatili huwa unaweza kusababisha madhara kama vile kuchanganyikiwa, kukosa

furaha, kukata tamaa ya kupenda tena na kuchukia mahusiano ya kimapenzi hasa

kwa yule aliachwa kutokana na mazoea aliyokuwa nayo katika mahusiano yake.

Page 54: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

41

Vilevile, katika shairi la “Hadija” (uk.22) hali hii ya ukatili katika mapenzi

imedhihirika. Mwandishi anasema:

Hadija

Umekata mti mtima

Umeanguka nyumba yako

Uziba mto hasira

Nyumba yako sasa mafurikoni

Na utahama

Watoto kuwakimbia.

Hapa mwandishi anaonesha mwanamke aliyemuua mumewe kwa kumpa sumu ili

apate uhuru. Hii ilitokana na mapenzi aliyokuwa nayo mume kwa mkewe. Baada ya

kufariki mume, mke anapata uhuru ila anaingiwa na simanzi kubwa mpaka anafikia

hatua ya kukata tamaa ya maisha kutokana na ukatili alioufanya. Nukuu hii

inadhihirisha hali ya ukatili alioufanya mwanamke dhidi ya mwanaume bila kujali

kilichotokea. Ukatili alioufanya dhidi ya familia yake umeibua hali ya majonzi,

simanzi na machungu makubwa kwa watoto kukosa watu wa kuwafariji na kukosa

baba, mlezi na hata mshauri katika makuzi yao. Kwa sababu mama sio mfano wa

kuigwa tena kutokana na ukatili alioufanya dhidi ya baba yao.

Katika diwani ya Dhifa mwandishi anaendelea kuonesha ukatili wa kijinsia

wanaofanyiwa baadhi ya watoto wa kike katika jamii. Kwenye shairi la “Hoja”

(uk.59) mwandishi anasema:

Lakini

Ninakumbuka habari nilizosoma

Nikiwa ndani ya daladala

Jana jioni kijana mmoja

Jinale limehifadhiwa

Alimbaka msichana

Wa miaka kumi na sita

Dhuluma ya ubabe huweza kuharibu

Haiba hulka ya utu kwa muda mfupi

Na adhabu, laini

Ni hoja

Ni bado asubuhi.

Katika shairi hili, mwandishi anaelezea falsafa kuhusu maisha. Anadhihirisha ya

kwamba unyanyasaji umekithiri katika jamii. Anaonesha namna watu wasivyojali

hisia za wanyonge. Ubeti huu unaonesha maumivu anayoyapata mtoto wa kike

ambaye amefanyiwa ukatili wa kijinsia ambao unaleta madhara ya kudumu katika

maisha yake. Mawazo ya nadharia ya upokezi yanaumana na mbinu ya utanzia kwa

Page 55: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

42

sababu msomaji ufinyangwa na kubadilishwa fikra kutokana na matini anayoipitia.

Hivyo, kubadilika kifkira baada ya kuisoma kazi fulani ya kifasihi. Kutokana na

maumivu, uchungu na misukosuko aliyoipitia anakosa furaha katika maisha yake,

kwa sababu ya kitendo cha kikatili aliyofanyiwa na jamii kushindwa kumsaidia.

Ukatili huo unaweza kumsababishia kukata tamaa ya kuwa na mahusiano, kuathirika

kisaikolojia, kuwa na ukatili kwa wengine na kushindwa kuanziasha familia

kutokana na athari za kitendo alichofanyiwa

4.2.8 Majanga

Mazongela (khj) anafafanua kuwa, majanga ni matukio makubwa yanayoleta hasara

kwa jamii husika. Matukio hayo ni kama vile, mafuriko, tetemeko la ardhi na

vimbunga. Majanga hupelekea jamii kuingiwa na huzuni, hofu na masikitiko

yanayoleta watu kushindwa kupambana na kuleta maendeleo katika jamii. Hivyo,

mwandishi Euphrase Kezilahabi ameweza kuitumia kalamu yake katika kuonesha

hali halisi inayojitokeza katika jamii kutokana na majanga yanayoikabili jamii

husika. Katika diwani ya Dhifa kuna shairi la “Mafuriko Msumbiji 2000”

linalosema:

Nimekuja kugonga

Lango lenu la wakati

Kwa nyundo ya huruma

Amkeni! Enyi Wahenga!

Kwani huko Msumbiji

Mafuriko ya damu

Ya miaka iliyopita

Mafuriko ya mvua ya sasa

Yamekokota wanenu

Na mifupa yenu sasa

Tupu yaelea

Matundu ya macho yakitazama

Ukanda wa fedha upeoni

Mwa maji mengi.

Wanenu waponea

Vikombe vya machozi

Yaliyochotwa kutoka visiwa

Vya uoni wa ndugu wazamao.

Nge wenye mikia isokunjika

Na pembe zizungukazo, waruka

Lakini washindwa kung’ata

Na kuua vyanzo vya umaskini

Sikilizeni mgong’oto wa mshairi

Bubu asemaje na kuomba kwa moyowe.

Page 56: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

43

Katika shairi hili mwandishi amedhihirisha namna majanga yanavyoathiri jamii kwa

kiasi kikubwa na kuleta athari ambazo zimedumu kwa kipindi kirefu katika jamii.

Hali hii inarudisha nyuma maendeleo ya jamii kutokana na madhara ya majanga

yaliyotokea. Mawazo ya nadharia yanaumana na mbinu ya utanzia kwa sababu

umchochea msomaji kujitafutia na kujigundulia mengi kwa kufumbua ujumbe

uliomo katika kazi inayosomwa. Majanga kama ya kimbunga, mafuriko na tetemeko

la ardhi yamekuwa tishio kwa ulimwengu mzima kwa sababu yameweza kuacha

watu bila makazi ya kudumu, yamepelekea vifo na kurudisha nyuma maendeleo kwa

ujumla.

Mwandishi Euphrase Kezilahabi anaendelea kudhihirisha kuwa maisha ya

mwanadamu yamegubikwa na majanga ambayo yanaleta madhara makubwa. Katika

diwani ya Kichomi katika shairi la “Mto Nili” (uk.7) mwandishi anasema:

Ninawaona wakimwagilia mashamba yao kwa damu

Ile damu ya watu waliozama zamani ziwani

Kwa sababu ya pepo za Julai

Ziwa, mto, bahari-maisha.

Mwandishi anaelezea madhila yaliyofanywa na ukoloni dhidi ya Afrika na

kusababisha madhara mbalimbali yaliyoacha kumbukumbu kubwa kwa wananchi.

Katika ubeti huo mwandishi anaonesha namna watu walivyopoteza maisha yao

kutokana na pepo zivumazo wakati wa kipupwe mwezi Juni na Julai kila mwaka.

Pepo hizo zilisababisha vyombo vya kusafiria majini kukosa uelekeo na kupelekea

watu kupoteza maisha. Madhara hayo yaliwakumba wanaotumia vyombo vya usafiri

kuvuka ziwani, mtoni na hata baharini. Kutokana na vifo vya watu waliopoteza

maisha yao katika maji imepelekea mwandishi kuona ni wazi maji yamejaa damu za

watu waliofariki kutokana na wingi wao. Kwa mfano, ajali ya meli ya Mv. Bukoba

ilipozama katika ziwa Victoria na kupoteza maisha ya watu wengi. Ajali hiyo

imekuwa ikikumbukwa kila mwaka katika nchi ya Tanzania kwa tarehe iliyotokea.

Hivyo, kufanyika maombolezo ya kuwakumbuka waliopoteza maisha yao kutokana

na ajali. Hali hiyo upelekea uwezekano kwa jamii kupatwa na hali ya utanzia kwa

kuingiwa na huzuni, majonzi pamoja masikitiko kwa sababu ya kuwapoteza

wapendwa wao.

Page 57: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

44

4.2.9 Kifo

Mazongela (2016) anafafanua kuwa kifo ni tukio ambalo mtu au mnyama kukosa

uhai, umauti unaosababishwa na mambo mbalimbali. Pia, Ali (2015) anasema kifo ni

tukio la kufa au mwisho wa uhai. Anaendelea kusema kuwa athari za kifo hicho

huwaweka jamaa wa karibu kuwa na jitimai na huzuni kubwa kwa kuondokewa na

yule wanayempenda. Kifo kinaweza kutokea kutokana na maradhi au ghafla bila ya

kujali umri, pesa, madaraka wala uwezo wa watu. Hali ya kumpoteza mtu au watu

tunaowapenda kunapelekea huzuni na simanzi kwa wale wanaobaki na kusababisha

majonzi makubwa. Hivyo basi, tukio la kifo linaonyesha utanzia kwa wanajamii kwa

ujumla kutokana na kumkosa au kuwakosa wapendwa wao waliowapoteza. Matukio

ya vifo yamedhihirika kupitia mashairi mbalimbali ya mwandishi Euphrase

Kezilahabi katika diwani yake ya Kichomi kwenye shairi la “Kumbukumbu 1” (uk.

39). Mwandishi anasema:

Katika ushairi licha ya hekima kumwanga

Ulitafuta kiaminifu ukweli wa maisha

Kwa picha na maneno yenye mizani kilio,

Na ukatuonyesha utamu wa titi la mama.

Vizuu vianja vilivyokuja kwa bu vikifikiri

Sisi waama tusoweza kuelewana kichini

Havikutambua kilichokuwa nguoni mwao.

Kwa hiyo basi Shaaban, nitakuzika kaburi

Moja na Muyaka na juu ya lenu kaburi

Nitaandika “Malenga wa Kiswahili.”

Shairi hili linaelezea harakati za ujenzi wa jamii mpya ambao ulianzishwa na waasisi

wa ushairi wa Kiswahili, Shaaban Robert na Muyaka bin Haji, waliokuwa washairi

wa mwanzo. Mwandishi anatoa rai ya kuyaenzi yale waliyoyafanya kwenye taifa letu

huku akionesha huzuni aliyonayo baada ya kuwapoteza. Ubeti huu umedhihirisha

uwezekano wa hadhira kutokewa au kupatwa na hali ya utanzia kwa sababu ya

kuwapoteza washairi nguli Shaaban Robert na Muyaka bin Haji. Kutokana na

ubunifu wao katika kazi mbalimbali za fasihi kumeweza kusaidia waandishi wengi

kuchipukia kupitia kazi zao. Majonzi na simanzi yaliikumba jamii kutokana na

kuondokewa na waandishi nguli ambao walikuwa na mchango mkubwa katika fasihi

ya Kiswahili.

Pia, katika shairi la “Kumbukumbu 2” (uk.40-41) anaendelea kuelezea jambo hilo la

kifo kwa kumpoteza tena mshairi Mathias Mnyampala. Mwandishi anasema:

Page 58: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

45

Na basi nitakupa? Kitu gani wataka kutoka

Kwangu? Machozi yangu hayana gharama:

Yanatoka hata kwa moshi. Inafaa tuonane

Nikuvike taji la ucheshi halafu nikutume

Kwa hiyo basi, nitamtuma maiti anayesema akuite,

Nami, kwa nguvu za uchawi wa kishairi

Nitakufufua ukae juu ya kaburi lako

Tuzungumze macho kwa macho

“Habari gani Mnyampala? Mbukwa! Mimi

Ni K. bin T. Unayafurahishiaje maisha baada ya

Kufa. Wanasemaje malenga wetu. Mwambie Robati

Na kwamba siku hizi Waafrika wenyewe

Wameanza kupalilia bustani yake. Mwambie

Kaluta kwamba ule mzozo sasa unajulikana

Na kwamba watu wengi siku hizi hutunga mashairi.

Katika shairi hili, mwandishi anaelezea harakati za ujenzi wa jamii mpya na kutoa

wasifu wa waandishi nguli walioaga dunia vipindi vya nyuma na kutambua mchango

wao katika fasihi ya Kiswahili. Hapa mwandishi ameonesha huzuni na masononeko

yake makubwa ya kuwapoteza watunzi wakongwe wa kipindi cha nyuma ambao ni

Shaaban Robert, Mathias Mnyampala, Kaluta Amri Abeid pamoja na Muyaka bin

Haji. Hawa walikuwa mashujaa na wenye mchango mkubwa sana katika ushairi wa

Kiswahili. Kutokana na hali ya kuwapoteza waandishi hao, mwandishi ameingiwa na

huzuni, simanzi na masikitiko makubwa yaliyopelekea utanzia katika kipindi kirefu

mpaka kuandika ushairi ili kuwaenzi daima.

Hata katika diwani ya Dhifa suala la kifo limeweza kuonekana kupitia shairi la

“Wazo Nje ya Wakati” (uk.23). Mwandishi anasema:

Wasubiri hitilafu za mitambo

Ndege ziangukapo na kuungua

Keshoye magazetini watangaza

Wavizia walio usingizini

Na wanawake wanaojifungua

Huwezi kujiwindia

Mbu aumapo mtu

Pembeni wazengeazengea

Usikiapo vita moyoni wafurahia

Radi ipigapo nyuma wanguruma

Kujitangazia ushindi

Mieleka hatujaianza.

Ubeti huu unaonyesha namna maisha ya mwanadamu yalivyozungukwa na umauti

na kifo. Hapa mwandishi anaonyesha hofu na mashaka aliyonayo mwanadamu, hasa

Page 59: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

46

anapokuwa katika vyombo vya usafiri juu ya usalama wa maisha yake. Kifo

kimekuwa sababu ya kumfanya mwanadamu kukosa furaha kwa sababu hajui siku

wala saa. Hivyo kupelekea kuwa na huzuni, masikitiko, masononeko na simanzi

zinazopelekea utanzia.

4.2.10 Mateso

TUKI (2004) wanafasili mateso kuwa ni mambo yanayompa taabu mtu, uonevu,

madhila. Hivyo, mateso ni ile hali ya mtu kuwa katika maumivu ya mwili au akili

yanayosababishwa na mtu mwingine kwa kukusudia au bila ya kukusudia. Mateso

yanatokana na shida mbalimbali anazoweza kuzipitia mtu katika maisha yake

ambazo zinaweza kumsababishia maumivu ya kudumu. Hivyo basi, mateso

hupelekea mtu kukosa furaha, kuwa katika hali ya masikitiko, majonzi ya mwili au

akili na hata kufikia hatua ya kukata tamaa ya kuendelea kuishi. Katika diwani ya

Kichomi mwandishi Euphrase Kezilahabi amedhihirisha hilo katika shairi lake la

“Kuchambua Mchele” (uk. 63). Anasema:

Tukaanza kutoa chenga, moja moja

Vidole vikafanya kazi kama cherehani

Usiku na mchana macho yakauma

Tufanya kichuguu kidogo cheupe

Chenga na mchanga vikawa vingi sana

Tukapika baada ya muda mrefu wa kazi

Tukaanza kula,

Tukakuta bado mchanga na chenga!

Lini tutaula bila mchanga, bila chenga?

Katika shairi hili mwandishi anazungumzia harakati za ujenzi wa wa jamii mpya ya

Tanzania kipindi cha Azimio la Arusha. Hapa tunaziona juhudi za wananchi katika

kujenga ujamaa na kuondoa unyonyaji. Mwandishi anaonesha mchele kama mfumo

wa ujamaa unaoleta usawa katika jamii kati ya mtu na mtu ila chenga ni vikwazo

vilivyojitokeza katika harakati za kujikomboa zilizowakuta wananchi wa Tanzania.

Vikwazo hivyo vilipelekea hali ya masikitiko iliyowakumba wananchi wa Tanzania

katika kipindi cha Azimio la Arusha. Kutokana na hali ngumu ya maisha, watu

waliokuwa wakipitia ya kula mchele wa chenga wenye mchanga kwa muda mrefu

badala ya kula mchele ambao hauna mchanga. Baada ya kujenga Azimio la Arusha,

walijua kutakuwa na mabadiliko katika maisha yao kutokana na ujamaa lakini

waliendelea kupata mateso yaleyale mpaka waliamua kukata tamaa. Hapa mwandishi

Page 60: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

47

amefananisha maisha duni kama chenga za mchele ambazo hazipaswi kuliwa na

mwanadamu.

Pia, katika shairi la “Fungueni Mlango” (uk.23) mwandishi ameelezea hali ya mateso

anayoyapitia mtu au watu katika jamii. Anasema:

Hewa kunikosa

Na jasho kunitoka ndani ya chumba

Kwa upweke

Ninajiona nimefungiwa.

Sioni madirisha lakini

Mlango wa karatasi uko mbele yangu

Ninaugonga kwa mkono

Kichwa na mabega

Mlango unatoa mlio kilio.

Lakini mwanadamu hatanifungulia.

Damu

Damu puani, damu mdomoni.

Katika shairi hili mwandishi anazungumzia mateso anayoyapitia mhusika kutokana

na kifungo kinachomkabili (hali ya kuwa kizuizini). Ubeti huu unaonyesha mhusika

yupo katika hali ya kutoelewa hatima ya maisha yake, upweke na kifungo; anaanza

kupiga kelele za kufunguliwa mlango uliofungwa katika maisha yake. Hali hiyo

inadhihirisha kuwa yuko katika misukosuko, machungu na majonzi ambapo

inaonyesha namna mioyo ya watu inavyotoka damu kutokana na mateso

waliyoyapitia na kukosa uhuru. Kutokana na mateso anayoyapitia mwanadamu kuna

wakati anakosa kabisa tumaini la kuendelea kuishi kwa sababu ya maumivu na

huzuni inayoibua utanzia katika maisha yake.

4.3 Dhima za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule

Utafiti umebaini kuwa matumizi ya mbinu ya utanzia huwa na dhima mbalimbali.

Dhima hizo ni kama ifuatavyo: kujenga hisia za woga kwa hadhira, kufikisha ujumbe

kwa jamii, kujenga uhalisi wa maisha, kuibusha majonzi kwa hadhira, upekee wa

mtunzi na nyenzo ya kuhuzunisha hadhira. Sehemu hii inazifafanua dhima hizo.

4.3.1 Kujenga Hisia za Woga kwa Hadhira

Utanzia, kama mojawapo ya mbinu ya kibunilizi, imekuwa ikitumiwa na waandishi

wa kazi za fasihi kwa lengo la kujenga hisia za woga kwa wasomaji wao. Hii ni

kutokana na sehemu kubwa ya utanzia kutawaliwa na visa na mikasa yenye kuleta

Page 61: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

48

hisia za huzuni. Katika visa au mikasa hiyo, aghalabu huwa na matukio yenye

kuogopesha kama vile ukatili anaofanyiwa mhusika kutokana na mfumo wa maisha

anamoishi, mateso anayoyapitia mhusika na namna anavyojikomboa na majanga

yanayoikumba jamii. Fish (1980) anadai kuwa, msomaji au mhakiki wa kazi ya

sanaa hawezi kutengwa na mawazo ya shairi analolisoma. Hii ni kwa sababu kazi ya

fasihi inaweza kumuathiri msomaji au mhakiki hata akiwemo katika harakati za

kuifafanua na kuifahamu kazi hiyo. Katika kazi ya fasihi maudhui ambayo

mwandishi anayajenga kupitia maandishi yake yanapelekea uwezekano wa hadhira

kupatwa au kuingiwa na hisia za woga. Mfano, tukirejelea shairi la “Mto Nili” (uk.7)

katika diwani ya Kichomi tunaziona hisia hizi za woga zikiibushwa kupitia huzuni

inayopatikana katika shairi. Katika ubeti wa pili, mwandishi anasema:

Ninawaona wakimwagilia mashamba yao kwa damu

Ile damu ya watu waliozama zamani ziwani

Kwa sababu ya pepo za Julai

Ziwa, mto, bahari- maisha.

Maelfu walifanywa watumwa na maelfu

Waliuawa kwa sababu zisijulikana

Halikuwa kosa lenu. Damu yetu

Iliwalewesha mlipotenda hivyo.

Shairi hili linaonesha madhara yaliyoikumba jamii kutokana na majira ya mwaka

pamoja na athari za utumwa katika bara la Afrika. Beti hizi zinasawiri tukio la

kuzama kwa watu katika maji. Hili ni tukio la kitanzia ambalo kwa hali ya kawaida

msomaji anapata kusisimka mwili na akili yake pamoja na kuingia woga kutokana na

mashamba kumwagiliwa kwa damu. Kutokana na kuwa kwa hali ya kawaida sio

rahisi kwa mashamba kumwagiliwa damu badala ya maji. Hali hii inaleta masikitiko

na majonzi zaidi kwa msomaji wa kazi ya fasihi kwa kupata picha halisi ya ziwa

lilojaa maji yenye damu.

4.3.2 Kufikirisha Hadhira

Kwa kiasi kikubwa, mbinu ya utanzia hufikirisha hadhira kutokana na matukio yake.

Matukio yanayoibua utanzia kama vile mateso, majanga, vifo, ugumba au utasa, hali

ngumu ya maisha na ukatili huwa yana kawaida ya kuifikirisha akili. Mtu anawaza

mara kwa mara kutokana na tukio lililomkumbuka ambalo lina utanzia ndani yake.

Mawazo ya nadharia yanaumana na mbinu ya utanzia kwa kuwa wanadharia wa

upokezi wanaamini kuwa, kazi ya fasihi ina mapengo mengi msomaji analazimika

Page 62: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

49

kuyajaliza mapengo hayo. Kutokana na kuyajaliza, msomaji hushurutishwa kutunga

matini mpya ambazo zimechochewa kuzalika kutokana na matini asili. Hivyo,

mwandishi wa kazi ya fasihi, kama vile, Euphrase Kezilahabi hutumia mbinu ya

utanzia kuifikirisha hadhira yake. Katika diwani za Kichomi na Dhifa baadhi ya

mashairi yamejenga ukuta imara wa kufikiri kwa wasomaji na kuibuliwa kwa hali ya

jitimai na huzuni. Katika diwani ya Kichomi kuna shairi liitwalo “Kisu Mkononi”

(uk.13) ambalo mwandishi anasema:

Wakati miaka inaibwa mmoja mmoja

Kurudi nyuma, kusimama, kupunguza mwendo

Siwezi, kama gurudumu nitajiviringisha

Mtelemko mkali huu

Lini na wapi mwisho sijui

Mbele chui mweusi, nyuma mwanga

Nionako kwa huzuni vifurushi maelfu ya dhambi

Kisu maisha kafiri haya

Kama kutazama nyuma au mbele

Ni kufa moyo mzima.

Kupitia shairi hili, mwandishi amezungumzia mtazamo wa falsafa ya maisha.

Anaona kuwa, maisha ni adhabu na tanzia anayokumbana nayo mtu mpaka anafikia

hatua ya kujiua. Beti hizo zenye kuibusha hisia za kitanzia zinamtafakarisha

msomaji. Msomaji wa beti hizo anatafakari hatma ya maisha yake na misukosuko

anayokumbana nayo huku akizidi kuwa mnyonge na kutawaliwa na huzuni.

Misukosuko anayoipitia mhusika katika shairi hili kunapelekea msomaji kutafakari

kwa kina namna ya kujikwamua katika hali ngumu anayoipitia mhusika na kufikia

hatua ya kuonesha ni kwa namna gani afanye ili kuepukana na mateso anayoyapitia

mhusika huyo.

Hata katika diwani ya Dhifa mwandishi amemchochea au kuamsha msomaji; hivyo,

anapaswa kufikiria kwa kina ili aweze kubaini ni kitu gani amekusudia kuzungumza.

Katika shairi la “Madomo Mapana” (uk. 7), mwandishi anasema:

Nitafukuzwa mbinguni

Kwa ushairi wangu mbaya

Lakini hata motoni nitaimba

Wanasema

Wanasiasa ni kama jizi

Lililosukumwa mtoto pembeni

Na kunyonya ziwa la mama

Wakati amelala usingizi usiku.

Page 63: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

50

Wanasema

Wanasiasa afapo

Tumejikimboa na domo

Moja pana lizibwalo na mchanga

Na kilima cha simenti ngumu

Lisisikike tena hadharani

Wanasema pia

Kusema haki

Kwa kawaida

Wanasiasa hatuwapendi

Kupiga kura ni hasira ya mkizi

Ni basi tu. Ni Ah!

Ah! Wanamalizia

Nchi mmeifilisi waacheni walimu

Wakajenge taifa jipya

Kama hamwezi kuona mbali

Bure kuweka mkono usoni

Bure kukuna kichwa

Kama hamwezi kufikiri.

Kupitia shairi hili, mwandishi anaelezea hali ya kusikitisha ya wanyonge kutokana

na kuwapo kwa viongozi ambao wanajifikiria wao wenyewe bila kujali maslahi ya

wananchi wanaowatawala. Katika ubeti huu mwandishi anaonesha namna wananchi

wanavyoteseka kutokana na madhila mbalimbali ya viongozi wa mfumo wa kibepari.

Mfumo huo ulioibua hisia za masononeko, majonzi na machungu anayoyapata

mwananchi kutokana ukandamizaji unaofanywa na viongozi. Hapa mwandishi

anamfananisha kiongozi kama jizi linalomsukuma mtoto pembeni ili lipate nafsi ya

kunyonya titi la mama na kumuacha mtoto bila maziwa ya mama yake. Mwananchi

anapompigia kura kiongozi anakuwa na matumaini mapya ya kutatuliwa changamoto

anazozipitia katika mfumo wa utawala lakini inakuwa kinyume na matarajio yake.

Mwananchi anaelezea majonzi na masikitiko aliyonayo baada ya kujikomboa kutoka

kwa wakoloni walionyonya nchi yake. Matarajio makubwa aliyokuwa nayo baada ya

uhuru yalikuwa kuijenga nchi na viongozi kutawala kwa usawa. Mwandishi

ametumia ubunifu mkubwa katika kusana ushairi wake na kupelekea msomaji

kufikiri kwa kina ili kuweza kugundua ni kitu gani alikuwa anakusudia kukisema.

4.3.3 Kujenga Uhalisi wa Maisha

Katika maisha ya mwanadamu kuna furaha na huzuni. Hali hizi mbili ni maarufu

kwa kila mtu hapa ulimwenguni. Ulimwengu umeumbwa na dhana ya uwili, yaani

kila kitu kina cha pili yake. Kwa mfano, kuna usiku na mchana, uhai na kifo, uzima

Page 64: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

51

na ugonjwa, mke na mume, na mrefu na mfupi. Mwendo huo wa maisha umekuwa

ukijitokeza hata katika kazi za fasihi. Utafiti umebaini kuwa kwa kuwa furaha

mwenzake ni huzuni basi si ajabu upande huu wa pili, yaani huzuni, kujitokeza

katika kazi za fasihi. Hii ni kwa sababu fasihi ni zao la jamii na mwanafasihi

anatokana na jamii (Senkoro, 1987). Mwandishi wa fasihi anapoisana kazi yake na

kuweka vionjo vya kitanzia anakusudia kuujenga uhalisi wa maisha yetu ya kila siku.

Hii ni kwa sabababu hapana mtu mwenye furaha au huzuni daima. Hivyo, kupitia

mashairi ya Euphrase Kezilahabi yaliyomo katika diwani zake teule tunaona kuwa

ametumia utanzia ili kuujenga uhalisi wa mwendo wa maisha ya mwanadamu.

Mwandishi ameweza kuonesha dhahiri suala hilo katika diwani ya Dhifa kupitia

shairi la “Kwa Walimu Wote”. Anasema:

Huu utakuwa wimbo wako

Utakapostaafu urudipo nyumbani

Umelewa kangara na nyayo zako

Zikishindwa kulenga njia nyembmba vijijini

Utakuwa kichekesho cha watoto

Watakaokuita, Ticha! Popote upitapo

Kumbuka mwalimu utakapostaafu

Mijusi watataga mayai ndani ya viatu

Vyako vilivyokwisha visigino

Na ndani ya sidiria chakavu

Zilizoshikizwa kamba kwa pini

Mende watazaliana ndani ya chupa tupu

Za marashi na za bia.

Shairi hili linaelezea hali duni ya watumishi wa umma kutokana na ujira mdogo

wanaoupata na changamoto zinazowakabili baada ya kustaafu. Katika ubeti huu

mwandishi ameonyesha hali ya unyonge, huzuni, masononeko na masikitiko

yanayodhihirisha utanzia. Baada ya kustaafu mtumishi anapaswa kupumzika na

kuishi maisha mazuri ya kustaafu; hata hivyo, imekuwa kinyume kwa watumishi

wengi wa umma. Hii inasababishwa na kushindwa kuweka akiba kwa sababu ya

mshahara mdogo anaopokea akiwa kazini. Ugumu wa maisha baada ya kustaafu

unapelekea baadhi ya walimu kuwa walevi ili kupunguza mawazo na changamoto za

maisha wanayoyapitia. Shairi hili limedhihirisha kuwa watumishi wanatumia muda

wao mwingi katika kufanya kazi lakini baada ya kustaafu wanakuwa katika hali

ngumu kimaisha. Hali hiyo ya kushindwa kuyamudu maisha baada ya kustaafu

Page 65: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

52

yanawafanya wawe katika masikitiko, majonzi, machungu hata huzuni kubwa na

kuona kama wamesahaulika.

Hata katika diwani ya Kichomi mwandishi amejenga uhalisia wa maisha aliyoishi

alipokuwa amezaliwa katika kijiji cha Namagondo kwa kuonesha huzuni yake

kutokana na kukosekana kwa mambo yaliyokuwepo hapo zamani. Katika shairi la

“Namagondo” (uk.67), mwandishi anasema:

Nakumbuka Namagondo mahali nilipozaliwa

Ya wapi tena mawele, mawele tuliyopiga

Leo hapa, kesho pale, kesho kutwa kwa jirani?

Viko wapi viazi vitamu vilivyowashinda walaji

Shambani vikajiozea kwa kutokuwa na bei?

Nalilia Namagondo kijiji nilipozaliwa.

Iko wapi tena pamba tuliyovuna kwa wingi

Vyumba vikajaa, watu tukavihama!

Nawakumbuka wanawake wenye nyingi shanga,

Karibu na barabara wakikoga kisimani

Na pembeni, watu wanavuna mpunga

Uko wapi tena mpunga uliokitajirisha watu?

Hapa kwa mzee Mbura, pale kwa mzee Mfunzi

Jiraniye ni Kahunda, pale mzee Magoma

Karibu yake, mzee Nabange, pale mzee Lugina

Sasa wote wamekwenda waliokiongoza kijiji

Miji mingine imevunjika, watoto wajihamia

Wameanza kufarakana kwa kujijengea miji.

Kupitia shairi hili, mwandishi anazungumzia mabadiliko ya mazingira na maisha.

Hali hii inatokana na uharibifu mkubwa uliofanywa wa mazingira uliopelekea

kupungua kwa shughuli za uzalishaji mali kama vile kilimo, uvuvi na biashara.

Katika beti hizo mwandishi ameonyesha hali halisi ya maisha waliyokuwa wanaishi

watu wa Namagondo ambayo kwa sasa hayapo tena. Anaelezea masikitiko, majonzi

na simanzi aliyonayo baada ya kuona vitenga uchumi kama vile kilimo, ufugaji na

uvuvi vilivyokuwa vinawapatia wananchi riziki ya kila siku havipo tena hii ni

kutokana na mifumo mipya ya maisha.

Mawazo ya nadharia ya upokezi yanaumana na mbinu ya utanzia iliyodhihirika

katika diwani teule. Hali hii imetokana na kuwa nadharia hii inahusisha historia na

ujumi au umbuji unaohusiana kwa kiasi kikubwa na dhana ya mkondo wa matarajio,

kwani msomaji huwa na matarajio fulani anapoisoma kazi fulani. Matarajio ya

Page 66: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

53

mhusika katika shairi la “Namagondo” yalikuwa kuona kijiji chake kinapiga hatua za

mbele zaidi na sio kurudi nyuma kimaendeleo. Mwandishi anasononeka

anapowakosa wazee wake kama vile: Mbura, Mfunzi, Magoma, Nabange na Lugina.

Wazee hao walikuwa msaada mkubwa kwa vijana, hasa katika ushauri mbalimbali,

kwa sasa hawapo tena. Hivyo, ni huzuni kubwa kwa waliobaki kwa sababu

wanazikosa hekima na busara zao. Anaonyesha kuwa, kilichokuwepo hapo mwanzo,

kama vile kilimo na uvuvi walivyokuwa wanavitegemea katika kujipatia kipato

havipo tena; bali yamebaki makaburi ya wazee wao tu.

4.3.4 Kuibua Majonzi kwa Hadhira

Utanzia unapotumiwa katika kazi ya fasihi huwa na lengo la kuibua majonzi kwa

wasomaji. Utafiti umebaini kuwa mashairi mengi ya Euphrase Kezilahabi

yaliyotumia mbinu hii ya utanzia yanaibua hisia za majonzi na huzuni kwa wasomaji.

Wafuasi wa nadharia ya upokezi wanaamini kuwa maana ya kazi yoyote ya kifasihi

humtegemea kwa kiasi kikubwa msomaji wa kazi hiyo. Jambo hili linamfanya

msomaji kusawiriwa kama mwenye mchango mkubwa katika kuijaza na kuibua

maana ya kazi inayohusika. Hali hiyo imeweza kudhihirika zaidi katika matukio

yaliyojitokeza katika diwani teule kama vile, ukatili katika mapenzi, ukatili wa

kijinsia, mateso, hali ngumu ya maisha na vifo. Mfano mzuri tunaweza kuuona

katika shairi la “Kwa Walimu Wote” (uk.2) katika diwani ya Dhifa. Shairi hili

limetumia lugha ya moja kwa moja katika kueleza hali halisi ya maisha ya mwalimu.

Limewakumbusha walimu pindi watakapostaafu na namna watakavyokabiliwa na

changamoto za kimaisha kutokana na kutokuwa na uwezo wa kujikimu. Mwandishi

ameibua majonzi na masikitiko kwa walimu kupitia shairi hili na kuwafanya walimu

wawaze maisha yao ya baadaye yatakuwaje. Anasema:

Tazama hilo rundo la madaftari mezani

Utalimaliza kwa mshahara mkia wa mbuzi?

Tuzungumze. Ninyi na mimi

Acha mioyo yenu izungumze

Mkiwa waoga na kujikunja kama jongoo

Mtawekwa kwenye vijiti na kutupwa

Nje ya ua, na ndani mtawaacha

Wacheza ngoma wakitunga nyimbo mpya.

Sikilizeni kwa makini

Umoja hatuna

Twasambaratika kama nyumbu

Tulichonacho ni woga

Page 67: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

54

Na kinachotuangusha ni unafiki

Lakini tusikate tamaa kama mbuni

Tukiupata umoja bado tunayo silaha

Kura.

Hapa, mwandishi ameonesha dhahiri hali duni ya maisha na mazingira magumu ya

kufanyia kazi wanayoipitia walimu kutokana na unyonge pamoja na uoga wao katika

kutekeleza majukumu yao ya kila siku. Mateso, misukosuko, machungu na tabu

wanazopitia za kupata ujira mdogo kwa kufanya kazi ngumu ya kuelimisha jamii

huishia kuishi maisha ya tabu na dhiki. Halikadhalika, baaada ya kustaafu wanaishia

kuwa na maisha duni kwa kuwa wamekata tamaa na wamekosa mtetezi wa

kuwatetea ili kupata haki zao za msingi. Hali ya kukosa umoja na mshikamano ndio

imekuwa chanzo kikubwa cha kushindwa kujikwamua katika changamoto

zinazowakabili.

4.3.5 Kujenga Upekee wa mtunzi

Utumikaji wa mbinu ya utanzia umeweza kuonyesha namna mwandishi anavyoweza

kuwa na mtindo wa kipekee katika kazi yake tofauti na ya mwandishi mwingine.

Upekee huo umeonekana pindi mwandishi anapoelezea jambo lilelile katika namna

tofauti na mwandishi mwingine. Topan (1973) anasema kuwa, mwandishi Euphrase

Kezilahabi hutumia hisi za ndani kueleza maisha na fikra zilizomjaa kichwani kwa

mtungo mpya. Katika kazi za ushairi, hutumia mpangilio wa maneno katika tungo

unaoambatana na mtiririko wa mawazo toka mwanzo hadi mwisho. Hudhihirisha

upekee mkubwa, kutokana na matumizi ya lugha ya picha, mafumbo kejeli na

dhihaka katika tungo zake kwa namna anavyolielezea jambo.

Mwandishi Euphrase Kezilahabi ametumia mbinu ya utanzia katika kazi zake za

ushairi kwa namna ya kuleta taharuki kwa msomaji na kufanya kazi yake kuwa na

upekee, tofauti na waandishi wengine. Mawazo ya nadharia ya upokezi yanaumana

na mbinu ya utanzia kwa sababu humchochea msomaji kujitafutia na kujigundulia

mengi kwa kufumbua ujumbe uliomo katika kazi inayosomwa. Hii ni kutokana

ufundi stadi wa mwandishi katika kutunga kazi yake ya kifasihi. Katika diwani zake

za Kichomi na Dhifa mwandishi ameelezea masuala mbalimbali yanayoonyesha

utanzia na kuleta simanzi, masitikito na kuhuzunisha hadhira yake. Masuala hayo

yameonyesha matukio ya kitanzia kama vile, ukatili, ajali, ugumba au utasa, majanga

au mabaa, magonjwa na vifo vinavyoikumba jamii na kuibua utanzia miongoni mwa

Page 68: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

55

wanajamii. Katika diwani ya Kichomi shairi la “Nimechoka” (uk.34) mwandishi

anasema:

Kati ya vitimbo, vichwa vinazuka ardhini

Ukweli wa masiha unakuwa kama ndoto ya uwongo

Kichwa kimoja kinasema kwa sauti “Mnaliona Hilo!”

Halafu vichwa vyote vyeupe vinacheka. Ninashangaa

Ninashangaa zaidi kusikia sauti ya baba

Ikicheka miongoni mwa vichwa hivyo vyeupe

Siyaamini macho, siyaamini masikio, sikiamini kichwa.

Wanadamu wameinama. Wanasali kwa haraka sasa

Utafikiri wanahesabu mchanga utakaojaza kaburi langu

Vichwa vyeupe vinacheka. Kingine kinasema tena

“Mnaliona Hilo! Joga! Vichwa vinacheka. Wanasali

“Nyinyi nyote hamna akili! Mnaniudhi!

Hamwoni hali yangu! Napiga kelele. Lakini vichwa

Havitishiki, na wanadamu hawatingishiki.

Katika beti hizo tunaona mwandishi ametumia ufundi wa hali ya juu katika kuelezea

falsafa ya maisha inayomkabili mwanadamu na namna anavyoweza kujikwamua.

Shairi hili lina taswira ambazo hujenga falsafa ya mwandishi kuhusu maisha tangu

mwanzo tumwonapo akiwa kafungwa na waya mgumu wa maisha usio na mwanzo

wala mwisho. Vilevile, akining’inia kama ndege aliyenaswa na mtego wa mtoto

mdogo. Picha ya ndege aliyenaswa inadhihirisha wazi falsafa ya maisha yaliyo na

woga na mashaka ambayo chanzo wala mwishowe haujulikani. Mambo yanakuwa

mabaya zaidi, wakati tumwonapo mshairi akishindwa kudondoka kutoka kwenye

waya ngumu kwani chini yake ipo miti iliyochongoka iliyo tayari kumchoma kama

mshikaki. Hali hii inamfanya aamue kuendelea kushikilia waya angali anapata

maumivu makali huku mwili umetapakaa damu na jasho. Hali ngumu ya maisha

imemfanya mtu kuchoka kabisa na kumrudia Mungu ili aweze kumsadia katika

matatizo yake maana wanadamu wenzake hawana msaada tena kwake. Hali hiyo

inapelekea uwezekano wa hadhira kupatwa na hali ya utanzia na kusababisha

masikitiko, machungu na majonzi makubwa.

Vilevile, katika kuonesha upekee katika kazi ya fasihi, mwandishi ametumia ufundi

wa kisanaa kwa kusana kazi ya ushairi. Euphrase Kezilahabi ameonesha umahiri

mkubwa katika kutumia mafumbo, lugha ya picha pamoja na sitiari katika diwani ya

Kichomi kwenye shairi la “Kisu Mkononi” (uk. 13) kwa kuelezea falsafa ya maisha

na kufafanua changamoto zinazomkabili mwanadamu mwandishi anasema:

Page 69: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

56

Mbele chui mweusi, nyuma mwanga

Nionako kwa huzuni vifurushi maelfu vya dhambi

Kisu, maisha kafiri haya

Kama kutazama nyuma au mbele

Ni kufa moyo mzima!

Kupitia shairi hili, mwandishi anafafanua falsafa ya maisha ya mwanadamu pamoja

na changamoto zinazomkabili. Mambo aliyoyaona na kumpata maishani na fikira

zilizomjia kichwani zaelezwa katika shairi hili. Hisi za nadani zimeelezwa katika

mtungo mpya. Mpangilio wa maneno katika tungo unaambatana na kufautana na

mtiririko wa mawazo ya mshairi toka mwanzo hadi mwisho. Nukuu hii inaonesha

namna mwandishi alivyoitumia mbinu ya utanzia katika kuelezea maisha ya

mwanadamu pamoja na changamoto anazozipitia zinazopelekea kutaka kuondoa uhai

wake. Mwandishi anaelezea hisi na mawazo yake hatua kwa hatua kwa kuyaonesha

mawazo ya unyonge ya mwanadamu kwa kutokujua la kufanya wakati maisha

yanamtatiza na kuishia kukata shauri la kujiua na kukumbwa na huzuni, majonzi,

msawajiko na masikitiko makubwa kutokana na kukata tamaa ya kuishi.

4.3.6 Nyenzo ya Kuhuzunisha Hadhira

Utanzia, kama mbinu ya kibunilizi, umetumika katika kazi za mwandishi Euphrase

Kezilahabi ili kuleta taharuki ya majonzi kwa wasomaji wake. Ali (khj) anaeleza

kuwa utumiaji wa mbinu bunilizi ni sehemu mojawapo ya kuteka hisia za wasomaji.

Anaongeza kusema kuwa, kupitia hali ya majonzi, masikitiko na kuwafanya wawe na

huzuni hali hii huchimbuka kutokana na ustadi wa kuyajenga matukio ya utanzia

katika kazi ya fasihi. Nadharia ya upokezi huhusishwa na jinsi kazi au matini fulani

zianavyopokelewa na jamii moja katika vipindi tofauti. Matumizi ya mbinu hii

hamasa yanatoa ya kuelewa baadhi ya mambo mbalimbali yaliyotokea katika jamii

ya Kitanzania, hususani katika fasihi ya Kiswahili. Kuna matukio mbalimbali ya

kuhuzunisha yaliyotokea katika jamii yetu kama vile vifo, njaa, ajali, ulemavu wa

viungo, ukatili, mafuriko na maradhi ambayo imelifanya taifa lipate pengo kubwa

sana lisilozibika. Katika diwani ya Kichomi kuna shairi la “Kumbukumbu 1” na

“Kumbukumbu 2” ambapo mwandishi ameeleza huzuni aliyonayo pindi

alipowapoteza washairi nguli wa fasihi ya Kiswahili ambao waliweka misingi imara

katika uandishi wa kazi za fasihi. Mwandishi anasema:

Nini basi nitakupa? Kitu gani wataka kutoka

Kwangu? Machozi yangu hayana gharama

Page 70: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

57

Yanatoka hata kwa moshi. Inafaa tuonane

Nikuvike taji la ucheshi halafu ikutume

Kwa hiyo basi, nitamtuma maiti anayesema akuite

Nami, kwa nguvu za uchawi wa kishairi

Nitakufufua ukae juu ya kaburi lako

Tuzungumze macho kwa macho

Habari gani Mnyampala? Mbukwa! Mimi

Ni K. bin T. Unayafurahiaje maisha baada ya

Kufa. Wanasemaje malenga wetu. Mwambie Robati

Kwamba yule mzungu amefanya kazi nzuri

Na kwamba siku hizi Waafrika wenyewe

Wameanza kupalilia bustani yake. Mwambie

Kaluta kwamba ule mzozo sasa unajulikana

Na kwamba watu wengi siku hizi hutunga mashairi.

Kupitia shairi hili, mwandishi anaelezea mambo mbalimbali yaliyofanywa na

mashujaa katika kazi za kifasihi. Nukuu hii inaonyesha simanzi, machungu na

masikitiko makubwa aliyonayo mwandishi katika kuelezea hisia zake baada ya

kuondokewa na waandishi wenzie. Mwandishi ametumia kalamu yake katika

kuwakumbuka watunzi mashuhuri waliofanya kazi kubwa katika fasihi ya Kiswahili

na sasa hawapo tena. Kutokana na majonzi aliyokuwa nayo, mtunzi angetamani

kupata nafasi nyingine ya kuwaeleza marehemu Shaaban Robert pamoja na Mathias

Mnyampala kile alichokuwa anafikiria. Hivyo, anaishia kutoa hisia zake kwa

kuandika mashairi kwa ajili ya kuwaenzi na kuonyesha umuhimu wao pamoja na

mawazo yao kuwa bado yanahitajika katika fasihi ya Kiswahili.

4.4 Athari za Matumizi ya Mbinu ya Utanzia

Utafiti umebaini kuwa matumizi ya utanzia katika mashairi ya Euphrase Kezilahabi

yana athari chanya na hasi kama ifuatavyo:

4.4.1 Athari Chanya za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule

Utafiti umebaini athari chanya zifuatazo za utanzia: nyenzo ya kufikisha ujumbe kwa

hadhira, huakisi uhalisi wa maisha, humweka karibu mwandishi na msomaji,

kuitafakarisha hadhira na kumpambanua mtunzi.

4.4.1.1 Nyenzo ya Kufikisha Ujumbe kwa Hadhira

Utanzia ikiwa ni mbinu ya kibunilizi kama mbinu zingine za kisanaa hutumika

kufikisha ujumbe kwa hadhira. Mtunzi wa kazi ya fasihinapoyajenga maudhui yake

ya kitanzia huwa na kusudi la kufikisha ujumbe. Hii ni kwa sababu utanzia

Page 71: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

58

umetumika kama suala la kiujumi ili kurahisisha uelewekaji wa ujumbe kwa jamii.

Langer (1977) anasema kuwa ujumi ni uzuri wa kisanaa au hali ya kutumia ufundi

stadi kwa lengo la kuwavutia wasomaji. Hivyo, mtunzi huweza kutumia mbinu hii

katika kuasa au kuonya jamii. Katika kuthibitisha hilo Mahenge (2020)2 anasema:

Mtunzi Euphrase Kezilahabi ametumia mbinu ya utanzia katika kazi

zake za Dhifa na Kichomi kwa lengo la kufikisha ujumbe kwa

hadhira aliyoikusudia. Kupitia dhamira na migogoro iliyoibuka

katika mashairi yake kumeweza kuleta huzuni na masikitiko kwa

hadhira yake. Lakini lengo la mbinu hizo zilizotumika katika kazi ya

fasihi ni kufika ujumbe uliokusudiwa kwa hadhira.

Maelezo yaliyotolewa yanathibitisha kuwa pamoja na mbinu mbalimbali

zinazotumika katika kusana kazi za kifasihi, mtunzi huwa na lengo kuu la kufikisha

ujumbe kwa jamii husika. Fish (1980) anadai kuwa msomaji anapaswa kusoma kwa

kina kirefu ili kuweza kupata ujumbe ambao mtunzi amekusudia kwa hadhira yake.

Hii ni kwa sababu kusoma kwake kwa kina kunaweza kumfanya agundue maudhui

ya matini hiyo. Katika mashairi ya “Madomo Mapana” na “Ukucha wa Mbwa”,

mwandishi ametoa ujumbe kwa hadhira yake ijapokuwa humuhitaji msomaji kusoma

kwa kina ili kuwaweza kugundua ujumbe aliokusudia mwandishi.

4.4.1.2 Huakisi Uhalisi wa Maisha

Suala la binadamu kukumbwa na huzuni ni la kawaida katika maisha. Mtunzi

anapotumia mbinu ya utanzia huwa na azma ya kuiakisi hali halisi ya maisha. Watu

hufurahi na kuingiwa na majonzi kutokana na mambo tofauti tofauti. Hadhira huiona

mbinu ya utanzia kama nyenzo muhimu ya kuwathibitishia kuwa matatizo na

misukosuko ndio hali ya maisha. Hivyo, kuiandaa jamii kukabiliana nayo. Kama

asemavyo Msigala (2020)3:

Udhihirikaji wa uhalisi wa maisha uliopo katika mbinu ya utanzia

umejitokeza katika kazi za fasihi kupitia wahusika. Kutokana na

matukio ya huzuni, kilio, majonzi na masikitiko yanayoweza

kusababishwa na vifo, vita, ajali, ugumba, ulemavu na majanga

anayoyapitia mhusika, ndivyo vitu vinavyoweza kubeba dhamira

zinazoakisi maisha ya jamii kwa ujumla.

2 Maelezo haya ni ya Dkt. Elizabeth Mahenge, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake tarehe

11/06/2020. Dkt. Mahenge ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu Dar es Salaam. 3 Maelezo haya ni ya Bwana Selestin Msigala, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake 9/06/2020.

Bw. Msigala ni Mhadhiri msaidizi katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Page 72: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

59

Maelezo hayo yanadhibitisha kuwa, mtunzi anapotumia mbinu bunilizi kama utanzia

katika kazi ya fasihi ni wazi kuwa kile anachokiandika kinaakisi jamii fulani. Hivyo,

wafuasi wa nadharia ya upokezi wanaona kwamba kazi ya fasihi ikiakisi uhalisi

huifanya kazi hiyo kuwa na uwazi mkubwa ambao utawezesha kutolewa maana

tofauti tofauti za matini ya kifasihi. Kama inavyodhihirika katika diwani ya Kichomi

kupitia shairi la “Namagondo” (uk. 67) ambapo mwandishi anaelezea huzuni, kilio

na masikitiko aliyonayo mhusika kutokana na mabadiliko yalipo katika kijiji cha

Namagondo. Namagondo ndiyo sehemu ambayo amezaliwa, amekulia na kuishi kwa

muda imebadilika tofauti na awali, hali hiyo ya mabadiliko imemfanya kuona uhalisi

wa eneo hilo haupo tena. Hii imetoka na uharibifu wa mazingira ambao umeleta

mfumo mpya wa maisha na kuondoa uoto wa asili uliokuwepo. Vilevile, katika

diwani ya Dhifa kupitia shairi la “Jibwa” (uk.5) anaakisi maisha halisi ya

ukandamizaji na unyonyaji kwa tabaka la chini. Kutokana mfumo mbaya wa utawala

kumechangia kutokea kwa matabaka mawili katika jamii (walionacho na

wasionacho). Hivyo kupelekea tabaka la chini kuona tabaka la juu kama jibwa lenye

tamaa ya fisi.

4.4.1.3 Humweka Karibu Mwandishi na Msomaji

Mbinu ya utanzia humweka karibu msomaji na mwandishi wa kazi husika. Hii ni

kutokana na uwazi kwamba, masuala yanayojenga utanzia ambayo yanajadiliwa

katika kazi husika huwa ni mambo ya kiulimwengu. Mambo haya kwa namna moja

au nyingine yanahitaji huruma ya watu. Watu husikitika na kusononeka kutokana na

matukio kama ajali, ugumba, majanga, mateso na hata maradhi. Mwandishi

anaposana mambo haya katika kazi yake hujikuta akiiweka karibu hadhira yake, hii

ni kutokana na msomaji kuingiwa na huruma, majonzi na humsikitikia mwandishi au

wahusika waliokumbwa na mikasa yenye utanzia. Kufanya hivyo, husaidia katika

kumfanya msomaji awe karibu naye kila hatua. Kyamba (2020)4 anathibitisha kwa

kusema:

Fasihi ya Kiswahili si ombwe bali inatoka katika jamii. Mwandishi

wa kazi za kifasihi anatunga kazi yake kutokana na yale

yanayoikumba jamii fulani kiuchumi, kisiasa na hata kiutamaduni.

Hivyo, yale anayoandika mtunzi yanatokea katika maisha ya kila

siku na kumfanya kuwa karibu sana na uhalisi uliopo kwenye jamii.

4 Maelezo haya ni ya Dkt. Anna Kyamba, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake tarehe

11/06/2020. Dkt. Kyamba ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Page 73: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

60

Maelezo hayo yanaonyesha namna mtunzi wa kazi za kifasihi anavyoweza kutumia

kalamu yake kuandika kile ambacho kinaikumba jamii na kumfanya kuwa karibu

zaidi na hadhira. Baadhi ya wafuasi wa nadharia ya upokezi wanaamini kuwa, maana

ya kazi yoyote ya kifasihi inamtegemea kwa kiasi kikubwa msomaji wa kazi hiyo.

Jambo hili linamfanya msomaji kusawiriwa kama mwenye mchango mkubwa katika

kuijaza na kuibuni maana ya kazi inayohusika. Hali unamfanya msomaji wa kazi ya

fasihi kuwa karibu zaidi na mwandishi kimawazo kutokana na kuingiwa na huzuni,

machungu hata kupata msawajiko kutokana na kile anachokipitia mhusika katika

kazi hiyo.

Katika diwani ya Kichomi na Dhifa kuna baadhi ya mashairi yanayoonyesha ukaribu

uliopo baina ya mwandishi na hadhira yake. Hii ni kutokana na kuwa masuala

anayoyazungumzia yameweza kuleta chachu kwa wasomaji kufananisha na uhalisi

uliopo katika jamii. Kwa mfano, katika diwani ya Dhifa kwenye shairi la “Kwa

Walimu Wote” (uk. 1) limedhihirisha wazi hali anayoipitia mwalimu baada ya

kustaafu. Mwandishi ametumia ubunifu katika kuelezea jambo hilo ambalo

linawakabili watumishi wengi baada ya kustaafu na kuleta hamasa katika kujiandaa

kabla ya kustaafu.

4.4.1.4 Kuitafakarisha Hadhira

Kwa kawaida utanzia humtafakarisha msomaji. Hii ni kutokana na matukio

yanayosababisha utanzia huwa yanaambatana na ufikiriaji wa hali ya juu. Hadhira ya

kazi ya fasihi huzama katika kufikiri kutokana na matendo yanayozua utanzia.

Katika utafakarishaji huo hadhira huweza kujiepusha au kuchukua tahadhari

kutokana na mambo yanayoleta utanzia kama vile ajali, majanga, kifo, kilio, mateso

n.k. Kimsingi, mbinu hii ni nyenzo muhimu ya kukuza uwezo wa kufikiri kwa

wasomaji wa diwani teule. Suala hili linatokana na ukweli kuwa kufikiri ndio afya ya

akili. Na watu hufikiri kutokana na matendo yanayowakumba katika maisha ya kila

siku. Hivyo, hata utanzia uliomo katika diwani teule hufikirisha hadhira. Thomas

(2020)5 anathibitisha hoja hiyo ya kuifanya hadhira kutafakari anasema:

Mtunzi huwa hatungi kazi ya fasihi kwa kupanga kile anachotunga,

ila msomaji au mhakiki ndio anaweza kupambanua kutokana na

mtazamo wake kulingana na kazi husika. Mwandishi anaweza akawa

5 Maelezo haya ni ya Dkt. Ramadhani Thomas, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake tarehe

9/06/2020. Dkt. Thomas ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Page 74: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

61

amemuathiri msomaji kiuchumi, kimwili hata kisaikolojia bila ya

mtunzi kufahamu hilo. Huenda mtunzi na msomaji au mhakiki wa

kazi ya kifasihi wanaweza kutofautiana kutokana na tafakari ya

msomaji.

Maelezo yaliyotolewa yanadhibitisha kuwa msomaji wa kazi za fasihi ana nafasi

kubwa katika kutafakari na kufafanua kazi ya mtunzi. Iser (1974) na Fish (1980)

wanadai kwamba kazi ya fasihi mara kwa mara ina mapengo mengi. Msomaji au

mhakiki anapaswa kuyaziba mapengo hayo. Kutokana na kuitafakari kazi ya fasihi

msomaji hulazimika kutunga matini mpya ambazo inatokana na matini aliyoipitia

(matini ya asili). Hivyo, msomaji wa kazi ya kifasihi ana jukumu kubwa la kufahamu

kwa kina kazi ya kifasihi. Kila msomaji au mhakiki wa kazi za Euphrase Kezilahabi

anaweza kuchambua kazi hiyo kwa namna alivyoelewa na mtazamo uliomwongoza.

Kama inavyoonekana katika shairi la “Mgomba” (uk. 8) anasema:

Hivyo ndivyo ufalme wa mitara ulivyo

Mti wa mji umelala chini hauna faida tena

Baada ya kukatwa na wafanya kazi

Wa bustani kwa kusita

Chumbani hakuna kitu

Isipokuwa upepo fulani wenye huzuni utingishao

Wenye hila waliokizunguka kitanda na kulia

Machozi yenye matumini yapiga

Mbiu ya hatari ya magomvi nyumbani.

Katika shairi mwandishi anaelezea harakati za ujenzi wa jamii mpya na fikira mpya

juu ya maisha na kuachana na zama za kizamani. Kupitia ubeti huu tunaona

mwandishi anaibua hisia za huzuni, masikitiko na mateso anayoyapata msomaji.

Tunaambiwa kuwa, kuna sauti ya kilio baada ya mhusika kushindwa kutimiza haja

zake za kimwili katika ndoa kwa wake zake, kama anavyosema “hivyo ndivyo

ufalme wa mitara ulivyo”. Hali inaonyesha majuto na masikitiko makubwa aliyonayo

mhusika baada ya kukosa nguvu za kushiriki tendo la ndoa kutokana na umri

mkubwa. Hivyo msomaji wa shairi hili anaweza kutafakari na kuweza kubaini maana

kulingana na uelewa wake binafsi pamoja na mtazamo uliomwongoza.

4.4.1.5 Kumpambanua Mtunzi

Utanzia pia huweza kumpambanua mtunzi kwa kuweza kumtofautisha na waandishi

wengine. Mbinu hii ya kiutunzi huwa ni kipambanuzi kizuri cha mtunzi. Mathalani,

wapo watunzi wamejiegemeza katika maandishi yao kutunga kutokana na hisia

Page 75: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

62

walizonazo na mitazamo yao ambayo huwatofautisha na wengine. Senkoro (1982)

anashadidia hoja hii kwa kusema kuwa mtindo ni upangaji wa fani na maudhui

katika kazi ya fasihi kwa njia ambayo hutokeza nafsi na labda upekee wa mtungaji

wa kazi hiyo. Anaendelea kusema kwamba mtindo hubainishwa kwa vipengele vitatu

ambavyo ni mbinu bunilizi, uteuzi wa maneno na uhusika na wahusika. Fuluge

(2020)6 anafafanua suala la kujipambanua kwa mtunzi kwa kusema kuwa Euphrase

Kezilahabi ametunga kazi zake za ushairi kwa kuteua matukio ya kitanzia kwa

namna ya kipekee tofauti na watunzi wengine. Kutokana na ufundi stadi wake wa

kazi za kifasihi zimedhihirisha msimamo wake kuhusu falasafa ya maisha. Hivyo

msomaji anaweza kumtambua mwandishi kutokana na uelekeo fulani hasa katika

matumizi ya mbinu bunilizi kama utanzia katika kazi husika. Kwa mfano, mwandishi

Euphrase Kezilahabi ameweza kujipambanua kutokana na mtindo wake wa uandishi

wake wa kazi zake zinazoonyesha anguko la mhusika mkuu. Katika kuthibitisha hilo

Topan (1973) katika dibaji aliyoandika kwenye diwani ya Kichomi anaelezea kuwa:

Kezilahabi alifuata mtindo mpya wa kuandika mashairi ya

Kiswahili, na kuleta mtindo mpya wa kutunga mashairi. Shairi la

kwanza lililotumia mtindo huo ni “Kisu Mkononi” (uk.14). Shairi

hili halina vina vya nje na kati, mistari haina mizani zilizopangwa

sare katika kila mstari, wala ubeti hauna mistari sare. Mwandishi

anasema:

Wakati miaka inaibwa mmoja mmoja

Kurudi nyuma, kusimama, kupunguza mwendo

Siwezi, kama gurudumu nitajiviringisha

Mtelemko mkali huu

Lini na wapi mwisho sijui.

Mbele chui mweusi, nyuma mwanga

Nionako kwa huzuni vifurushi maelfu vya dhambi

Kisu maisha kafiri haya

Kama kutazama nyuma au mbele

Ni kufa moyo mzima!

Maelezo yaliyotolewa na Topan yanadhihirisha utofauti mkubwa aliokuwa nao

mwandishi Euphrase Kezilahabi na watunzi wengine wa zama zake. Hali hii

imeonyesha kwa namna ambayo mtunzi aliweza kujipambanua katika kazi zake za

kifasihi. Hapa mwandishi anaelezea hisia alizonazo mtu ambaye amepata

misukosuko katika maisha ambapo tunamuona mhusika ameshika kisu mkononi

6 Maelezo haya ni ya Bwana Adria Fuluge, mahojiano haya yalifanyika jijini Dodoma tarehe

13/03/2020. Bw. Fuluge ni Mhadhiri msaidizi katika Chuo Kikuu cha Mzumbe. Pia ni mwanafunzi wa

Shahada ya Uzamivu katika fasihi ya Kiswahili Chuo Kikuu cha Dodoma.

Page 76: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

63

tayari kwa kujiua. Tukio hilo la kukata tamaa kwa mhusika limeoneshwa na

mwandishi katika namna tofauti ukilinganisha na watunzi wengine. Falsafa ya

maisha anayoonesha mwandishi Euphrase Kezilahabi katika kazi zake inamfanya

ajipambanue na kutambulika kwa wasomaji wake.

4.4.2 Athari Hasi za Matumizi ya Utanzia katika Diwani Teule

Utanzia huweza kuleta athari hasi. Utafiti umebaini athari hasi zifuatazo:

4.4.2.1 Kutopata Wasomaji

Ingawa utanzia ni mbinu ya kibunilizi yenye tija, hata hivyo inapokithiri katika kazi

ya fasihi husababisha kupunguza idadi ya wasomaji. Hii inatokana na ukweli kuwa

katika jamii si watu wote wanaopenda kusoma kazi zenye maudhui ya kusikitisha

kiasi cha kumtoa mtu machozi. Hii ni kwa sababu wasomaji wengi wanapenda

kusoma kazi zinazowaletea furaha, kuwachekesha na kuwaburudisha. Wanapokutana

na kazi zinazowafanya wawe na huzuni, simanzi na masikitiko makubwa, hujikuta

wanakata tamaa. Hali hii inampelekea msomaji wa kazi ya fasihi kulia na kukata

shauri. Badala ya kupambana na tatizo linalomkabili katika maisha yake, huingiwa

na huzuni na kukata tamaa katika changamoto inayomkabili. Mawazo haya

yanafafanuliwa zaidi na Fuluge (2020)7 kwa kusema:

Matumizi ya mbinu ya utanzia katika kazi za kifasihi yanapelekea

uwezekano wa hadhira kupatwa au kutokewa na hisia za kusikitisha

na kuhuzunisha. Hisia hizo zinaweza kumfanya mtu kupata

maumivu, uchungu, majonzi, hofu, jitimai na masikitiko

yatakayopelekea kushindwa kuendelea kusoma kazi hiyo.

Kwa maelezo hayo, tunaona namna kazi ya fasihi inaweza kumuathiri msomaji wa

kazi hiyo na kupelekea kushindwa kuendelea kusoma kazi zenye maudhui ya namna

hiyo. Wamitila (2002) anasisitiza kuwa kuna aina nyingi za wasomaji ikiwemo aina

ya msomaji lengwa na msomaji mwashiriwa. Msomaji anapatikana kutokana na sifa

za ndani au za nje za kazi ya kifasihi. Anaona kuwa ni kawaida kuwasikia waandishi

wa kazi fasihi wakidai kuwa kazi zao zinalenga wasomaji fulani, ingawa kazi

zenyewe zinaashiria wasomaji tofauti kutokana na wasifu wake wa kiumbuji na

kimuundo. Ndipo baadhi ya wasomaji na wahakiki huona kuwa kazi hizo ni kwa ajili

ya kundi fulani na sio wao.

7 Maelezo haya ni ya Bwana Adria Fuluge, mahojiano haya yalifanyika jijini Dodoma tarehe

13/03/2020. Pia Bw. Fuluge ni mwanafunzi wa Shahada ya Uzamivu katika Chuo Kikuu Dodoma.

Page 77: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

64

4.4.3 Ugumu katika Kueleweka kwa Kazi ya Fasihi

Matumizi ya mbinu ya utanzia katika ushairi yanapelekea kusababisha kazi

kutokueleweka kwa wasomaji kwa urahisi. Mbinu hii ya utanzia inachukua muda

kwa msomaji kutafakari kwa kina ili kuweza kuelewa namna mwandishi

alivyoitumia. Hata hivyo, Mohamed (2011) anaunga hoja hiyo kwa kusema kwamba

uelewekaji wa ushairi wa Euphrase Kezilahabi unategemea umahiri wa wasomaji

katika kutambua ishara mbalimbali zinazojengwa kupitia mbinu mbalimbali za

usimulizi. Msomaji wa kazi za ushairi wa Euphrase Kezilahabi kushindwa kuelewa

kazi zake kutokana na kupata maana zaidi ya moja katika mashairi yake. Matumizi

ya mbinu ya utanzia yamepelekea hali ya huzuni, majonzi na simanzi kwa hadhira

pindi wanapofasiri kazi ya mwandishi. Hali hiyo inawafanya hadhira kushindwa

kubainisha kwa urahisi lengo alilokusudia mtunzi katika kazi yake.

Vilevile, Ponera (2014) anasema kazi za Euphrase Kezilahabi husababisha utata

katika kueleweka kwa maudhui na fani aliyoitumia katika kuelezea mambo ya

kusikitisha, kuhuzunisha, kuogopesha na hata kukatisha tamaa. Kutokueleweka kwa

urahisi kwa kazi ya mwandishi kunawafanya wasomaji wa kazi zake kujenga maana

kulingana na upeo wao pamoja na kuhusisha na mazingira yanayowazunguka. Hata

baadhi ya wanafasihi wameshindwa kuzichambua kazi za mtunzi huyu kwa sababu

ya kasumba kuwa kazi zake ni ngumu kueleweka kwa urahisi. Katika kuthibitisha

hoja hii Feruzi (2020)8 anafafanua kwa kusema:

Mwandishi Euphrase Kezilahabi ameweza kuzisana kazi zake katika

ustadi wa juu sana hivyo, msomaji au mhakiki anapaswa kusoma

kwa makini na kwa kina ili kuweza kutafakari yale ambayo

mwandishi ameyaandika. Ndipo ataweza kuelewa kusudi la utunzi

wa kazi hiyo ya fasihi.

Maelezo hayo yanathibitisha kuwa mwandishi Euphrase Kezilahabi ni mtunzi

kwenye kutumia ubunifu wa hali ya juu katika kutunga kazi za kifasihi. Wafuasi wa

nadharia ya upokezi wanaamini kwamba wasomaji wachache wa kawaida ndiyo

ambao wanaweza kuzielewa kazi hizo kwa wepesi. Muumano wa mawazo haya ya

nadharia ya upokezi na mbinu ya utanzia yanadhihirisha kuwa msomaji wa kazi ya

kifasihi anapata ugumu kuielewa kazi hiyo, kutokana na namna ya uwasilishaji wa

dhamira zake kwa njia ya huzuni, majonzi au masikitiko. Hivyo, inahitaji mhakiki au 8 Maelezo haya ni ya Dkt. Abdul Malick Feruzi, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake tarehe

09/03/2020. Dkt. Feruzi ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dodoma.

Page 78: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

65

msomaji wa kazi ya fasihi kusoma kwa kina kazi za kifasihi zilizotumia mbinu ya

utanzia ili kuweza kuelewa alichokusudia mwandishi.

4.4.4 Athari za Utumizi wa Mbinu za Kisanaa kwa Watunzi Wengine

Matumizi ya mbinu za kisanaa kama ufutuhi, kejeli na dhihaka yanaweza kudhihirika

katika kazi za watunzi wakongwe na watunzi chipukizi katika kazi zao. Hivyo,

kuathiri uumbaji wa vipengele vya fani na maudhui za kazi za kifasihi. Euphrase

Kezilahabi, kama waandishi wengine, ameweza kuathiriwa na mbinu hizo

mbalimbali za kibunilizi. Mwakibete (2014) anaeleza kuwa, Euphrase Kezilahabi

amewaathiri watunzi wengine katika mbinu za kisanaa. Baadhi ya watunzi hao ni

Kulikoyela Kahigi; Mugyabuso Mulokozi na Mohamed Said Abdulla katika uumbaji

wa kifani na kimaudhui. Hivyo, kupelekea mfanano mkubwa wa kazi zao na

kufifisha kazi za kifasihi kwa kushindwa kuibua mambo mapya hasa katika mbinu za

kisanaa. Kwa mfano, diwani za Euphrase Kezilahabi zimerandana kwa kiasi kikubwa

na diwani ya “Malenga wa Bara” ya Mulokozi M. M na Kahigi K. K hasa katika

vipengele vya uumbaji wa taswira, lugha ya picha na ishara. Katika kutumia mbinu

hii ya utanzia, hasa katika diwani zake za Kichomi na Dhifa, mwandishi ameonesha

ufundi mkubwa katika kuibua vipengele vya huzuni, masikitiko na jitimai. Katika

diwani ya Dhifa kupitia shairi la “Harusi”, mwandishi anasema:

Waogopao kufa

Hapa

Kuna wimbo:

Yawezekana kinyonga

Na konokono hajawahi

Harusi hata moja na labda hata mazishi

Lakini ingawa wasikia wakinung’unika

Yawezekana pia hakuna binadamu

Anayetaka kuwahi kufa

Hali ikiwa hii

Mwendo wa kinyonga na konokono

Ndio mwendo wa maisha

Haya basi

Tufe tufapo

Tufapo tumekufa.

Katika ubeti wa shairi hili mwandishi ametumia mbinu ya utanzia huku lugha ya

kificho ikitumika kuonyesha mwisho wa maisha ya mwanadamu. Badala ya

kuonyesha shughuli ya kuoa au kuolewa kitu ambacho hufurahisha na sio

kuhuzunisha. Mwandishi ameibua simanzi, kilio na majonzi kwa sababu ameonesha

Page 79: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

66

mwisho wa maisha ya mwanadamu hutokea bila mtu kujua siku wala saa. Culler na

Iser (1976) wanasema kutokana ubunifu wa kutumia mbinu za kisanaa, kaida na

kanuni wanazotumia watunzi katika kazi za kifasihi inapaswa wasomaji wa kazi

hizo, kuwa na umilisi au ujuzi fulani wa kuzitumia kaida hizo. Kwa sababu kaida

hizo zitawezesha wasomaji kuimarisha uzoefu wao katika kupitia kazi za kifasihi

kikamilifu au kutozielewa kabisa kazi hizo. Katika kuunga mkono hoja hiyo

Mapunda9 anathibitisha kwa kusema:

Matumizi ya mbinu ya utanzia kama mbinu zingine bunilizi katika

fasihi ya Kiswahili imesaidia katika kukuza fasihi. Hivyo kuna

maendeleo makubwa katika fasihi ya Kiswahili hasa tunapoona

zikitumika katika tanzu mbalimbali hasa ushairi. Inaonekana

utanzia umejadili zaidi katika tanzu nyingine za fasihi, lakini kwa

sasa tunaona unajitokeza hata katika ushairi.

Maelezo hayo yanadhihirisha wazi matumizi ya mbinu za kibunilizi kama utanzia,

ufutuhi, dhihaka, kejeli na ucheshi sio tu zinatumika katika riwaya na tamthiliya bali

hata katika ushairi wa Kiswahili.

4.4.5 Kukata tamaa

Kukata tamaa ni hali ya kupoteza matumaini juu ya jambo fulani (TUKI, 2013).

Katika kutumia mbinu hii ya utanzia kuna masuala ambayo mwandishi anayaelezea

kwa wahusika wake yanayopelekea kukatisha tamaa. Masuala hayo yanaweza kuwa

kifo, maradhi, mateso, majanga na hata ulemavu yanayowafanya wasomaji wa kazi

za kifasihi kuona maisha hayana maana. Hii inatokana na ukweli kuwa, kazi za

kitanzia mhusika mkuu kufikwa na misukosuko, matatizo au dhiki; wakati mwingine

huishia katika kifo (Wamitila, 2003). Kutokana na kazi za kitanzia kudhihirisha

anguko la mhusika mkuu, ni rahisi kumfanya msomaji kukosa matumaini kabisa.

Hali hii upelekea utanzia unaomvaa msomaji wa kazi ya fasihi kupata funzo

kutokana na anguko la mhusika mkuu. Hivyo kunamfanya aone kuwa hapa duniani

maisha yamejaa misukosuko, pamoja na kukosa tumaini la kuendelea kupambana na

changamoto zinazomkabili.

9 Maelezo haya ni ya Bwana Henry Mapunda, mahojiano haya yalifanyika ofisini kwake tarehe

17/07/2020. Bw. Mapunda ni Mhadhiri msaidizi katika Chuo Kikuu cha Dodoma.

Page 80: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

67

Senkoro (1987) anasema, Aristotle katika andiko lake la Poetics aliwagawa watu

katika pande kuu mbili. Sehemu ya kwanza ni tabaka la juu yenye uwezo wa

kuchanganua mambo ambao wanafaa kusoma kazi za kitanzia. Sehemu ya pili ni

tabaka la chini ambao wana uwezo mdogo wa kufikiri wanafaa kusoma kazi za

vichekesho. Hivyo, tungo za kitanzia zinatoa funzo kwa msomaji wa kazi ya kifasihi

kulingana na namna alivyoweza kuitafakari na kuielewa. Katika kufafanua mawazo

hayo Malugu10 anasema:

Katika shairi la “Kisu Mkononi” linaonesha mateso na misukosuko

anayopitia mtu na kufikia hatua ya kukata tamaa ya maisha. Hali

hiyo inaweza kumpelekea mhusika kukata tamaa mpaka anafikia

hatua ya kuona ni bora kifo kuliko kuishi. Kama inavyodhirika

katika ubeti wa pili (2) mwandishi anasema:

Mbele chui mweusi, nyuma mwanga

Nionako kwa huzuni vifurushi maelfu ya dhambi

Kisu maisha kafiri haya

Kama kutazama nyuma au mbele

Ni kufa moyo.

Maelezo haya yanadhihirisha uwezekano wa hadhira kupatwa na hali ya utanzia

ambayo inaweza kuleta majonzi, masikitiko na huzuni kubwa kwa wasomaji. Katika

kazi za kifasihi mbinu ya utanzia hutumika kuonesha matukio mbalimbali kama vile,

ukatili, kifo, hali ngumu ya maisha, mateso na yanayoelezwa na mwandishi ili

kuibua hisia za woga kwa wasomaji. Atwood (1982) anadai kuwa usomaji ni

mfanyiko na unakubadilisha. Huwezi kuwa mtu yule yule uliyekuwa kabla na baada

ya kuisoma kazi ya kifasihi. Hivyo msomaji wa kazi ya kifasihi anapoisoma kazi

iliyotumia mbinu ya kitanzia anaweza kuathirika kwa kuingiwa na simanzi, majonzi,

masikitiko, kilio na huzuni. Hali hiyo inampelekea kukata tamaa kutokana na

matukio ya kitanzia yaliyodhihirika katika kazi husika ya fasihi.

4.5 Muhtasari wa Sura ya Nne

Sura hii imehusu uwasilishaji na mjadala wa matokeo ya utafiti. Mjadala umehusisha

diwani mbili za Euphrase Kezilahabi ambazo ni Kichomi na Dhifa kwa kuangalia

mdhihiriko wa utanzia, huku ikijielekeza katika kutimiza malengo matatu ya utafiti.

Sura hii imegawanyika katika sehemu tano. Sehemu ya kwanza imeelezea muhtasari

10 Maelezo haya ni ya Bwana Alfred Malugu, mahojiani haya yalifanyika jijini Dodoma tarehe

26/06/2020. Bw. Alfred Malugu ni Mhadhiri msaidizi katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine

Mwanza.

Page 81: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

68

wa diwani teulu. Sehemu ya pili imebainisha matukio ya utanzia ndani ya diwani

teule. Matukio hayo ni hali ngumu ya maisha, kifo, maradhi, majanga, ukatili na

mateso. Sehemu ya tatu imefafanua lengo la pili la utafiti. Katika sehemu hii dhima

anuwai za utanzia zimebainishwa. Dhima hizo ni pamoja na kufikirisha hadhira,

kujenga uhalisi wa maisha, kuhuzunisha hadhira na kujenga hisia za woga kwa

hadhira. Sehemu ya nne imechambua athari chanya na hasi za utanzia kwa wasomaji

kwa kuzingatia misingi ya nadharia ya upokezi katika diwani teule. Tasnifu hii

imebainisha kwamba, wasomaji wa kazi za ushairi za Euphrase Kezilahabi

wameathiriwa waziwazi na uandishi wake kifani na kimaudhui. Athari hizo ni kukata

tamaa, kuibusha majonzi kwa hadhira, ugumu katika kueleweka kwa kazi ya fasihi,

athari za utumizi wa mbinu za kisanaa kwa watunzi wengine na kuitafakarisha

hadhira. Sehemu ya tano imeelezea muhtasari wa sura nne. Sura inayofuata

inafafanua muhtasari, hitimisho na mapendekezo.

Page 82: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

69

SURA YA TANO

MUHTASARI, HITIMISHO NA MAPENDEKEZO

5.1 Utangulizi

Utafiti wetu ulihusu Mdhihiriko wa Utanzia katika Ushairi wa Kiswahili, ambapo

mifano imetolewa katika riwaya mbili za Euphrase Kezilahabi za Kichomi na Dhifa.

Katika sura hii ya mwisho, tumewasilisha muhtasari wa tasinifu, hitimisho na

mapendekezo. Sura imegawanyika katika sehemu tatu. Sehemu ya kwanza inatoa

muhtasari wa tasnifu. Sehemu ya pili ni hitimisho la tasinifu na sehemu ya tatu ni

mapendekezo kwa tafiti zijazo.

5.2 Muhtasari

Tasinifu hii imechunguza matumizi ya utanzia katika mashairi ya Euphrase

Kezilahabi. Utafiti uliongozwa na malengo matatu ambayo ni kubainisha matukio ya

utanzia katika diwani teule, kufafanua dhima za matumizi ya utanzia katika diwani

teule na kuchambua athari za utanzia katika diwani teule. Nadharia ya upokezi

ilitumika katika ukusanyaji na uchambuzi wa data.

Tasinifu hii ina jumla ya sura tano. Sura ya Kwanza ni ya utangulizi wa jumla.

Katika sura hii vimejadiliwa vipengele mbalimbali vya utangulizi. Vipengele hivyo

ni usuli wa tatizo la utafiti, tamko la tatizo la utafiti na malengo ya utafiti. Aidha,

sura hii imebainisha maswali ya utafiti, manufaa ya utafiti na mawanda ya utafiti

pamoja na kuelezea historia fupi ya mwandishi.

Sura ya Pili imebainisha maandiko mbalimbali yanayohusiana na mada ya utafiti.

Maandiko hayo yamegawanywa katika makundi mawili. Kundi la kwanza

limejumuisha maandiko kuhusu dhana ya utanzia, kundi la pili limejumuisha

maandiko kuhusiana na ushairi wa Euphrase Kezilahabi. Pia, sura hii imebainisha

mapengo yaliyojitokeza kutokana na kupitia maandiko. Aidha, katika sura hii

tumefafanua nadharia ya upokezi ambayo ndiyo ilituongoza katika utafiti wetu.

Sura ya Tatu imevifafanua vipengele vya methodolojia ya utafiti. Vipengele hivyo ni

usanifu wa utafiti, eneo la utafiti, walengwa wa utafiti, ukusanyaji wa data, njia na

zana za kukusanyia data na mchakato wa ukusanyaji wa data. Vipengele vingine ni

uchanganuzi wa data, itikeli za utafiti, uhalali na uthabiti wa matokeo ya utafiti na

changamoto za utafiti na utatuzi wake.

Page 83: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

70

Sura ya Nne imehusu uwasilishaji na mjadala wa matokeo ya utafiti. Sura

imegawanyika katika sehemu nne. Sehemu ya kwanza imechambua lengo la kwanza

la utafiti. Sehemu ya pili imechambua lengo la pili la utafiti. Sehemu ya tatu

imechambua lengo la tatu la utafiti wetu na kufuatiwa na muhtasari wa sura ya nne.

Sura ya Tano ina sehemu kuu tatu. Sehemu ya kwanza ni ya muhtasari. Sehemu ya

pili ni hitimisho ambapo tumeeleza kuhusu utoshelevu wa nadharia ya upokezi na

mchango mpya wa tasinifu hii. Sehemu ya tatu inatoa mapendekezo kwa ajili ya

tafiti zijazo.

5.3 Hitimisho

Katika sehemu hii tumejadili utoshelevu wa nadharia iliyotumika pamoja na

mchango mpya wa tasinifu.

5.3.1 Utoshelevu wa Nadharia

Utafiti uliongozwa na nadharia ya upokezi. Kupitia mihimili yake tumeweza

kukusanya na kuchambua data za utafiti wetu. Kwa kiasi kikubwa nadharia ya

upokezi imeweza kutusaidia katika malengo yote matatu ya utafiti huu. Kutumika

kwa nadharia hii katika utafiti huu kumetoa mwanga kwa mtafiti kubaini kuwa ili

msomaji wa kazi ya kifasihi aweze kuzielewa mbinu bunilizi hana budi kuzihusisha

na historia, siasa, uchumi na utamaduni. Euphrase Kezilahabi anajipambanua kwa

kuwatetea wanyonge kupitia ushairi wa Kiswahili kwa kutumia mbinu ya utanzia ili

kukwepa mkono wa dola. Matumizi ya mbinu ya utanzia yalimwezesha mwandishi

kufichua mambo mbalimbali yanayoikabili jamii kwa ujumla.

5.3.2 Mchango Mpya wa Tasinifu

Matokeo ya utafiti huu yameleta upya katika taaluma ya fasihi. Hii ni kwa sababu

tasinifu imeweza kuyabainisha matukio yaletayo utanzia. Pia, tasinifu imeweza

kufafanua sababu za utumiaji wa utanzia pamoja na kuchambua dhima za utanzia

katika diwani teule. Tasinifu hii imebainisha kuwa utanzia ni mbinu inayotumiwa na

washairi katika kujenga maudhui yao tofauti na hapo mwanzo utanzia uliweza

kuonekana kwenye tamthiliya pekee. Pia tasinifu hii imeweza kuonyesha tofauti kati

ya tanzia na utanzia katika kazi za fasihi.

Page 84: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

71

5.4 Mapendekezo kwa Tafiti Zijazo

Kutokana na mipaka ya utafiti wetu kujikita katika malengo matatu na vitabu viwili

vya ushairi vya Euphrase Kezilahabi, tunapendekeza tafiti zijazo zishughulikie

utanzia kwa jicho la kilinganishi baina ya mtunzi mmoja na mwingine ili kuona

kufanana na kutofautiana kwao. Pia, utanzia unaweza kuchunguzwa katika tanzu

zingine za fasihi andishi kama riwaya na tamthilia. Aidha, katika fasihi simulizi ya

Kiswahili watafiti wanaweza kuchunguza na kubaini mbinu hii inavyofanya kazi

hasa katika tanzu za fasihi simulizi kama vile hadithi na semi. Vilevile, pamoja na

wataalamu wengi wa fasihi kujihusisha na utanzia katika tanzu mbalimbali za fasihi,

tunapendekeza tafiti zijazo zishughulikie suala la utanzia katika fasihi ya watoto.

Page 85: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

72

MAREJELEO

Atwood, M. (1982). Second Words: Selected Critical Prose. Canada: House of

Anansi Press.

Acquaviva, G. (2004). “Jazanda ya Njozi katika Baadhi ya Mashairi ya Euphrase

Kezilahabi”. Katika Kiswahili Forum Juzuu 11 uk: 69-73.

BAKITA, (2017). Kamusi Kuu ya Kiswahili. Nairobi: Longhorn.

Chiraka, C. (2011). Tahakiki ya Vitabu Teule: Dar es Salaam: Afro-Plus Publishers.

Cohen, L. na Wenzake (2007). Research Methods in Educational6th Edition. London:

Routledge.

Enon, J. C. (1998). Educational Research, Statistics and Measurements. Kampala:

Makerere University.

Fuluge, A. (2013) “Dhana ya Kujiua katika Kazi za Euphrase Kezilahabi.” Tasnifu

ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya Kiswahili.Chuo Kikuu cha Dodoma

(Haijachapishwa).

Gaudioso, R. (2018). “Mikondo ya Mtiririko wa Kishairi: Mabadiliko ya Ushairi wa

Kiswahili wa Kezilahabi na Mulokozi.” Fasihi, Lugha na Utamaduni wa

Kiswahili na Kiafrika: Kwa Heshima ya Profesa M.M Mulokozi. Dar es

Salaam: TUKI.

___________. (2014). “Kuwako na Wakati: Mipaka ya Lugha kama Hatua za Falsafa

katika Mashairi ya Euphrase Kezilahabi.” Katika Kiswahili Forum Juzuu 21.

Uk: 76-103.

Haji, A. K. (2015). “Matumizi ya Utanzia katika Riwaya teule za Said Ahmed

Mohamed”.Tasnifu ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya Kiswahili.Chuo

Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

Hays, D. G.na Sigh, A. A. (2012). Qualitative Inquiry in Clinical and Educational

Settings. New York: The Guilford Press.

Page 86: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

73

Kaishozi, L. (2012). “Kulinganisha Mitizamo ya maisha kati ya Euphrase Kezilahabi

na Sayyid Abdallah Bin Ali Bin Nassir. Tasnifu ya Shahada ya Umahiri

katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

Kezilahabi, E. (1974). Kichomi: Nairobi: Heinemann Education Books (EA) Ltd.

________. (1988). Karibu Ndani: Dar es Salaam: Dar es Salaam University Press.

________. (2008). Dhifa. Dar es Salaam: Vide-Muwa Publishers Ltd.

King’ei, G. K. na Kisovi, A. (2005). Misingi ya Fasihi Simulizi. Nairobi: Kenya

Literature Bureau.

Kombo, D. K na Tromp, D. L. A. (2006). Proposal and Thesis Writing: An

Introduction. Nairobi: Pauline Publication Africa.

Kothari, C. R. (2004). Research Methodology: Methods and Techniques 2nd Edition.

New Delhi: New Age International Publishers Limited.

Khatib, M. S. (1987). “Washairi wa Kiswahili Wanavyoliona Azimio la Arusha”

katika Mulika Na. 19. Dar es Salaam: TUKI. Kur. 69-73.

Mackeon, R. (1947). Introduction of Aristotle. New York: Randon House.

Malugu, A. (2011). “Suala la Itikadi Katika Riwaya za Euphrase Kezilahabi” Tasnifu

ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma

(Haijachapishwa).

Maxwell, J. A. (2013). Qualitative Research Design: An Interactive Approach.

Calfonia: Sage Publication Inc.

Mazongela, K. S. (2016). “Matumizi ya Utanzia katika Riwaya Pendwa ya

Kiswahili: Ulinganisho wa Riwaya za Ben Mtobwa na Hussein Tuwa”.

Tasnifu ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha

Dodoma (Haijachapishwa).

Page 87: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

74

Mganga, N. A. (2019). “Matumizi ya Ramsa na Tanzia katika Ushairi wa Kiswahili:

Mifano kutoka katika Utenzi wa Al-Inkishafi. Tasnifu ya Shahada ya

Uzamivu katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma

(Haijachapishwa).

Moh’d, H. K. (2016). “Utanzia katika Kasida za Kiswahili: Mifano kutoka Mkoa wa

Mjini Magharibi Unguja.” Tasnifu ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya

Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

Mulokozi, M. (1983). “Uhakiki wa Dunia Uwanja wa Fujo” katika Kiswahili 50/1:1-

12Dar- es- Salaam: TUKI.

_______. (1996). Fasihi ya Kiswahili (OSW 105). Dar es Salaam: Chuo Kikuu Huria

cha Tanzania.

_______. (2017). Utangulizi wa Fasihi ya Kiswahili. Dar es Salaam: KAUTTU

Limited.

Mulokozi, M. na Kahigi, K. (1982). Kunga za Ushairi na Diwani Yetu. Dar es

Salaam: Tanzania Publishing House.

Mwakibete, H. (2014). “Kejeli na Dhihaka katika Mashairi ya Euphrase Kezilahabi:

Sababu za Kutumika na Athari zake kwa Wasomaji”. Tasnifu ya Shahada ya

Umahiri katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma

(Haijachapishwa).

Ponera, A. S. (2019). Misingi ya Utafiti wa Kitaamuli na Uandishi wa Tasinifu.

Dodoma: Central Tanganyika Press.

_________. (2014). “Ufutuhi katika Nathari ya Kiswahili: Ulinganisho wa Nathari za

Shaaban Robert na Euphrase Kezilahabi”. Tasnifu ya Shahada ya Uzamivu

katika Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

__________. (2010). “Ufutuhi katika Riwaya za Shaaban Robert: Dhima, Sababu na

Athari Zake kwa Jamii”. Tasnifu ya Shahada ya Umahiri katika Fasihi ya

Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

Page 88: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

75

_________. (2016). Suala la Matumizi ya Nadharia kama Kiunzi cha Tafiti za

Kitaamuli: Mfano wa Matumizi ya Nadharia ya Ukanivali. Journal of

Humanities, School of Humanities, The University of Dodoma, 3(1), 116–

129.

Prewitt, C. R. (1995). Introductory Research Methodology. African Publication.

Ocassional Paper No. 10. Institute of Development Studies: University of

Nairobi.

Said, Z. (2016). “Usawiri wa Ufungwa katika Riwaya za Kiswahili: Mifano kutoka

katika riwaya za Umleavyo na Haini. Tasinifu ya Shahada ya Umahiri katika

Fasihi ya Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma.

Sanga, A.N. (2018). “Mkengeuko wa Ujumi wa Kiafrika katika Hadithi fupi Andishi

za Kiswahili Kipindi cha Utandawazi: Mifano kutoka Magazeti ya Habari leo

na Nipashe na Mwananchi”. Tasnifu ya Shahada ya Uzamivu katika Fasihi ya

Kiswahili, Chuo Kikuu cha Dodoma (Haijachapishwa).

Semzaba, E. (1997). Tamthiliya ya Kiswahili. Dar es Salaam: Chuo Kikuu Huria cha

Tanzania.

Sengo, T. S. Y. (1992). “Utamaduni wa Kiswahili: Wilaya ya Kusini Unguja” katika

African Studies, Juz. Na. 1, uk 53-79.

Senkoro, F. E. M. K. (2011). Fasihi. Dar es Salaam: KAUTTU Ltd.

_______________. (1988). Ushairi: Nadharia na Tahakiki. Dar es Salaam: Dar es

Salaam Press.

________________. (1987). Fasihi na Jamii. Dar es Salaam: Press and Publicity

Centre.

________________. (1982). Fasihi. Dar es Salaam: Press and Publicity Centre.

Shahid, I. (1980). “Arabic Literature” katika Cambridge History of Islam.Tol.Na.

2B.uk. 657-671. Cambridge: Cambridge University Press.

Page 89: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

76

Soileau, C. (2006). “Money and Tragedy in the Nineteeth- Century Novel”.Tasnifu

ya Shahada ya Uzamivu katika Fasihi Linganishi, Chuo Kikuu cha Lousiana

(Haijachapishwa).

Topan, F. (1974). “Utangulizi” katika Kezilahabi, E. Kichomi. Nairobi: Heinemann

TUKI. (2004). Kamusi ya Kiswahili Sanifu. Nairobi: Oxford University Press.

UWAKI, (2013). “Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii: Mwongozo wa Kisera wa

Sekta ya Afya ya Kuzuia na Kupambana na Ukatili wa Jinsia”. Iliyosomwa

16/07/2020 katika w.w.w.healthpolicyinitiative.com.

Wafula, R.M. na Njogu, K. (2007), Nadharia za Uhakiki wa Fasihi, Sai Industries

Limited, Nairobi.

Wamitila, K. W. (2003). Kamusi ya Fasihi: Istilahi na Nadharia. Nairobi: Focus

Books.

______. (2002). Uhakiki wa Fasihi: Misingi na Vipengele Vyake. Nairobi: Phoenix

Publishing Ltd.

______. (2016). Kichocheo cha Ushairi: Mwongozo wa Uchambuzi wa Mashairi.

Nairobi: Vide-Muwa.

White, B. (2002). Skills for Bussiness Management. London: Penguin Books Ltd.

Page 90: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

77

VIAMBATISHO

A. Miongozo ya Mahojiano na Uchanganuzi Matini

A.1 Mwongozo wa mahojiano kwa Wataalamu wa Fasihi ya Kiswahili

Maswali:

1. Kwa maoni yako, unaielewaje dhana ya utanzia?

2. Je, utanzia huweza kudhihirishwa kupitia vipengele gani?

3. Kuna uhusiano wowote wa utanzia unaojitokeza katika kazi ya fasihi na matukio

ya maisha ya mtunzi? Kama upo, ni matukio gani husawiriwa na utanzia

4. Ni mashairi yapi katika diwani teule za Euphrase Kezilahabi yamedhihirisha

utanzia?

5. Je, mbinu ya utanzia itumikapo katika kazi ya fasihi huweza kuiathiri jamii

katika vipengele gani na kwa vipi?

6. Nini maoni yako kuhusiana na utumiaji wa mbinu ya utanzia katika ushairi wa

Kiswahili?

A.2 Mwongozo wa Uchanganuzi Matini

Uchanganuzi wa matini utashughulika na usomaji wa maandiko mbalimbali

yanayohusiana na mada ya utafiti. Maandiko yatakayodurusiwa ni yale ya maktabani

na kwenye vyanzo vya kielektroniki. Uchanganuzi wa matini katika vyanzo vya

kielektroniki utazingatia vyanzo vinavyohusisha taasisi zinazojulikana na kuaminika.

Mwongozo wa uchanganuzi wa matini unafafanuliwa katika jedwali lifuatalo:

Vyanzo vya Maarifa Vipengele

Vitakavyochanganuliwa

Lengo

Diwani ya Kichomi na

Diwani ya Dhifa

Mashairi, maana, dhana ya

utanzia inayojitokeza

Kuchanganua

matukio ya utanzia,

dhima na athari

zake kwa jamii.

Page 91: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

78

B: BARUA ZA ITHIBATI YA KUFANYIA UTAFITI

Page 92: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

79

Page 93: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

80

C: PICHA MBALIMBALI ZINAZOHUSIANA NA UTAFITI

Picha Na. 1: Mtafiti (kulia) akifanya mahojiano na Dkt. Elizabeth Mahenge wa

Taasisi ya Taaluma za Kiswahili (TATAKI), Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam. Mahojiano haya yalifanyika tarehe 11/06/2020 ofisini kwake

Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

Page 94: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

81

Picha Na. 2: Picha ya Dkt. Abdul Malick Feruzi akiwa na mtafiti (kulia) akifanya

mahojiano ofisini kwake tarehe 09/03/2020, Chuo Kikuu cha

Dodoma.

Page 95: Mdhihiriko wa utanzia katika ushairi wa Kiswahili: Mifano

82

D: TAARIFA ZA WATAFITIWA

Na JINA TAREHE

ZA USAILI

MAHALI PAUSAILI

1. Dkt. Elizabeth Mahenge 11/06/2020 Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam

2. Dkt. Anna Kyamba 11/06/2020 Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam

3. Dkt. Ramadhani Thomas 09/06/2020 Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam

4. Dkt. Abdul Malick Feruzi 09/03/2020 Chuo Kikuu cha Dodoma

5. Bw. Adria Fuluge 13/03/2020 Jijini Dodoma

6. Bw. Alfred Malugu 26/06/2020 Jijini Dodoma

7. Bw. Henry Mapunda 17/07/2020 Chuo Kikuu cha Dodoma

8. Bw. Selestin Msigala 09/06/2020 Chuo Kikuu cha Dar es

Salaam